Monday, June 29, 2015

Hawa Ghasia azionya mamlaka za serikali za mitaa.

Waziri wa TAMISEMI, Mhe. Hawa Ghasia, akihutubia katika sherehe za ufunguzi wa wiki ya serikali za mitaa, katika viwanja vya Mashujaa mjini Mtwara.

 
Na Juma Mohamed, Mtwara.

WAZIRI wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Hawa Ghasia, amezitaka mamlaka za serikali hizo kuanza mapema maandalizi ya mchakato wa kura ya maoni ya katiba pendekezwa na uchaguzi mkuu, ili kuepukana na changamoto zilizojitokeza katika uchaguzi uliopita.
Akizungumza wiki iliyopita mjini Mtwara katika uzinduzi wa maadhimisho ya wiki ya serikali za mitaa katika viwanja vya mashujaa, ambayo kitaifa yanafanyika mkoani humo, amesema mamlaka hizo zinatakiwa kudumisha hali ya ulinzi na usalama ili wananchi waweze kushiriki katika mazingira ya amani na utulivu.
Alisema maadhimisho hayo ya 11 yanafanyika ikiwa ni baada ya kukamilika kwa uchaguzi katika ngazi za mitaa, vijiji na vitongoji na kwamba kilichobaki sasa ni kujiandaa na uchaguzi mkuu wa madiwani, wabunge na Rais mwezi Oktoba mwaka huu, bila kusahau mchakato wa kura ya maoni ya katiba pendekezwa.
“Napenda nitumie fursa hii tena kuziagiza mamlaka zote za serikali za mitaa nchini kufanya yale yote yanayofanikisha mazoezi haya..nikisema hivyo nadhani wakurugenzi mnanielewa na mnafahamu waliofanya vibaya katika uchaguzi wa serikali za mitaa yaliyowakuta, japo siombei yatokee tena katika uchaguzi mkuu.” Alitahadharisha.
Aidha, alizitaka halmashauri zote ambazo bado hazijachangia maadhimisho hayo, kufanya hivyo kabla ya Julai 1 mwaka huu ambapo ndio itakuwa kilele chake huku yakitarajiwa kufungwa na waziri mkuu wa jamhuri ya muungano wa Tanzania, Mhe. Mizengo Pinda.
“Taarifa nilizonazo ni kwamba zipo baadhi ya halmashauri ambazo zinasuasua kuchangia maonyesho haya tangu miaka iliyopita na hata ya mwaka huu..napenda kutoa kauli kwamba halmashauri zote ambazo hazijachangia zihakikishe zinafanya hivyo kabla ya julai 1, na hata zile ambazo hazijashiriki, mpaka kufikia tarehe hiyo ziwe zimefika katika mji wa Mtwara.” Aliongeza.
Kwa upande wake, mkuu wa wilaya ya Mtwara, Fatma Ally, akizungumza kwa niaba ya mkuu wa mkoa, Halima Dendego, alitaja miradi ya maendeleo inayotekelezwa ndani ya mkoa ambapo ni pamoja na hospitali ya rufaa ya kanda ambayo ujenzi wake umeshaanza na tayari serikali imeshatenga bajeti yake kwa mwaka 2015/2016 ambayo ni sh. Bilioni 3 ili kuhakikisha ujenzi huo unaendelea.
“Pia tuna mradi wa ujenzi wa reli ya mchuchuma Luganga, Mbamba bay..yapo makampuni matano ambayo yanashirikiana na kwa sasa bado wanaendelea na zoezi la upembuzi yakinifu.” Alieleza.
Naye, katibu mkuu wa TAMISEMI, Juma A. Sagini, alisema madhumuni ya maadhimisho hayo yenye kaulimbiu inayosema “Mwananchi pigia kura katiba pendekezwa na chagua kiongozi bora kwa maendeleo endelevu baada ya 2015” pamoja na mambo mengine, ni kutoa fursa kwa wadau wa serikali za mitaa kutafakari shughuli mbalimbali wanazozifanya kwa lengo la kuharakisha maendeleo ya mamlaka zao na taifa kwa ujumla.

……………………mwisho………………………………………..

No comments: