Friday, October 14, 2016

Wabanguaji wadogo wa Korosho Mtwara walia na Kangomba.


Baadhi ya wanakikundi cha Jipange Cashewnut cha mjini Mtwara wakiwa katika shughuli yao ya uuzaji wa korosho.



Na Juma Mohamed, Mtwara

Wabanguaji wadogo wa korosho wa kikundi cha kina mama cha Jipange Cashewnut Group mkoani Mtwara wako hatarini kusitisha shughuli hiyo inayowaingizia kipato kutokana na serikali mkoani humo kupiga marufuku ununuzi holela wa zao hilo maarufu Kangomba.
Wakizungumza na Juma News, walidai kuwa korosho wanazobangua sasa na kuziuza walizinunua msimu uliopita kwa njia ya Kangomba, lakini kutokana na marufuku ya serikali, na kutokuwa na uwezo wa kwenda minadani kushindana na wanunuzi wakubwa, hawajui watumie njia gani ili wapate korosho msimu huu.
“Yani sasa hivi Kangomba wamepiga marufuku je, sisi serikali inatusaidiaje?..na tusipofanya hivyo sisi mitaji tutapata wapi wenye biashara ndogondogo, maana sisi wengine tuna mitaji midogo hatuna mitaji mikubwa..sisi tunachoomba serikali itusaidie sisi wenye mitaji midogo.” Alisema Zuhura Mfaume.
Bodi ya Korosho Tanzania CBT kupitia kwa makamu mwenyekiti wake Mudhihiri Mudhihiri, ilieendelea kusisitiza kukomeshwa kwa ununuzi wa Kangomba na kwamba yeyote atakayekutwa ananunua kwa njia hiyo akamatwe na kuchukuliwa hatua za kisheria.
Aidha, Mudhihiri alisema Bodi itawasaidia wabanguaji wadogo na tayari wapo katika hatua nzuri ya kuwasajili ili iwe rahisi kuwasaidia kupitia chama chao sambamba na kuwapatia elimu mbalimbali juu ya ubanguaji.

Makamu mwenyekiti wa Bodi ya Korosho Tanzania CBT-Mudhihiri Mudhihiri



“Kwahiyo sisi tumeamua kwenda kwa wabanguaji wadogo hao kuwasaidia shida zao lakini tuliona tukienda kwa mojamoja tutakuwa tunatumbukiza hela mtoni, ndiomana tunawasajili wawe na umoja wao tuweze kutoa elimu kwa urahisi na kuweza kuwafikia kwa misaada kwa urahisi..” alisema Mudhihiri.
Bodi hiyo imetangaza rasmi kuanza kwa minada ya ununuzi wa korosho ambapo kwa mkoa wa Mtwara mnada wa kwanza umefanyika leo Oktoba 14 wilaya za Masasi na Newala, huku jumla ya kampuni 66 zikiwa zimepata leseni za ununuzi ikiwa ni sawa na ongezeko la asilimia 22 kutoka kampuni 54 za msimu uliopita.

No comments: