Monday, April 23, 2012
HII NDIYO SIMBA SC, MNYAMA MKALI ANAYEISHI KATIKATI YA JIJI
Kikosi cha Simba msimu huu |
JIONI hii Simba SC
imeifunga Moro United mabao 2-0 katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania
Bara, na sasa inahita pointi moja tu katika mechi zake tatu zilizobaki ili
kutawazwa rasmi kuwa mabingwa.
Simba wanawavua
ubingwa wapinzani wao wa jadi, Yanga SC ambao msimu huu ‘wamefulia’ kiasi cha
kukosa hata nafasi ya pili, ambayo ingewawezesha kucheza michuano yua Afrika
mwakani.
Ni ukweli usiopingika
kwamba chachandu ya soka ya Tanzania ni klabu mbili kongwe, Simba na Yanga,
ambazo kwa sababu hiyo, zina mashabiki lukuki nchini.
Maelfu ya Watanzania
wanaweza kuziunga mkono timu za majimboni mwao, wilayani mwao, mikoani mwao,
lakini mwisho wa siku wanabakia kuwa na timu ambazo zipo kwenye damu zao, Simba
au Yanga.
Ni kwamba, Tanzania
ina wapenzi wawili tu wa soka, mmoja ni wa klabu ya Simba na mwingine wa Yanga.
Hata wale ambao wamejijengea umaarufu kama mashabiki wa timu fulani, mfano
Yamungu aliyekuwa Reli Morogoro na Mang'ombe aliyekuwa Pamba FC ya Mwanza, nao
pia inadaiwa kuna timu waipendayo miongoni mwa hizo.
Hakuna ubishi, Simba
na Yanga ndiyo maana halisi ya soka Tanzania.
Je, waijua vyema
Simba SC?
Jezi za rangi
nyekundu na nyeupe ndio utambulisho wao dimbani, rangi ambayo inatumiwa na klabu
nyingi kubwa za Ulaya, hususan England, kama Liverpool, Manchester United na
Arsenal.
Unapoizungumzia
Simba, unamaanisha klabu kubwa Tanzania na Afrika kwa ujumla, ambayo ilianzishwa
mwaka 1936, enzi hizo ikijulikana kwa jina la Queens, yaani Watoto wa
Malkia.
Baadaye Simba
ilibadilisha jina na kuwa Eagles, yaani ndege aina ya Tai, kabla ya kuanza
kutumia jina jingine, Sunderland, ambalo lilidumu hadi mwaka 1971
lilipobadilishwa na kuwa Simba.
Wakati huo Sunderland
ilikuwa ina matawi yake, ambayo yalikuwa ni timu za Morning Stars, Canada Dry,
Liverpool na Ilala Stuff, ambako huko mchezaji aliyeonekana kukomaa alipelekwa
kukipiga Sunderland.
Sababu ya kuachana na
jina la Sunderland ni aliyekuwa Rais wa Kwanza wa Zanzibar, Abeid Amaan Karume
(sasa marehemu), ambaye wakati anaweka jiwe la msingi kwa ajili ya ujenzi wa
jengo la klabu hiyo, lililopo Mtaa wa Msimbazi, mwaka huo 1971, alikemea tabia
ya kupenda kuiga mambo ya Waingereza, akiamini kufanya hivyo ni kuendelea
kuutukuza ukoloni.
Rais Karume,
aliwaambia Simba waachane na majina ya kizungu na watumie jina la asili ya
Afrika na ndipo jina la Mnyama tishio zaidi porini, Mfalme wa Nyika, Simba,
lilipowavutia hata ukawa mwanzo wa Simba SC.
Simba ikiwa inaitwa
Sunderland, iliweza kutwaa ubingwa wa Tanzania mara mbili tu, ikiweka rekodi ya
kuwa klabu ya kwanza kutwaa taji hilo mwaka 1965 na kuutetea mwaka 1966 na baada
ya hapo haikuutia tena mikononi hadi ilipobadilishwa jina na kuwa Simba, ndipo
ilipourejesha mwaka 1973.
Simba ilishindwa
kutetea taji lake mwaka 1974, baada ya kuporwa na watani wao wa jadi, Yanga
mwaka uliofuata, kwa kipigo cha mabao 2-1 katika fainali ya kihistoria
iliyopigwa kwenye Uwanja wa Nyamagana, mjini Mwanza.
Adamu Sabu (marehemu)
aliyeingia uwanjani kuchukua nafasi ya Saad Ali, aliifungia Simba bao la
kuongoza, kabla ya Sunday Manara kuisawazishia Yanga na Gibson Sembuli (marehemu
pia) kufunga la ushindi kwa Watoto wa Jangwani.
Ubingwa wa Tanzania
mwaka 1975 kwa mara ya kwanza ulikwenda nje ya Dar es Salaam, ukichukuliwa na
Mseto ya Morogoro, iliyokuwa ikinolewa na kocha maarufu, Mohamed
Msomali.
Simba iliurejesha
ubingwa wake mwaka 1976 na kuutetea kwa miaka minne mfululizo, 1977, 1978, 1979
na 1980. Baada ya hapo, Simba iliyumba na kupoteza makali, kabla ya kuibuka
mwaka 1984 na kutwaa taji hilo. Ililipoteza tena na kulazimika kulisubiri hadi
mwaka 1990, kabla ya kulipoteza na kulitwaa tena mfululizo mwaka 1994 na 1995.
Simba ilitwaa tena taji hilo katika miaka ya 2001, 2003, 2004, 2007 katika Ligi
Ndogo, ikiifunga Yanga kwenye fainali na msimu uliopita.
Ukiachana na utawala
wa Simba katika soka ya Tanzania, kwenye medani ya kimataifa klabu hiyo ndiyo
inayoongoza kwa kuipeperusha vyema bendera ya Tanzania.
Simba ndiyo klabu
pekee iliyoweza kufika Nusu Fainali ya Klabu Bingwa Afrika, mwaka 1974 ikiitoa
timu ngumu ya Ghana katika Robo Fainali, Hearts Of Oak kwa jumla ya mabao
2-0.
Yalikuwa ni mabao ya
Sabu na Abdallah 'King' Kibadeni, Wakenya wakimuita Ndululu kutokana na ufupi
wake, mjini Accra, yaliyoipa timu hiyo ushindi wa 2-0, kabla ya kuja kulazimisha
sare ya bila kufungana mjini Dar es Salaam.
Hata hivyo, baada ya
kushinda 1-0 mjini Dar es Salaam dhidi ya Mehala El Kubra, Simba ilikwenda
kufungwa pia 1-0 na Waarabu hao mjini Cairo, hivyo mchezo kuhamia kwenye mikwaju
ya penalti, ambako Wekundu wa Msimbazi waling'olewa.
Nyota wengine wa
Simba walikuwa ni kipa Athumani Mambosasa, mabeki Shaaban Baraza, Mohamed
Kajole, Athur Mwambeta, Omari Chogo, viungo Khalid Abeid, Willy Mwaijibe,
Haidari Abeid, Abbas Dilunga na washambuliaji Adam Sabu na Abdallah
Kibadeni.
Nyota hao ndio
waliowafunga watani wao wa jadi, Yanga mwaka 1973, baada ya Watoto hao wa
Jangwani kutawala soka ya Tanzania kwa miaka mitano mfululizo, wakichukua
ubingwa wa nchi tangu mwaka 1968 hadi 1972. Hao pia ndio waliotwaa ubingwa wa
Afrika Mashariki na Kati kwa mara ya kwanza mwaka 1974 mjini Dar es
Salaam.
Simba pia ni klabu
pekee ya Tanzania, iliyoweza kucheza fainali ya michuano ya Shirikisho la Soka
Afrika (CAF). Hiyo ilikuwa ni mwaka 1993, ilipofanikiwa kutinga fainali ya Kombe
la CAF, (sasa limeunganishwa na Kombe la Washindi na kuwa Kombe la Shirikisho)
na kufungwa na Stella ya mjini Abidjan, Ivory Coast.
Bahati haikuwa yao
Wekundu wa Msimbazi, kwani baada ya kulazimisha sare ya bila kufungana ugenini,
wengi waliamini kwenye mechi ya marudiano, Stella hawatapona Dar es Salaam,
lakini matokeo yake, wenyeji walilala 2-0 kwa mabao ya Boli
Zozo.
Klabu hiyo pia
ilifanikiwa kuwa ya pili Tanzania kucheza Ligi ya Mabingwa Afrika mwaka 2003,
baada ya Yanga kuwa ya kwanza mwaka 1998. Lakini Simba ilitinga hatua hiyo kiume
zaidi, ikiwatoa waliokuwa mabingwa watetezi, Zamalek ya Misri, kwa mikwaju ya
penalti.
Hiyo ilifuatia
ushindi wa 1-0 mjini Dar es Salaam, kabla ya kwenda kufungwa 1-0 na yenyewe pia
Cairo, lakini mchezo ulipohamia kwenye mikwaju ya penalti, Juma Kaseja, mtaalamu
wa kuokoa michomo hiyo, aliibeba Simba baada ya kucheza penalti
mbili.
Nyota waliokuwa
wakiunda kikosi cha Simba mwaka 2003 ni Juma Kaseja, Amri Said, Said Sued,
Boniface Pawasa, Ramadhan Wasso, Victor Costa, Yusuf Macho, Athumani Machuppa,
Jumanne 'Shengo' Tondola, Emmanuel Gabriel, Steven Mapunda, Madaraka Selemani,
Ulimboka Mwakingwe, Patrick Betwel, Selemani Matola, Amani Mbarouk, Farouk
Ramadhan, Yahaya Akilimali, Primus Kasongo, Abu Amrani, Kevin Mhagama, Majuto
Komu, Lubigisa Edward Lubigisa, Christopher Alex, William John, Emmanuel Kingu,
Edibilly Lunyamila na Clement Kahabuka.
Aidha, Simba pia
ndiyo klabu iliyoweza kutwaa mara nyingi zaidi Kombe la Klabu Bingwa Afrika
Mashariki na Kati, lijulikanalo kama Kombe la Kagame katika miaka ya 1974, 1991,
1992, 1995, 1996 na 2002.
Katika michuano
mingine midogo ya Afrika Mashariki, Kombe la Tusker, Simba tena ndiyo timu
iliyotwaa mara nyingi zaidi taji hilo, mara nne kati ya michuano saba ya Kombe
hilo, katika miaka ya 2001, 2002, 2003 na 2005. Ililikosa mwaka 2006,
lilipochukuliwa na Kagera Sugar, mwaka 2007 lilipochukuliwa na Yanga, mwaka 2008
lilipochukuliwa na Mtibwa Sugar na mwaka 2009, lilipiochukuliwa na Yanga tena.
Asili ya Simba SC
tangu enzi na enzi ni kucheza soka ya utulivu yenye kuburudisha mashabiki wake,
wakitandaza pasi kwa wingi kabla ya kulifikia lango. Imekuwa bahati iliyoje
makocha wote wameendelea kuuenzi utamaduni huo hadi kesho.
Japokuwa imepita
mikononi mwa makocha wengi tangu kuanzishwa kwake, lakini makocha wa kihistoria
na wa kukumbukwa kwenye klabu hiyo ni watano tu, kwanza Paul West Gwivaha (sasa
marehemu), pili Nabby Camara, tatu Abdallah Kibadeni, nne Msomali Enteneh
Esheteh na wa mwisho ni Mkenya, James Siang'a.
Kwa nini hao ndio
makocha wa kihistoria Simba SC?
Wakati Simba inafika
Nusu fainali ya Klabu Bingwa Afrika mwaka 1974, ilikuwa inanolewa na Gwivaha na
wakati inafika fainali ya Kombe la CAF mwaka 1993, ilikuwa chini ya Kibadeni na
Esheteh na mwaka 2003 ilipoitoa Zamalek katika Raundi ya Pili ya Ligi ya
Mabingwa, ilikuwa inanolewa na Siang'a.
Camara, aliyekuwa
raia wa Guinea, atakumbukwa kwa kuvumbua vipaji vya nyota waliowika Simba
baadaye, kama Abbas Kuka, Filbert Rubibira, Nico Njohole na George 'Best'
Kulagwa, kupitia timu ya vijana aliyounda mwaka 1975, baada ya kutua
Simba.
Kwa sasa Simba iko
chini ya kocha wa zamani wa timu ya taifa ya Zambia, Patrick Phiri, ambaye
ameiwezesha kurejesha makali yake, huku mashabiki wa Wekundu hao wa Msimbazi,
wakiwa wana matumaini ya kula raha zaidi chini ya Mzambia
huyo.
Simba SC ipo chini ya
Mwenyekiti Ismail Aden Rage, Makamu Mwenyekiti, Geoffrey Nyange ‘Kaburu’,
Wajumbe sita wa Kamati ya Utendaji, ambao ni Joseph Kinesi, Suedi Mkwabi, Saidi
Pamba, Daniel Manembe, Francis Waya na Ibrahim Masoud. Simba ina watendajiwa wa
kuajiriwa, ambao ni Ofisa Utawala, Evodius Mtawala na Ofisa Habari, Clifford
Ndimbo- wakati meneja wa timu ni Innocent Njovu na daktari ni Cosmass Kapinga.
Rasilimali kubwa za
Simba ni majengo yake mawili pacha yaliyopo Mtaa wa Msimbazi, Dar es Salaam.
Jengo la kwanza la Simba lilijengwa kwa mchango wa Karume na wanachama wa klabu
hiyo wakaongezea fedha na wakashiriki ujenzi, wakibeba, zege, mchanga, kokoto-
yaani vifaa vya ujenzi kwa ujumla na hata kufyatua tofali. Jengo la Simba
lilijengwa chini ya uongozi wa Mwenyekiti Dumelezi na Katibu Mkuu Said
Mpolaki.
Jengo la pili
lilijengwa kwa mpango maalumu wa mkataba na mtu aliyeamua kuwekeza kwenye
kiwanja cha wazi cha klabu hiyo. Mwekezaji aliruhusiwa kujenga na kutumia jengo
kwa biashara zake hadi mwaka 2012 alikabidhi kwa klabu.
Mpango kamili wa
ujenzi wa jengo hilo ulioanzishwa na aliyekuwa Katibu Mkuu wa Simba, Kassim
Mohamed Dewji, ni kuwa na ghorofa nane katika mtindo huo wa makubaliano na watu
wenye nia ya kuwekeza kwenye jengo hilo.
Mwekezaji wa sasa
angeweza kuendelea na ujenzi wa jengo hilo, kama wanachama wa klabu hiyo
wasingefungua kesi mahakamani kupinga zoezi hilo.
Simba SC pia ina
mpango wa kujenga Uwanja wake wa kisasa hivi sasa na tayari Rage
amekwishakaririwa mara kadhaa akizungumzia ujenzi huo- kwamba mipango inaendelea
vizuri ingawa haujaanza.
Pamoja na mafanikio
hayo, Simba imepitia vipindi tofauti, vikiwemo vigumu, wakati ilipokutwa na
misiba ya viongozi na wachezaji wake. Migogoro pia, imekuwa sehemu ya matatizo
ndani ya klabu ya Simba, ingawa kwa upande mwingine hiyo ni demokrasia.
Mbali na majengo
yake, Simba inajivunia udhamini wa kampuni ya Bia Tanzania, kupitia bia ya
Kilimanjaro.
Kilimanjaro imeleta
ukombozi Simba, ambayo ilikuwa inahaha tangu kumpoteza mdhamini wake wa mwisho,
Mohamed Enterprises Limited (MeTL), kampuni inayomilikiwa na mpenzi mkubwa wa
klabu hiyo, Mohamed Gullam Dewji.
Wafadhili wengine wa
Simba, tangu enzi za Sunderland ni mmiliki wa Salama Travel Agency, Saleh Ruwey
ambaye aliwanunulia basi la kwanza, Colt Rosa (sasa halipo tena), Ramesh Patel,
Fakhrudin Amijee, Ally Mwinyi Tambwe na Abdulrahman Muchacho, ambaye alikuwa
akiilisha Simba.
Miaka ya 1990, ndipo
walipoibuka wafadhili wengine kama Azim Dewji, ambaye baadaye aliitema timu hiyo
kutokana na migogoro, japo amebaki mwanachama na anahudhuria mikutano wakati
mwingine.
Mkataba wa awali wa
Kilimanjaro uliokuwa na thamani ya Sh bilioni 3, kila mwaka Simba ilikuwa
inapata Sh bilioni 1, kwa ajili ya shughuli za uendeshaji wa
timu.
Mkataba huo,
ulisainiwa Agosti 18, mwaka 2008, katika hoteli ya Movenpick, mjini Dar es
Salaam.
Kilimanjaro Premium
Lager, ambayo imetoa pia udhamini kama huo kwa Yanga, imekuwa ikiipa Simba Sh
milioni 16, kila mwezi kwa ajili ya mishahara ya wachezaji, hiyo ikiwa ni mbali
na kupatiwa mabasi mawili madogo. Mabasi hayo, moja aina ya Hiace na jingine
Coaster, tayari yamekwisha kukabidhiwa kwa klabu hiyo na yameanza
kutumika.
Aidha, Kili pia
imeweka utaratibu wa kuipa Simba zawadi, iwapo itafanikiwa kushika moja ya
nafasi mbili za juu kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, ikiwa
bingwa itapata Sh milioni 25 na ikishika nafasi ya pili, itapewa Sh milioni
15.
Agosti mwaka jana,
TBL kupitia bia yake ya Kilimanjalo ilisaini mkataba mpya na Simba katika hoteli
ya Double Tree.
Mkataba huo ulioanza
rasmi Agosti 1, mwaka jana utaisha Julai 31, mwaka 2016.
Katika mkataba huo,
Simba watakuwa wanapewa fedha za mishahara kwa mwezi Sh. Milioni 25 kwa mwezi,
watapewa basi jipya la abiria 54, fedha za kuendeshea Mkutano Mkuu wa mwaka,
Shilingi Milioni 20 kwa kwa ajili ya tamasha la kila mwaka, Simba Day, vifaa vya
mechi na mazoezi vyenye thamani ya Sh. Milioni 35 kila msimu, wakiwa mabingwa
watapewa Sh Milioni 25, wakiwa washindi pili Sh. Milioni
15.
Simba, inayojulikana
pia kwa majina ya utani kama Wekundu wa Msimbazi, Mnyama na Taifa Kubwa, imekuwa
ikipewa vifaa vya thamani na vya kisasa vya michezo, lengo likiwa ni kuifanya
iwe bora na mfano wa kuigwa katika ligi hiyo.
Lakini Simba ina
kundi la wapenzi wa klabu hiyo, waliounda umoja wao chini ya Kassim Dewji,
uitwao Friends Of Simba, ambalo linasaidia mno klabu hiyo. Kundi hilo
lililoibuka mwaka 2001, likiwa na watu kama Crescentius Magori, Evans Aveva,
Mulamu Nghambi, Mohamed Nassor, Musley Ruwey, Harrison Mutembey, Jerry Yambi na
wengine, limekuwa likisaidia huduma za timu, usajili na
kadhalika.
Bado kuna watu
wengine mashuhuri nchini, wakiwemo wafanyabiashara na viongozi wa serikali,
ambao kwa mapenzi yao wamekuwa wakiisaidia mno Simba.
Timu hii yenye
mashabiki hadi nchi jirani za Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi, ina sura ya
kitaifa na ina matawi hadi mikoani, bara na visiwani.
Ingawa tathmini
inaonyesha Yanga ndiyo yenye mashabiki wengi zaidi ya Simba, lakini siku za
karibuni ni kama mambo yanaanza kubadilika, kwani kwa vigezo vile vile
vilivyotumika kubaini kuwa Yanga ndiyo yenye mashabiki wengi, Simba nayo
inaonekana kuongeza idadi ya mashabiki wake.
Kigezo kikubwa
kinachotumika ni idadi ya mapato yatokanayo na viingilio vya milangoni, Simba
nayo siku hizi inavutia watu wengi na kutengeneza mapato makubwa, wakati
mwingine kuliko Yanga.
Yote kwa yote,
linapokuja swali nani zaidi baina ya watani wa jadi, ukiachilia mbali mechi
baina ya wababe hao, Simba inaweza kujinasibu ndiyo mbabe, kutokana na rekodi
nzuri katika medani ya kimataifa.
Naam, hao ndio Simba
SC, Wekundu wa Msimbazi, wapeperusha vyema bendera ya nchi kwenye michuano ya
kimataifa.
REKODI ZA
SIMBA:
UBINGWA WA LIGI
KUU:
1965, 1966, 1973,
1976, 1977, 1978, 1979, 1980, 1984, 1990, 1994, 1995, 2001, 2003, 2004 na 2007
(Ligi Ndogo), 2010 na 2012.
LILILOKUWA KOMBE LA
NYERERE:
1984, 1995 na 2000
LILILOKUWA KOMBE LA
MUUNGANO:
1993, 1994, 1995,
2001, na 2002
KOMBE LA TUSKER:
2001, 2002, 2003 na
2005
KOMBE LA CAF:
Ilifika fainali mwaka
1993
KOMBE LA
KAGAME:
1974, 1991, 1992,
1995, 1996 na 2002
LIGI YA MABINGWA
AFRIKA:
Kucheza hatua ya
makundi 2003
KLABU BINGWA
AFRIKA:
Kucheza Nusu Fainali
1974
MABINGWA WA JUMLA
LIGI KUU:
1965 : Sunderland
(Dar es Salaam)
1966 : Sunderland
(Dar es Salaam)
1967 : Cosmopolitans
(Dar es Salaam)
1968 : Yanga
1969 : Yanga
1970 : Yanga
1971 : Yanga
1972 : Simba
1973 : Simba
1974 : Yanga
1975 : Mseto SC
(Morogoro)
1976 : Simba
1977 : Simba
1978 : Simba
1979 : Simba
1980 : Simba
1981 : Yanga
1982 : Pan African
1983 : Yanga
1984 : Simba
1985 : Yanga
1986 : Tukuyu Stars
(Mbeya)
1987 : Yanga
1988 : Coastal Union
(Dar es Salaam)
1989 : Yanga
1990 : Simba
1991 : Yanga
1992 : Yanga
1993 : Yanga
1994 : Simba
1995 : Simba
1996 : Yanga
1997 : Yanga
1998 : Yanga
1999 : Mtibwa Sugar
(Morogoro)
2000 : Mtibwa Sugar
(Morogoro)
2001 : Simba
2002 : Yanga
2003 : Simba
2004 : Simba
2005 : Yanga
2006 : Yanga
2007 : Simba (Ligi
Ndogo)
2008 : Yanga
2009: Yanga
2010: Simba
SC
2011: Yanga
SC
2012: Simba
SC
SIMBA SC BINGWA 2012
Msimamo Ligi Kuu ya Vodacom
TAN
Nafasi | Timu | MP | W | D | L | GF | GA | +/- | Pts | |
---|---|---|---|---|---|---|---|---|---|---|
1 | Simba SC | 25 | 18 | 5 | 2 | 42 | 12 | 30 | 59 | |
2 | Azam | 23 | 15 | 5 | 3 | 34 | 11 | 23 | 50 | |
3 | Young Africans | 24 | 15 | 4 | 5 | 38 | 21 | 17 | 49 | |
4 | Mtibwa Sugar | 23 | 10 | 5 | 8 | 31 | 25 | 6 | 35 | |
5 | Coastal Union | 24 | 10 | 2 | 12 | 24 | 29 | -5 | 32 | |
6 | Kagera Sugar | 24 | 7 | 10 | 7 | 25 | 25 | 0 | 31 | |
7 | JKT Ruvu | 24 | 7 | 10 | 7 | 25 | 30 | -5 | 31 | |
8 | Ruvu Shooting | 24 | 7 | 9 | 8 | 20 | 19 | 1 | 30 | |
9 | JKT Oljoro | 23 | 7 | 8 | 8 | 16 | 20 | -4 | 29 | |
10 | Toto African | 24 | 5 | 11 | 8 | 23 | 27 | -4 | 26 | |
11 | African Lyon | 24 | 5 | 8 | 11 | 20 | 29 | -9 | 23 | |
12 | Villa Squad | 24 | 6 | 5 | 13 | 26 | 43 | -17 | 23 | |
13 | Moro United | 25 | 3 | 10 | 12 | 27 | 44 | -17 | 19 | |
14 | Polisi Dodoma | 25 | 3 | 8 | 14 | 18 | 34 | -16 | 17 |
No comments:
Post a Comment