Friday, July 29, 2016

Dangote Mtwara wapigwa faini kutokana na uchafu wa mazingira.




Lango kuu la kuingilia ndani ya kiwanda cha Saruji cha Dangote Industries Limited, Mtwara.




Eneo la nje ya kiwanda cha Saruji cha Dangote.


Mazingira hayaridhishi, nje ya kiwanda cha Saruji cha Dangote.



Na Juma Mohamed, Mtwara.

Baraza la Taifa la Udhibiti na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kanda ya kusini limekitoza faini ya shilingi Milioni 15 kiwanda cha Saruji cha Dangote Industries Limited cha mkoani Mtwara kutokana na uzembe wa utunzaji wa taka ngumu za viwandani.
Mratibu wa NEMC kanda ya kusini, Lewis Nzari, amesema uongozi wa kiwanda hicho unatakiwa kulipa faini hiyo ndani ya wiki moja, ambayo imetokana na kiwanda kuwa katika mazingira machafu ya taka ngumu pamoja na kukosekana kwa choo nje ya kiwanda kwa matumizi ya madereva na makondakta.
Hatua hiyo imekuja kutokana na ziara ya waziri wa nchi ofisi ya makamu wa Rais Muungano na Mazingira, Mhe. Luhaga Mpina, ambaye alifika kiwandani hapo huku pamoja na mambo mengine alibaini kuwapo kwa uchafu ndani nan je ya kiwanda hicho.
“Kwahiyo tunawapiga faini kama fundisho na kuwakumbusha ili wengine wawekezaji wengine wasije wakafanya kosa kama hili, faini ya shilingi za Kitanzania sh. Milioni 15..” alisema Nzari.

Ziara ya Naibu waziri wa Mazingira, Mhe. Luhaga Mpina ndani ya kiwanda cha Saruji, Dangote Industries Limited.



Kwa upande wake,naibu waziri alisema pamoja na faini hiyo, uongozi wa kiwanda unatakiwa kuhakikisha ndani ya wiki mbili wanakamilisha ujenzi wa choo katika eneo la kuegesha malori pamoja na kuhakikisha mazingira yanakua masafi wakati wote.
“Suala la kujenga vyoo hatuwezi kuwaruhusu mwezi nzima, kwa maana ya wiki mbili lazima vyoo view tayari vimejengwa na vinatumika, sasa hili lingine wameshatoa maelekezo na sitaki kulirudia lakini meseji ni hiyo kwamba choo kikamilike ndani ya siku 14 na malipo hayo ya faini yafanyike ndani ya siku saba..” alisema.
Aidha, ameagiza uongozi kuhakikisha wanakuwa na afisa mazingira wa kiwanda, ambaye pamoja na majukumu mengine atasaidia kushauri mambo mbalimbali yakimazingira kiwandani hapo.
Kabla ya maagizo hayo, naibu waziri alitoa nafasi kwa madereva wa malori yanayobeba Saruji hiyo, kueleza changamoto zao ambazo zilijikita katika kulalamikia kukosa huduma ya choo.

Naibu waziri wa nchi ofisi ya makamu wa Rais Muungano na Mazingira, Mhe. Luhaga Mpina, akizungumza na maofisa wa Baraza la Udibiti na Usimamizi wa Mazingira Tanzania-NEMC kanda ya Kusini, wakiwa katika ziara ya kikazi katika kiwanda cha Saruju cha Dangote Mtwara.



“Kero kubwa sisi madereva tunajisaidia kwenye mapori humo, kwahiyo mtusaidie, sasa mtu umekosa choo utaenda wapi, hapa (Mlango wa kuingilia ndani ya kiwanda) huruhusiwi kuingia kama hauhusiki..kwahiyo kitu kikubwa unachukua kopo lako na maji unakwenda maporini..” alisema Khamis Juma.
Mkuu wa idara ya utumishi na utawala wa kiwanda hicho, Kajiri James, alijaribu kuomba radhi kutokana na faini hiyo lakini hakuweza kukubaliwa, hivyo kuridhia kulipa kutokana na maagizo yaliyotolewa.
“Ni jambo ambalo linasikitisha kwamba katikati ya juhudu zote ambazo tunazifanya tunajikuta tunawekewa hiyo adhabu..labda pia kwa heshima tu niombe adhabu isitishwe ili tupatiwe muda na kupata fedha zaidi na kuweza kuendelea kumalizia shughuli ambazo tumepewa.”  Aliomba Kajiri.
Alisema kilichotokea ni bahati mbaya ambayo haikutarajiwa huku akitaja kwamba walikuwa wakikabiliwa na baadhi ya changamoto ikiwa ni pamoja na kucheleweshewa vibali vya kuruhusu ujenzi.



No comments: