Tuesday, April 19, 2016

Wananchi Mtwara wahamasika kuchangia Madawati.

Viongozi wa vijiji na wawakilishi wa makundi mbalimbali wa Tarafa ya Mpapura, halmashauri ya wilaya ya Mtwara, waliohudhuria kikao cha mkuu wa wilaya ya Mtwara, Fatma Ally kwa ajili ya kujadili masuala ya kimaendeleo katika ngazi za vijiji, kata na tarafa.




Fatma Ally, akiongea na wananchi



Na Juma Mohamed, Mtwara.

WANANCHI wa vijiji mbalimbali halmashauri ya wilaya ya Mtwara wamehamasika na kuunga mkono jitihada zinazofanywa na mkuu wa wilaya ya Mtwara Fatma Ally, za kutatua changamoto ya ukosefu wa madawati katika shule za msingi na sekondari.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti katika ziara iliyofanywa na mkuu wa wilaya huyo kwa ajili ya kuhamasisha wananchi kushiriki kikamilifu katika shughuli na mipango mbalimbali ya kimaendeleo, walisema awali suala hilo lilipokelewa tofauti kwa kujua ni jukumu la viongozi wa ngazi za juu pekee.

Mkazi wa kata ya Mpapura, Saidi Saidi, akiwasilisha mchango wake katika kikao cha pamoja kati ya viongozi na wawakilishi wa makundi mbalimbali katika tarafa ya Mpapura, kilichoitishwa na mkuu wa wilaya ya Mtwara, Fatma Ally.


“Agizo baada ya kupokelewa, tulisema ameagizwa mkuu wa wilaya, ameagizwa mkuu wa mkoa hatukujua kwamba tumeagizwa mpaka sisi sasa leo umetuzindua tuko macho, nasema kwamba miti ipo na watu wakufanya kazi wapo mimi mwenyewe ninao mti mmoja na ninautoa sasa hivi..taratibu sasa ya jinsi gani tunafanya ndio tulikuwa hatujajua..” alisema Sadiki Sadiki, mkazi wa kata ya Mpapura.
Alitoa wito kwa viongozi wa vijiji kuwafikishia kwa wakati wananchi wao taarifa za kimaendeleo zinapowafikia sambamba na kuwapatia elimu pale inapobidi kufanya hivyo ili wapate fursa ya kushiriki katika mambo muhimu yanayohitaji nguvu ya pamoja.

Mkazi wa kata ya Mayanga, akiwasilisha ya moyoni kwa mkuu wa wilaya ya Mtwara, Fatma Ally, baada ya kufanya kikao cha kazi na viongozi na wawakilishi wa makundi mbalimbali katika kata hiyo kujadili masuala ya kimaendeleo.


Naye, Yusufu Chikunyembe, mkazi wa kijiji cha Mpapura ambaye alikuwa anawakilisha vijana, alisema ataitumia elimu aliyoipata kupitia kikao hicho cha mkuu wa wilaya kwa ajili ya kwenda kuwahamasisha vijana wenzake katika kuunga mkono na kushiriki katika utatuzi wa mahitaji hayo.
Alitoa mti mmoja ambao upo katika shamba lake kwa ajili ya kupasuliwa mbao zitakazotumika kutengenezea madawati huku akiiomba serikali ya kijiji kuwaandaa watu kwa ajili ya kwenda kufanya kazi hiyo.
Moses Mnunduma, ambaye ni mwenyekiti wa kijiji cha Mayanga, aliahidi kwenda kuwahamasisha wanakijiji wake kuanza harakati za kuchangia madawati huku akilalamikia vitendo vya viongozi wa kata kuchelewa kuwasilisha taarifa kwa wananchi wao.
Aidha, mkuu wa wilaya ambaye kupitia mfuko wake wa kuhamasisha wananchi kuchangia madawati kwa hiyari aliyouita ‘Haba na haba hujaza kibaba’ ambao mpaka sasa amekusanya sh. Milioni 14, aliagiza ziundwe kamati za watu 10 katika kata Tatu ambazo alizitembelea juzi na kuzipa jukumu la uhamasishaji wa suala hilo.
Alisema, kamati hizo zitakuwa na wajumbe watakaowakilisha makundi mbalimbali ikiwa ni pamoja na wazee maarufu wa kijiji, vijana maarufu pamoja na viongozi wao wa vijiji ambapo aliahidi kurudi tena baada ya siku 10 kwa ajili ya kupata mrejesho wa utekelezaji wa maagizo yake.

Mkuu wa wilaya ya Mtwara, Fatma Ally, akiongea na wananchi wa tarafa ya Mpapura, halmashauri ya wilaya ya Mtwara, juu ya masuala mbalimbali ya kimaendeleo.


“Muhamasishe vijana wenzenu maarufu kwa ajili ya wale wazee wetu ambao wametupa heshima ya kutupa mbao mshirikiane nao mkacharange hiyo miti ili tupate hizo mbao zipelekwe kwenye eneo ambalo tumeliandaa..mgambo wa tarafa wapewe kazi ya kulinda zile mbao, mafundi waanze kazi baada ya siku 10 nitakuja na mkuu wa mkoa atakuja kuwakagua kazi inaendeleaje..” alisema mkuu wa wilaya.



No comments: