Monday, May 2, 2016

RC Mtwara atumbua majipu manne Masasi na Nanyumbu.

Mkuu wa mkoa wa Mtwara, Halima Dendego, akihutubia katika maadhimisho ya siku ya wafanyakazi (Mei Mosi) yaliyofanyika katika halmashauri ya wilaya ya Nanyumbu.



Wafanyakazi wa Bodi ya Korosho Tanzania (CBT) mkoa wa Mtwara.




Na Juma Mohamed, Mtwara.
SHEREHE ya maadhimisho ya siku ya wafanyakazi (Mei Mosi), imekuwa chungu kwa maafisa utumishi watatu wa halmashauri ya mji wa Masasi na wilaya na mmoja wa halmashauri ya wilaya ya Nanyumbu, baada ya kusimamishwa kazi na mkuu wa mkoa wa Mtwara, Halima Dendego kwa tuhuma za ubadhirifu wa fedha.
Mkuu wa mkoa alifanya maamuzi hayo wakati akihutubia katika sherehe hizo zilizofanyika kimkoa katika halmashauri ya wilaya ya Nanyumbu ambapo aliwataja wanaotuhumiwa kuwa ni Shaibu Mwakakita, Haswege Kaminyonge na Kheri Kagogoro wa halmashauri ya mji wa Masasi pamoja na Suleiman Katete wa halmashauri ya wilaya ya Nanyumbu.
Alisema maafisa utumishi watatu wa halmashauri ya mji na wilaya ya Masasi wamejipatia fedha zaidi ya sh. Milioni 192 kwa njia ya udanganyifu jambo ambalo linapelekea kuziingizia hasara halmashauri hizo na kushindwa kulipa mafao ya wafanyakazi.

Gari la halmashauri ya wilaya ya Nanyumbu lenye uwezo wa kuchimba visima vya maji vya kina kirefu


“Mhe. Amesema tusaidiane kutumbua, kama tukisema tumuachie yeye kila siku atumbue pekeyake haitawezekana..kwahiyo nikasema leo ni siku ya furaha lakini ni lazima furaha hii iambatane na machungu kwa wale ambao hawataki kuienzi siku hii, kwahiyo naagiza tena kupitia hadhara ya leo hasa kikao hiki cha Mei Mosi na mkutano huu wale maafisa utumishi wote watatu waliohusika na mambo hayo wanasimama kazi kwanzia leo na taratibu nyingine zianze kuchukuliwa..” alisema.
Alilitaka jeshi la polisi kuwakamata haraka na kuwafikisha mahakamani huku hatua nyingine za kisheria zitafuata, huku akimsimamisha kazi afisa utumishi wa halmashauri ya wilaya ya Nanyumbu, Suleiman Katete.
Kuhusu wafanyakazi hewa, alisema mpaka siku moja kabla ya maadhimisho hayo mkoa wa Mtwara ulikuwa na wafanyakazi hewa 107 huku zaidi ya sh. Milioni 300.9 ambazo zingesaidia kulipa madeni ya uhamisho na masaa ya ziada kwa wafanyakazi.
 Akizungumza kwa niaba ya katibu wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA) mkoa wa Mtwara, Ado Chiwangu, katibu wa Chama cha Walimu Mkoa wa Mtwara (CWT), Fratern Kwahisson, alisema kaulimbiu ya mwaka huu inayosema  “Nidhamu ya mabadiliko iinue hali ya wafanyakazi”, inalenga kuitaka serikali, waajiri na wadau wengine wa ajira kuboresha ustawi wa wafanyakazi ili kuleta tija.

Wafanyakazi wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO)


Alisema, kaulimbiu hiyo imelenga kuitaka serikali ya awamu ya tano kupitia upya mapendekezo yote yaliyowahi kupendekezwa na vyama vya wafanyakazi na wasomi mbalimbali zikiwemo tume zilizoundwa na kubuni namna ya kufanyia kazi.



No comments: