Wednesday, August 24, 2016

Wakulima wa korosho Mtwara wahofia kuibiwa kwa kutojua kusoma Mizani.




Meneja wa Wakala wa Vipimo mkoa wa Mtwara, Augustine Maziku, akitoa elimu ya Mizani kwa wakulima wa korosho katika kijiji cha Kitama ya Kwanza wilayani Tandahimba, mkoani Mtwara.



Juma Mohamed, Mtwara.

Mkoa wa Mtwara ni miongoni mwa mikoa inayoongoza kwa kufanya vizuri katika kuzalisha zao la korosho ambalo ndio zao kuu la biashara mkoani humo, huku matarajio ni kuvuna tani laki nne ndani ya kipindi cha miaka Mitatu ijayo kutoka tani laki moja na nusu za sasa.
Licha ya kufanya vizuri zao hili, wakulima wanakabiliwa na changamoto kadhaa ambazo zinahitaji kupatiwa utatuzi wa haraka, ikiwa ni pamoja na kukosa elimu ya kuweza kusoma mizani zinazotumika kupima korosho zao.
Changamoto hii kwa kiasi kikubwa inalalamikiwa na wakulima wa kijiji cha Kitama ya Kwanza, ambao wanadai kuwa hali hiyo inawafanya wakose kuwa na uhakika na kudhani kama wanaibiwa korosho zao baada ya kupimwa na makarani.
“Kwanza mimi kama mimi yani sijui Mzani yani sijui kilo ngapi na hapa kilo ngapi hata sijui..na hapa sasa hivi nilipo wala nilikua sijui kama kuna mkutano humu ndani nimekurupushwa tu, kwahiyo sisi akina mama tumewekwa nyuma sana..” alisema Jazila Machenje, ambaye ni mkulima katika kijiji cha Kitama.

Mmoja wa wakulima wa zao la korosho katika kijij cha Kitama ya Kwanza wilayani Tandahimba, mkoani Mtwara akitoa maoni yake juu ya changamoto za Mizani.



“Mali ile ninapoipeleka ghalani kama Mzani siujui basi naona kama nadhurumiwa kwasababu ninaweza nikazikadiria nyumbani kwamba hizi zinaweza zikafika kilo hamsini nikija huku nikiambiwa kilo arobaini na tano kwakweli nakubali kwasababu kwasababu si nimeshazipeleka sokoni lakini kwa moyo wangu siamini kama kweli hizi hapa ni kilo hamsini..” aliongeza Said Samli.
Kwa kuona umuhimu wa utatuzi wa changamoto hiyo, serikali kupitia kwa Wakala wa Vipimo Nchini (WMA) iliamua kuendesha zoezi la kutoa elimu kwa wakulima hao kabla ya kuanza kwa msimu mpya wa mauzo, pamoja na kuhakiki ubora wa Mizani.
Akiwa katika zoezi la kutoa elimu hiyo, afisa vipimo mkuu wa WMA, Moses Ezekiel, alisema wamebaini idadi kubwa ya wakulima ambao hawawezi kusoma Mizani pale walipowaambia wasome Mizani ambapo walionekana kushindwa kutoa majibu sahihi.
“Tumejitahidi kutoa elimu wapo wanaodai kwamba wanafahamu lakini unapomwambia kwamba pima utaje kilo zako sahihi hawawezi..hilo tumeliona lipo na tunaendelea kutoa elimu kwa Oparesheni maalumu ya wakala wa vipimo lakini pia kuhakiki Mizani hizi kwa mtindo wa tofauti na pale nyuma..” alisema Moses.

Augustine Maziku akitoa elimu ya Mizani



Kwa upande wake, meneja wa WMA mkoa wa Mtwara, Augustine Maziku, alibainisha baadhi ya vifungu vya sharia vinavyotafsiri adhabu wanazopaswa kuchukuliwa watu wanaokiuka sheria ya vipimo.
“Sheria ya vipimo sura namba 340 inabainisha vizuri adhabu ambazo mkosaji wa biashara ya mizani anapaswa kuadhibiwa..kwa kosa la kwanza anapigwa faini ya sh. 10,000 kwa kila kosa linalohusiana na kosa alilofanya au kifungo kisichozidi miaka mitatu..” alisema.
Wadau wa zao hilo wanatarajiwa kukutana Agosti 26 na 27 mwaka huu mjini Bagamoyo kujadili masuala mbalimbali pamoja na kuzindua msimu mpya wa korosho.

No comments: