Saturday, July 30, 2016

Mtwara kuanza Oparesheni ya ukaguzi wa vyoo nyumba kwa nyumba.



Naibu waziri wa Mazingira, Mhe. Luhaga Mpina, akiwa na katibu tawala wa mkoa wa Mtwara, Alfred Luanda na mkuu wa wilaya ya Mtwara, Dkt. Khatib Kazungu katika ziara ya kukagua Jalala la kuhifadhi taka ngumu la manispaa ya Mtwara Mikindani.

Naibu waziri wa Mazingira, Mhe. Luhaga Mpina, akiwa katika ukaguzi wa Jalala la kuhifadhi taka ngumu la manispaa ya Mtwara Mikindani, lililopo Mangamba. Kushoto ni mkuu wa wilaya ya Mtwara, Dkt. Khatib Kazungu.



'Tunakagua ubora wa Jalala'


Na Juma Mohamed, Mtwara.

Serikali imeutaka mkoa wa Mtwara kuendesha oparesheni ya nyumba kwa nyumba kukagua vyoo kwa kila kaya, na kwamba kaya itakayobainika kukosa choo itapigwa faini pamoja na usimamizi mkali kuhakikisha choo kinajengwa mpaka kinakamilika.
Naibu waziri wa ofisi ya makamu wa Rais Muungano na Mazingira, Mhe. Luhaga Mpina alitoa maagizo hayo mbele ya katibu tawala wa mkoa huo Alfred Luanda na msaidizi wake anayeshugulika na maji na mazingira Rejea Ng’ondya, baada ya kupewa taarifa ya mazingira ya mkoa inayosema zaidi ya kaya elfu ishirini na tano hazina vyoo.

Choo cha shule ya msingi Maendeleo, manispaa ya Mtwara Mikindani.


“Na hii oparesheni ifanyike ‘immediately’ ya kuzipitia hizi familia kwasababu hizi familia ambazo zinazungumzwa hazina vyoo zina wanaume wana nguvu kabisa na wanaamka wanakula na wanaenda kutembea wanaenda kudhurula, tutakachofanya ni oparesheni kubwa mnafika pale mnawapiga faini alafu mnawasimamia wanajenga choo mpaka kinaisha..” alisema.
Aidha, naibu waziri huyo imeitaka manispaa ya Mtwara Mikindani kuhakikisha wanakamilisha mradi wa ujenzi wa Jalala la kisasa la kuchakata taka lililopo Mangamba ifikapo mwezi Agosti mwaka huu.
Awali, akitoa taarifa ya mazingira ya mkoa, katibu tawala msaidizi anaeshughulika na Maji na Mazingira, Rejea Ng’ondya, alisema kaya ambazo hazina vyoo ni zaidi ya 25,000 ambazo ni sawa na asilimia 6 huku akikiri kuwa changamoto hiyo ipo kwa kiasi kikubwa katika mikoa ya Pwani.

Naibu waziri wa Mazingira, Mhe. Luhaga Mpina akiwa katika ziara ya kukagua soko la halmashauri ya mji wa Masasi. Wapili kushoto ni mkuu wa wilaya ya Masasi Seleman Mzee.


 Naibu waziri huyo amehitimisha ziara yake ya siku tatu mkoani humo kwa kuwaongoza wananchi wa wilaya ya Masasi na maeneo jirani katika kushiriki zoezi la usafi wa mazingira linalofanyika kila Jumamosi ya mwisho wa mwezi nchini kote.

Naibu waziri wa Mazingira, Mhe. Luhaga Mpina akikagua samaki katika soko la halmashauri ya mji wa Masasi, ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kikazi katika wilaya ya Masasi.

 
Aidha, pamoja na kutoa pongezi kwa wananchi hao kuhamasika kwa kiasi kikubwa kufanya usafi, amewataka viongozi wa mitaa na vijiji kuhakikisha wanasimamia vyema sheria za mazingira na kutosita kuwachukulia hatua wachafuzi wa mazingira na wanakwepa kufanya usafi.


No comments: