Wednesday, November 4, 2015

Wasomea chini ya miti kwa kukosa madarasa-Mtwara vijijini

Wanafunzi wa shule ya msingi Nanyati, kata ya Mkunwa, halmashauri ya Mtwara vijijini, wakiwa chini ya mti ambako ndipo wanaposomea kutokana na kukosa madarasa huku wengine wakiwa wamekaa chini kwa kukosa madawati, wakimsikiliza mwalimu wao, Shaibu Hoja.


Wanafunzi wa shule ya msingi Nanyati.



Wanafunzi wa shule ya msingi Nanyati.






Na Juma Mohamed.

WAKATI Halmashauri ya wilaya ya Mtwara vijijini mkoani hapa ikijidai kwa mafanikio ya kuongoza kimkoa katika matokeo ya mtihani wa darasa la saba, baada ya kutoa shule tatu bora, wanafunzi wa shule ya msingi Nanyati, kata ya Mkunwa katika halmashauri hiyo wanalazimika kusomea chini ya mti kutokana na kukosa madarasa.
Shule hiyo iliyoanzishwa miaka mitatu iliyopita ambayo ina jumla ya wananfunzi 210 kuanzia darasa la awali mpaka la tatu, inakabiliwa na changamoto lukuki huku zaidi ikiwa ni vyumba vya madarasa ambapo kuna chumba kimoja kinachotumiwa na wanafunzi wa darasa la pili huku wale wa awali na darasa la tatu wakisomea chini ya mti.

Mwalimu mkuu wa shule ya msingi Nanyati, Shaibu Hoja, akielezea changamoto zinazoikabili shule hiyo

Akizungumza na Nipashe shuleni hapo, mwalimu mkuu wa shule hiyo, Shaibu Hoja, alisema changamoto nyingine zilizopo ni uhaba wa walimu ambapo mpaka sasa shule ina walimu wawili wa serikali na mmoja wa kujitolea, jambo ambalo linapelekea wanafunzi kukosa masomo inapotokea mwalimu mmojawapo amepatwa na dharula ya kutohudhuria kazini kwa muda Fulani.
Alizitaja changamoto nyingine, kuwa kukosa vyoo, nyumba za walimu, ofisi za walimu pamoja na ukosefu wa madawati ambapo yaliyopo ni madawati 26 huku shule ikihitaji madawati 88.
Alisema, kwa kukosa madarasa, wanafunzi wanakuwa katika mazingira magumu ya kupata masomo hasa kinapofika kipindi cha mvua kwasababu wanalazimika kukimbia kueudi nyumbni kwao na kukatisha masomo.
“Mpaka sasa shule ina madarasa matatu pamoja na la awali na kufanya idadi ya madarasa manne, lakini sasaivi shule ina chuma kimoja tu kilichokamilika na kingine bado hakija kamilika..tunaongea huu ni mwezi wa 11, Januari tunataka kuanza darasa la nne lakini chumba kilichokamilika ni kimoja, inamaana madarasa manne yatakua nje hayana mahala pakusomea..changamoto yatatu ni ukosefu wa madawati, kwani nilitonayo ni 26 tu na ninahitaji nipate madawati 88..” alisema.
Na kuongeza, “ile changamoto ya kukosa madarasa imechukua nafasi ya kwanza kwasababu wanafunzi wanasomea chini ya miti, wanasumbuliwa na mvua, jua kali, wanapata maumivu ya vichwa kwa kukaa maeneo yanayopitisha jua, wanaloa maji na mvua inaponyesha na shule inafungwa siku hiyo hata ikiwa siku tatu hakuna shule..” aliongeza.
Aliziomba serikali za kijiji na halmashauri ya wilaya kushughulikia kero hizo kwa haraka ili kuwaokoa wanafunzi hao kuondokana na vikwazo hivyo katika kujitafutia elimu.
Wanafunzi wa shule hiyo, wameitaka serikali kuwatatulia changamoto hizo ambazo wamezitaja kuwa ni kikwazo katika safari yao ya kujipatia elimu kutokana na muda mwingi kukosa masomo hasa pale inaponyesha mvua na inapotokea mwalimu mmoja amekosekana.
“Tupate viwanja vya mpira, tupate madarasa, tupate madawati..wanafunzi wengi wanakaa chini, tunasomea chini ya mkorosho, uandikaji wetu ni wa matatizo na mvua inatunyeshea na tunarudi nyumbani tunakosa masomo..mwalimu akimwa tunafunga shule tunakosa kusoma, mimi inaniuma sana..” alisema Asha Selemani, mwanafunzi wa darasa la tatu.
Nao, wananchi wa kijiji hicho ambao nguvu zao kwa pamoja ndio zimefanikisha ujenzi wa shule hiyo, wameitaka serikali kuwasaidia kuboresha miundombinu ya shule na kuongeza eneo kwa kuwahamisha wananchi wanaoishi kuizunguka sule hiyo.
“Pia serikali tunaiomba itujengee choo cha kudumu kwa ajili ya wale watoto kwasababu tulichonacho ni cha muda mfupi..pia itupatie walimu wakutosha kwasababu hatukuanzisha ile shule iwe kwa ajili ya wanakijiji pekee, na tunawapokea watoto kutoka vijiji jirani wanaokuja kusoma hapa.” Alisema Issa Chonga.
Naye, Fidea Chiponde, ambaye ni wenyekiti wa kamati ya shule, alisema shule inamahitaji katika sehemu mbalimbali, ikiwa ni pamoja na waalimu ambao wanahitajika wapatao wanne, madarsa matano, matundu manane ya vyoo pamoja na nyumba saba za walimu, huku wakkabiliwa na changamoto nyingine ya ukosefu wa vitendea kazi.

Mwenyekiti wa kamati ya shule ya msingi Nanyati, Fidea Chiponde, akielezea changamoto za shule hiyo.

Alisema bado hawajapata msaada kutoka serikalini ukiachiliambali fedha sh. Milioni 3 kutoka halmashauri ambazo zilitumika katika ujenzi wa darasa moja ambalo hata hivyo bado halijakamilika, pamoja na msaada uliotolewa na mbunge wa jimbo la Mtwara vijijini, Mhe. Hawa Ghasia, ambaye alichangia mabati 100.
Katika hatua nyingine, wakazi wa kijiji hicho wanakabiliwa na ukosefu wa Zahanati kiasi cha kulazimika kusafiri umbali mrefu wa hadi km 5 kufuata huduma hiyi inayopatikana kijiji jirani na kupelekea baadhi ya kina mama wajawazito kujifungulia majumbani mwao.

Afisa mtendaji wa kijiji cha Nanyati, akizungumzia kero za kjijini hapo zinazowakabili wananchi

Mtendaji wa kijiji hicho, Hassan Mohamed, alisema anapata malalamiko mara kwa mara kutoka kwa wananchi wake juu ya hadha wanayoipata kutokana na ukosefu wa huduma hiyo ambayo inapatikana katika kijiji cha Kawawa.
Alisema, wadau wa afya waliwahi kutembelea kijijini hapo na kutaka kujua jamii imefikia wapi katika jitihada za kuanza kutatua tatizo hilo ambapo waliambiwa kuwa tayari limepatikana eneo kwa ajili ya ujenzi lakini imeshindikana kuanza kwa wakati kutokana na kutatua kero ya elimu ambayo bado inategemea nguvu za wananchi.


Kaimu mkurugenzi wa halmashauri ya Mtwara vijijini, Tamimu Komba, akifafanua juu ya changamoto zinazolalamikiwa na wakazi wa Nanyati kuhusu huduma za kijamii.


Kwa upande wake, kaimu mkurugenzi wa halmashauri hiyo, Tamimu Kambona, ambaye pia ni afisa elimu shule za msingi, akizungumzia changamoto za shule, alisema wanazo taarifa juu ya shle hiyo na kwamba tatizo lililokwamisha ujenzi wa madarasa ni kutokana na kuwekeza nguvu nyingi katika ujenzi maabara ambao ulitiwa mkazo na mkuu wa mkoa kwa kutekeleza agizo la Rais Jakaya Kikwete.
Alisema juhudi zinafanyika katika kutekeleza ujenzi wa shule hiyo, ambapo bajeti ya mwaka 2015/2016 yatatekelezwa hayo ikiwa ni pamoja na ujenzi wa vyoo unaotegemewa kutekelezwa kupitia wafadhili wanaoshughulikia katika sekta hiyo.
“Makusanyo ya mwaka jana mengi yalikimbilia katika ujenzi wa maabara, tulishindwa kukamilisha lile, lakini nafikiri kwa mwaka huu sasa nguvu yetu tutaielekeza huko baada ya kukamilisha maabara..kuhusu suala la walimu ni kweli kuna walimu wawili, na ikitokea mmoja ni mgonjwa tayari kunakua na shida, tumeliona hilo na kwa mwaka huu kwa bahati mbaya TAMISEMI haikutupatia mwalimu hata mmoja, lakini tunafanya juhudi ifikapo likizo ya mwezi Desemba tuweze kufanya uhamisho..” alisema.
Alisema, walishindwa kufanya uhamisho kipindi hiki kutokana na kukumbwa na madeni ya fedha za uhamisho ambazo zilifikia zaidi ya milioni 70, lakini kwasasa madeni hayo yamelipwa na serikali na uwezekano wa kufanya uhamisho upo.
Kuhusu suala la zahanati, aliwataka wananchi kuwa na subira kwani zamu yao itafika kwasababu sera ya taifa ni kuhakikisha kila kijiji kinakuwa na Zahanati, kwahiyo kwasasa kuna vijiji ambavyo vinatekelezewa huduma hizo na baada ya hapo yatafuata maeneo mengine ikiwa ni pamoja na Nanyati.





No comments: