Friday, November 6, 2015

KUELEKEA MECHI YA PILI YA FAINALI YA CAF CHAMPIOS LEAGUE-TP MAZEMBE VS USM ALGERS




Na Juma Mohamed

IKIWA imebaki siku moja kabla ya watanzania wapenda soka na Afrika kwa ujumla kuelekeza macho na masikio nchini Kongo DRC, huko Lubumbashi ambako watanzania wawili, Mbwana Ally Samatta na Thomas Ulimwengu wataiwakilisha Tanzania katika mchezo wa fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika (CAF Champions League), kati ya wenyeji TP-Mazembe ambao watawakaribisha waarabu wa Algeria, USM Alger, haya ni mambo muhimu kuyatambua kabla hujatazama mchezo huo.
-Baada ya kupatikana bingwa mpya wa michuano hiyo ambaye atampokonya taji Al-Ahli ya Misri, atakwenda kuliwakilisha bara la Afrika katika fainali za klabu bingwa ya dunia ambazo zitafanyika nchini Japani.

-Wakati USM wakiingia kwa mara ya kwanza katika fainali ya Champions League toka kuanzishwa kwa klabu hiyo miaka 78 iliyopita, Mazembe wamechukua ubingwa wa Afrika mara 4 na sasa wanaufukuzia ubingwa wa 5.
-Tangu kuanza kwa michuano hiyo mwaka 1965, Mazembe ambayo ilianza kucheza michuano hiyo ikifahamika kama TP-Englebert, imecheza mechi 77 katika uwanja wa nyumbani na kufanikiwa kushinda mara 59, sare mara 15 na kupoteza mara 3.
-Mara ya mwisho kufungwa katika uwanja wa nyumbani, Mazembe ilikuwa ni mwaka 2009, ambapo ilifungwa na Al-Hilal Omduman, ya Sudan kwa magoli 2-0 katika mchezo wa marudiano. Katika mchezo wa kwanza ambao ulichezwa Omduman, Sudan, Mazembe walishindwa kwa mabao 5-2, na kuwafanya wafuzu kucheza fainali kwa kukutana na Heatland ya Nigeria ambapo baadaye walifanikiwa kutwaa ubingwa.
-Ushindi wa magoli 2-1 walioupata Mazembe nchini Algeria ni wakwanza, katika mara sita walizokwenda kucheza nchini humo na timu tofauti.

-USM hawana matokeo mazuri ya kushinda ugenini/nje ya nchi yao, michezo mingi walioshinda ugenini wameshinda nchini mwao katika hatua ya makundi.
-Ushindi pekee walioupata nje ya Algeria ni pale walipowafunga Al-Hilal magoli 2-1.
-Ili USM waweze kutwaa ubingwa wao wa kwanza, wanatakiwa wapate angalau ushindi sio chini ya magoli 2-0, lakini matokeo chini ya hapo yatawapa Mazembe ubingwa.
-Wachezaji wawili wa USM ambao ni Youcef Belaili na Hocine El Orfi, watakosekana katika mchezo wa Jumapili. Belaili, ana adhabu ya muda mrefu kutokana na kesi ya matumizi ya dawa za kulevya, huku El Orfi akiwa anatumikia adhabu ya kadi nyekundu ambayo aliipata katika mchezo uliopita.
Ptrice Carteron
Kocha wa Mazembe, mfaransa, Patrice Carteron, alikiri kuwa mchezo huo utakuwa mgumu na lolote linaweza kutokea hapo Jumapili, licha ya kucheza nyumbani.
“Tunaujua ubora wa USM. Ni timu nzuri katika michuano hii, na walifanya vizuri katika baadhi ya michezo yao ya ugenini na wanaweza kutushangaza.”
“Algeria wanafahamika kwa ubora wao ambao unawafanya waweze kuamua mchezo katika mazingira yoyote. Lazima tuupe uzito wa kipekee mchezo huu.” Alisema.
Aidha, aliwaahidi mashabiki kuwa timu yao itacheza kwa kushambulia kama kawaida yao.
Patrice Carteron
 “Tumeshinda ugenini, tuna namna nyingi za kufanya. Lakini bado tutacheza kwa tahadhari kubwa na kwa kujilinda..mashabiki wetu wanapenda soka safi na tutawaridhisha. Hatuna namna, timu yetu lazima icheze kwa kushambulia.” Aliongeza.
Mazembe, watawakosa nyota wao wawili ambao ni mfungaji mahiri wa Zambia, Rainford Kalaba, ambaye alipata kadi nyekundu katika mchezo wa kwanza, na Jean Kasusula, ambaye anasumbuliwa na mkono alioumia baada ya kupata ajali ya pikipiki Jumapili iliyopita aliporejea Lubumbashi wakitokea Algeria. Mlinzi huyo atakuwa nje ya uwanja kwa majuma kadhaa.
Mchezaji ambaye anategemewa kurejea uwnjani hapo Jumapili, ni Nahodha, Joel Kimwaga, ambaye alikuwa anatumikia adhabu ya kadi za njano alizopata katika hatua ya makundi.
Naye, kiungo wa timu hiyo raia wa Ghana, Daniel Nii Adjei, amewaonya wenzake kuelekea katika mchezo huo.
“Bado kazi haijaisha, tumeshinda mara moja lakini chochote kinaweza kutokea katika mchezo wa pili..wanweza kuja Lubumbashi na wakatuduwaza. Tunatakiwa kujiandaa vizuri ili tuwafunge na tuchukuwe ubingwa.” Alisema.

No comments: