Monday, May 23, 2016

Wanafunzi sekondari ya madimba mtwara hatarini kusomea chini ya miti.


Wanafunzi wa shule ya sekondari ya Madimba, halmashauri ya wilaya ya Mtwara wakiwa darasani huku wakikalia mbao zilizo juu ya matofali kutokana na uhaba wa madawati.



Juma Mohamed, Mtwra.

WANAFUNZI wa shule ya sekondari ya kutwa ya Madimba halmashauri ya wilaya ya Mtwara, wako hatarini kusomea chini ya miti kutokana na shule yao kukabiliwa na uhaba wa vyumba vya madarasa hali inayopelekea wasomee kwenye vyumba vya Maabara ambavyo bado havijakamilika.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti shuleni hapo, walisema kwa sasa wanalazikia kutumia vyumba vya Maabara ambavyo ujenzi wake unatarajiwa kukamilika muda mfupi ujao jambo ambalo litawafanya wakose mahala pakusomea.
“Hii hapa ni Maabara sasa ikiisha sisi tutasomea chini ya Mikorosho, na chini ya mikorosho kuna jua sasa tutasomea wapi wakati chini ya mikorosho kuna jua?..mvua nayo itachangia, inamaana kwa kifupi hatuna sehemu ya kusomea endapo hii maabara itaisha..tunaiomba itujengee madarasa ya kutosha na itujengee bweni kwa ajili wengine tunatoka mbali..” alisema Kamilu Chilolo na kuongeza;
“Kipindi kama hiki wanyama wakali wabaya, watu wanaweza wakawabaka wasichana..tunaomba watujengee bweni ambalo litatusaidia sisi kusoma kwa urahisi na kufaulu mitihani yetu..” aliongeza.
Naye, Amina Mohamed, aliiomba serikali kuwajengea madarasa pamoja na kuongeza juhudi katika ujenzi wa maabara ili waweze kusoma vizuri masomo ya sayansi ambayo yanahitaji vitendo zaidi ili kuwajengea uwelewa.
Mkuu wa shule hiyo, Ahmad Kwerendu, alisema licha ya uhaba wa vyumba vya madarasa, changamoto nyingine wanazokabiliana nazo ni ukosefu wa ofisi za walimu pamoja na nyumba za walimu ambapo ipo moja ya mkuu wa shule ambayo hata hivyo analazimika kukaa na baadhi ya walimu wengine.
Mkuu wa mkoa wa Mtwara, Halima Dendego, alimwagiza mwenyekiti wa kijiji cha Madimba, Mohamed Madiva, kuwahamisha wananchi wake kushiriki katika zoezi la kufyatua matofali yatakayosaidia kutatua changamoto za miundombinu shuleni hapo ikiwa ni pamoja na ujenzi wa nyumba za walimu.
Dendego alifanya ziara ya kikazi shuleni hapo kwa ajili ya kukagua miradi ya maendeleo pamoja na kusikiliza kero na kupokea maoni ya walimu katika shule hiyo ambayo huu ni mwaka wa tatu toka kuanzishwa kwake.
Ikumbukwe kuwa kata ya Madimba ndiko ambako kuna mradi mkubwa wa kiwanda cha kuchakata gesi asilia ambao tayari umeshaanza uzalishaji ukizinduliwa na Rais wa awamu ya Nne Mhe. Jakaya Kikwete mwezi Oktoba mwaka jana.


No comments: