Tuesday, June 21, 2016

Kuchelewa pembejeo za ruzuku kero kwa wakulima wa korosho Lindi na Mtwara.




Baadhi ya wakulima wa korosho na viongozi wa vyama vya msingi kutoka mikoa ya Lindi na Mtwara wakiwasilisha kero zao kwa mkuu wa mkoa wa Mtwara, Halima Dendego, baada ya kutembelea ghala la chama kikuu cha ushirika la Tandahimba, Newala Cooperative Union (TANECU).



Mkuu wa mkoa wa Mtwara, Halima Dendego, akielekea ndani ya ghala la TANECU kwa ajili ya kukagua pembejeo za ruzuku za zao la korosho. Kulia ni mkuu wa wilaya ya Tandahimba, Emmanuel Luhahula.



Na Juma Mohamed, Tandahimba.

Baadhi ya viongozi wa vyama vya msingi katika mikoa ya Lindi na Mtwara wamelalamikia uchelewaji wa pembejeo za ruzuku za zao la korosho, zinazosambazwa na Mfuko wa Kuendeleza Zao la Korosho (WAKFU), na kulazimika kutumia muda mwingi wakiwa maghalani kusubiri mzigo.
Wakizungumza mbele ya mkuu wa mkoa wa Mtwara, Halima Dendego, katika ghala kuu la Chama Kikuu cha Ushirika cha Tandahimba, Newala Cooperative Union (TANECU), walisema hali hiyo inapelekea kuwapo kwa mvutano kati ya wakulima na viongozi wa vyama.
“Pembejeo kutoka mwezi wa sita haziendani na kilimo cha korosho, kwasababu sasa hivi korosho zimeshachipuza na watu wanatarajia..kwahiyo tunakuwa tunasutana, mimi wananisuta wakulima na mimi nawasuta watu wa pembejeo..sasa mkuu wa mkoa tunakuomba hili ulizingatie na usome nyakati..” alisema Awadhi Mbeweka, mwenyekiti wa AMCOS ya Masasi.

Wakulima wa korosho na viongozi wa AMCOS



Naye, Abdallah Matandika ambaye ni kiongozi wa chama cha msingi cha Chibula wilayani Ruangwa mkoani Lindi, alisema katika wilaya hiyo ni vyama vinne pekee kati ya vyama 21 ambavyo vimepata pembejeo.
Mbunge wa jimbo la Tandahimba, Katan Ahmaed, alikiri kupokea malalamiko kutoka kwa baadhi ya wakulima wakilalamikia changamoto hiyo, ambapo amewashauri kuwasilisha malalamiko yao ofisi ya mkuu wa mkoa kabla ya kwenda ngazi za juu zaidi, kwani mkuu wa mkoa anauwezo wa kutatua kwa haraka changamoto zao.
“Miongoni mwa malalamiko makubwa ilikuwa ni watu wa Liwale pamoja na Nachingwea, lakini nilipata shida baada ya ku ‘crosscheck’ baina ya watu wale na watu wa mfuko maelezo kidogo yalikuwa tofauti..wapo watu walitoa taarifa za mbali sana, na hili lazima nitoe tahadhari kwa watu kwamba tuna mkuu wa mkoa kama mmeona mmempa taarifa leo na amekuja kwa haraka, lakini kuna watu wanakawaida ya kuruka hatua..” alisema Katan.

Mkuu wa mkoa wa Mtwara, Halima Dendego, akisikiliza maelezo kutoka kwa mwenyekiti wa bodi ya wadhamini wa Mfuko wa Kuendeleza Zao la Korosho Nchini (WAKFU), Athuman Nkinde, juu ya masuala ya pembejeo za ruzuku za korosho. Kushoto ni mkuu wa wilaya ya Tandahimba, Emmanuel Luhahula.



Kaimu katibu mtendaji wa WAKFU Ramadhan Mmari, alisema bado mfuko unafanya jitihada za dhati kuhakikisha pembejeo hizo zinafika kwa wakulima kwa wakati, ambapo jumla ya tani elfu 10 tayari zimegawanywa katika mkoa wa Mtwara ambazo ni sawa na asilimia 70 huku mkoa wa Lindi zimegawiwa kwa asilimia 56 na Ruvua asilimia 38.
Kwa upande wake, mkuu wa mkoa wa Mtwara Halima Dendego, amewataka watendaji wa ugawaji wa pembejeo hizo kufanya kazi usiku na mchana, ili kuondoa usumbufu wa kupanga foleni kwa viongozi hao wakati wa kusubiri kupatiwa pembejeo.
“Lakini kubwa mhe. Mwenyekiti mimi niwaombe watendaji, waache kufanya kazi kwa mazoea, wanapoona kuna tatizo wafanye kazi usiku na mchana saa 24 baadala ya kufanya kazi mpaka saa 10 baadae wanaenda kulala haya magari tusingeyakuta kama ingekuwa wanakesha hapa..” alisema.
Kwa mujibu wa WAKFU, ni kwamba mpaka kufikia June 26 mwaka huu mzigo wote uliobaki wa tani 65,000  wa pembejeo hizo utakuwa tayari umeshawasili kwa ajili ya kuugawa kwa wakulima.

No comments: