Thursday, August 16, 2012

BIN KLEB AMTUNUKIA TUZO YA UONGO 'ALHAJ' RAGE

 

Bin Kleb

 
MJUMBE wa Kamati ya Utendaji ya klabu ya Yanga, Abdallah Ahmad Bin Kleb, amerejea Dar es Salaam na kusema kwamba Mwenyekiti wa Simba SC, Alhaj Ismail Aden Rage anastahili tuzo ya kutunga uongo kwa kitendo chake cha kuwadanganya wanachama wa Simba eti kuna mtoto wa kigogo aliingilia usajili wa Mbuyu Twite.
“Rage anastahili tuzo ya muongo, ile vita ilikuwa kati yangu mimi na yeye, nadhani yeye alikuja Kigali kupiga picha na yule mchezaji, baada ya kushindwa kufanya hivyo alipokuwa Dar es Salaam, maana yake alikuja haraka haraka akazungumza na kiongozi mmoja wa FERWAFA (Shirikisho la Soka Rwanda), akapiga picha na Twite akaondoka.
Karudi Dar es Salaam kwenye Mkutano Mkuu anasema amemsajili Twite, baada ya mimi kuonyesha vielelezo vya kumsajili huyo mchezaji kama mikataba na picha akiwa anasaini na kukabidhiwa jezi, akaanza kusema kuna mtoto wa kigogo, huyo mzee vipi? Mbona anakuwa muongo namna hii.
Yeye aseme kweli tu, hana uzoefu na mambo haya, yeye ni mtu wa kuropoka tu, hawezi kazi,”alisema Bin Kleb.
Rage, alilalamika hadi kutoa machozi mjini Dodoma, wakati akizungumzia sakata la Mbuyu Twite akidai kuna mtoto wa kigogo aliingilia kati na ndio maana mchezaji huyo akabadilisha uamuzi wake na kwenda Yanga.
Rage alidai kumsaini kwanza Twite, huku akinywa kahawa mjini Kigali na akadai wakati anamsaini na kumpa dola za Kimarekani 30,000 Yanga wakapiga simu na mchezaji huyo akawajibu amekwishamalizana na watu wa Simba.
Lakini baadaye Twite akaibuka akisaini Yanga na kurudisha fedha za Wekundu hao wa Msimbazi.

MTAKATIFU TOM AELEZA MIKAKATI YAKE KABLA YA LIGI KUU

Mtakatifu Tom kazini Yanga

 
KOCHA wa klabu ya Yanga ya Dar es Salaam, Mbelgiji Tom Saintfiet amesema kwamba anataka mechi mbili kabla ya kutoka nje ya nchi kwenda kuweka kambi fupi ya kujiandaa na msimu mpya wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
Akizungumza na BIN ZUBEIRY jana, Mtakatifu alisema kwamba mechi ni dhidi ya timu hapa ya nyumbani na nyingine dhidi ya timu ya nje na baada ya hapo atakuwa tayari kwa safari ya nje nchi.
Kuhusu hilo, Katibu Mkuu wa Yanga, Celestine Mwesigwa alisema jana kwamba maandalizi ya mechi hizo yanaendelea vizuri na wanaweza kucheza na African Lyon ya Dar es Salaam na AFC Leopard ya Kenya.
Habari za ndani zinasema kwamba Yanga itakwenda Rwanda kuweka kambi fupi ya kujiandaa na msimu na huko itacheza na mechi za kirafiki na vigogo wa huko kama APR, Rayon, Rayon na Polisi.
Akiwa anaingia mwezi wa pili tangu aanze kazi Yanga, tayari Tom amekwishaweka Kombe moja kwenye kabati la mataji la Yanga, ambalo ni la Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame.
Yanga ilitwaa Kombe la Kagame kwa mara ya pili mfululizo wiki mbili zilizopita, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kwa kuifunga Azam FC mabao 2-0, ambayo yalitiwa kimiani na Hamisi Kiiza ‘Diego Milito’ na Said Bahanuzi ‘Spider Man’.
Hiyo kwa ujumla ilikuwa mara ya tano mfululizo, Yanga inatwaa Kombe hilo, baada ya awali kuchukua mwaka jana, wakiifunga Simba katika fainali bao 1-0, Uwanja wa Taifa mfungaji Kenneth Asamoah ambaye ametemwa, ingawa siku hiyo Kiiza pia alifunga bao safi, ambalo refa alilikataa.
Yanga ilichukua kwa mara ya kwanza Kombe hilo, mwaka 1975 ikiifunga tena Simba katika fainali, mabao 2-0 wafungaji Sunday Manara ‘Computer’ na Gibson Sembuli (sasa marehemu) Uwanja wa Amaan, Zanzibar.
Ikachukua tena mwaka 1993, Uwanja wa Nakivubo, Kampala, Uganda kwa kuifunga SC Villa mabao 2-1, yaliyotiwa kimiani na Said Nassor Mwamba ‘Kizota’ (sasa marehemu) na Edibily Jonas Lunyamila.
Ilichukua tena mwaka 1999, ikiifunga tena SC Villa, Uwanja wa Nakivubo, kwa penalti 5-3, kufuatia sare ya 1-1 ndani ya dakika 120, Yanga ikisawazisha bao kupitia kwa Lunyamila, baada ya Hassan Mubiru kutangulia kuifungia Villa, siku hiyo Manyika Peter akicheza penalti mbili za Waganda.
Aidha, kwa kutwaa Kombe hilo chini ya Mbelgiji huyo, Yanga imeendeleza rekodi yake ya kutwaa mataji ya michuano hiyo, chini ya makocha wa kigeni baada ya mwaka 1975 kuchukua chini ya Tambwe Leya aliyekuwa raia wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) kabla ya kuchukua uraia wa Tanzania, (sasa marehemu), 1993 chini ya Nzoyisaba Tauzany aliyekuwa raia wa Burundi kabla ya kuchukua uraia wa Tanzania, mwaka 1999 chini ya Raoul Shungu wa DRC na mwaka jana chini ya Mganda, Sam Timbe.

MATOLA ASEMA MTIBWA SUGAR WATAANGUKIA PUA KAMA AZAM

Suleiman Matola

 
KOCHA wa timu ya vijana ya Simba SC, Suleiman Abdallah Matola amesema kwamba hawahofii kabisa Mtibwa Sugar kuelekea fainali ya michuano ya Bank ABC Sup8R na anaamini atabeba Kombe mbele yao keshokutwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Akizungumza na BIN ZUBEIRY jana baada ya mechi Uwanja wa Taifa, Matola ambaye ni Nahodha wa zamani wa Simba SC, alisema kwamba Mtibwa ni timu nzuri aliiona vizuri wakati ikiifunga 5-1 Jamhuri ya Pemba, lakini bado kwa Simba B wataangukia pua.
“Itakuwa mechi ngumu hilo naamini kabisa, lakini nataka nikuambie, kama nilivyosema kabla ya kucheza na Azam, nasema tena kabla ya kucheza na Mtibwa Sugar, tutawafunga bila kuongezewa nguvu ya wachezaji wa timu A,”alisema Matola.
Simba jana ilitinga Fainali ya michuano ya BankABC Sup8R baada ya kuifunga Azam FC, mabao 2-1 kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na Jumamosi itamenyana na Mtibwa Sugar, ambayo katika mechi ya kwanza imeifunga Jamhuri ya Pemba mabao 5-1, uwanja huo huo.
Katika mchezo huo, hadi mapumziko, Simba B walikuwa mbele kwa bao 1-0, lililotiwa kimiani na Rashid Ismail aliyeunganisha krosi ya Edward Christopher dakika ya pili tu ya mchezo huo.
Kipindi cha pili ‘Watoto wa Matola’ walirudi na moto na kulisakama kama nyuki lango la Azam, wakigongeana pasi za uhakika ndefu na fupi na kuwafunika kabisa mabingwa wa Kombe la Mapinduzi.
Christopher Edward aliifungia Simba bao la pili kwa penalti dakika ya 56, baada ya yeye mwenyewe kuangushwa ndani ya eneo la hatari na Luckson Kakolaki.
Azam walipata bao la kufutia machozi dakika ya 71, mfungaji Zahor Pazi aliyeingia kipindi cha pili kuchukua nafasi ya Gaudence Mwaikimba, baada ya kutokea purukushani kwenye lango la Simba B.
Christopher Edward amezidi kujiimarisha katika mbio za kusaka kiatu cha dhahabu kwa kutimiza mabao matano, akifuatiwa na Shaaban Kisiga ‘Malone’ mwenye mabao manne.
Simba iliingia Nusu Fainali, baada ya kuongoza Kundi A, kwa pointi zake saba, baada ya kutoa sare moja na kushinda mechi mbili, wakati Mtibwa inayofundishwa na Nahodha pia na Nahodha wake wa zamani, Mecky Mexime, iliongoza Kundi B kwa pointi zake tisa baada ya kushinda mechi zote tatu.
Kanuni za mashindano haya ni kushirikisha timu zilizoshika nafasi tatu za juu katika Ligi Kuu za Bara na visiwani na mbili zilioongoza katika kupanda Ligi Kuu zote mbili, lakini kwa Bara, Yanga waliokuwa washindi wa tatu msimu uliopita, walijitokea na nafasi yao ikachukuliwa na Mtibwa Sugar ambayo ilishika nafasi ya nne kwenye Ligi Kuu.
Bingwa wa michuano hiyo mipya itakayokuwa ikifanyika kila mwaka, ataondoka na Sh. Milioni 40, mshindi wa pili Sh. Milioni 20, wa tatu Sh. Milioni 15 sawa na wa nne, wakati washiriki wengine wataondoka na Sh. Milioni 5 kila moja.

AZAM WAKUBALI MATOKEO, WAIPA GWALA SIMBA B YA MATOLA

Kipre Tchetche wa Azam kulia

 
AZAM FC imekubali matokeo ya kutolewa katika Kombe la BankABC Sup8R na imewapongeza Simba SC sababu timu yao ya vijana ni nzuri.
Msemaji wa Azam FC, Jaffar Iddi Maganga alisema jana kwamba, bahati ilikuwa yao Simba SC, kwani nafasi mbili walizopata walizitumia vizuri kwa kufunga mabao yao yaliyowapeleka fainali.
Jaffar alisema kwamba jana bahati haikuwa upande wa Azam, kwani walipoteza nafasi za wazik za kufunga mabao zaidi ya tano.
“Mtu kama Kipre Tcheche peke yake, alipoteza nafasi nne za wazi kabisa za kufunga akiwa amebaki yeye na kipa, lakini hiyo ndiyo soka na sisi tumekubali matokeo.
Tunawapongeza Simba SC, tunarudi kambini kuanza kujiandaa na mechi ya Ngao ya Jamii, ambayo tutacheza tena na Simba,”alisema.
Wakati jana Simba ilicheza timu ya vijana na Azam ilitumia wachezaji wengi wa akina, Mechi ya Ngao timu zote zinatarajiwa kushusha vikosi vyake kamili vya Ligi Kuu.
Mara ya mwisho, vikosi kamili vya timu hizo vilikutana kwenye mechi ya Robo Fainali ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame mwezi uliopita na Simba ilichapwa mabao 3-0, yote yakitiwa kimiani na John Raphael Bocco ‘Adebayor’, ambaye kwa sasa yupo Afrika Kusini akifanya majaribio ya kucheza soka ya kulipwa katika klabu ya Super Sport United.
 

MECKY MEXIME ASEMA WATOTO WA SIMBA HAWAMNYIMI USINGIZI

Mecky Mexime

 
KOCHA wa Mtibwa Sugar ya Morogoro, Mecky Mexime amesema kwamba ana matumaini ya kuwafunga Simba B na kubeba na Kombe la Bank ABC katika fainali itayapopigwa keshokutwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Akizungumza na BIN ZUBEIRY jana, Mecky alisema kwamba amewaona Simba wakati wanaitoa Azam kwa kuichapa 2-1 ni wazuri na wanacheza kwa uelewano sana, lakini Jumamosi anaamini atawafunga tu.
“Kabla sijawa kocha wa Mtibwa ya wakubwa, nilikuwa kocha wa vijana, na nilikuwa pia kocha wa vijana wa Morogoro katika Copa Coca Cola, ambayo ilikchukuja ubingwa. Kwa hiyo nawajua vijana, hivyo vijana wa Simba hawanipi hofu,”alisema Mecky.
Mexime alisema anajua namna ya kuwapoteza vijana uwanjani na kuvuna ushindi, tena wa mabao ya kutosha kabisa,
Mtibwa Sugar ilitinga Fainali kwa kishindo, kwa kuinyuka Jamhuri ya Pemba, mabao 5-1, ambayo yalitiwa kimiani na Babu Ally Seif dakika ya 15, Salvartoy Ntebe dakika ya 17, Mfaume Shaaban aliyejifunga dakika ya 38, Vincent Barnabas dakika ya 43 na Awadh Juma dakika ya 85 wakati la kufutia machozi la Jamhuri lilifungwa na Mbarouk Chande dakika ya 62.
Hadi sasa, Mtibwa ndio timu pekee ambayo haijapoteza pointi hata moja kwenye mashindano hayo baada ya kushinda mechi zake zote tatu za Kundi B, 2-1 dhidi ya Polisi Moro, 2-0 dhidi ya Azam na 5-0 dhidi ya Super Falcon na jana 5-1 dhidi ya Jamhuri katika Nusu Fainali.
Simba B yenyewe ilitoa sare moja tu ya kufungana 1-1 na Jamhuri katika mchezo wa kwanza, lakini mechi zake nyingine ilizifunga 2-0 kila timu, Mtende na Zimamoto ya Zanzibar.
 

HUYU NDIYE PASCHAL OCHIENG, KISIKI KIPYA SIMBA SC KILICHOWAHI KUKIPIGA YANGA

Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba SC, Zacharia Hans Poppe (kushoto) akimkabidhi jezi beki mpya wa klabu hiyo, Paschal Ochieng katika ukumbi wa mikutano wa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Tazama wasifu wake hapo chini.

JINA Pascal Ochieng
KUZALIWA Mei 15, 1986 (Miaka 26)
ALIPOZALIWA Kenya
NAFASI Beki
KLABU ALIZOCHEZEA
KLABU YAKE Simba SC
TIMU ZA WAKUBWA
MWAKA TIMU

2000-2001 Mathare United
2001-2002 Mazarea Dina
2003-2004 World Hope FC
2004-2005 Re-Union Nairobi
2005 Young Africans S.C.
2005-2006 Brabrand IF
2006-2008 Young Africans S.C.
2008-2009 Kenya Commercial Bank FC
2010 Posta Rangers F.C.
2012 Johor FC
National team
Tangu 2001- Kenya anachezea timu ya taifa Kenya Mechi 23 (Bao 1)

No comments: