Kikosi cha Ndanda Fc kilichoanza katika mchezo dhidi ya Azam Fc jana. |
Wachezaji wa Azam Fc wakiwasalimia mashabiki wao waliosafiri kutoka Dar es Salaam mpaka Mtwara kwa ajili kuishangilia timu yao, walipomenyana na Ndanda Fc ya Mtwara |
Nahodha wa Azam Fc, Himid Mao, akichuana na Nahodha mwenzie wa Ndanda Fc, Kiggi Makassy |
Na Juma
Mohamed.
LICHA ya
kupoteza mchezo wao dhidi ya Azam Fc ya jijini Dar es Salaa kwa goli 1-0,
mashabiki wa timu ya soka ya Ndanda Fc ya mkoani hapa wameonyesha kufurahishwa
na kiwango kilichoonyeshwa na wachezaji ambao walionekana kucheza kwa kujituma
zaidi.
Akizungumza
baada ya kumalizika mchezo wa ligi kuu ya Tanzania bara kati ya timu hizo
uliochezwa jana katika uwanja wa Nangwanda Sijaona mkoani hapa, shabiki
aliyejitambulisha kwa jina moja la Magita, alisema matokeo hayo sio mabaya kwa
mashabiki ukilinganisha na matokeo ya mchezo uliopita dhidi ya Toto Africans ya
mwanza.
Alisema,
Azam walistaili kupata matokeo ya ushindi kutokana na ubora wa timu yao na aina
ya wachezaji walionao, lakini Ndanda walipaswa kuwafunga Toto Africans kutokana
na kuwa ni timu ngeni katika ligi ambayo wachezaji walionao hawanatofauti na wa
timu ya Ndanda.
Heka heka katika lango la Ndanda. |
“Matokeo
siyo mabaya lakini tunaulaumu sana uongozi wetu kutokana na kuelekeza nguvu
nyingi kwenye timu kubwa lakini zinapokuja timu ndogo tunatoka nao droo (sare)
au wanakuja kutufunga hapa..yani mimi kama mdau, viongozi wa Ndanda
wanavyofanya sio vizuri..” alisema.
Alisema,
Ndanda wanapaswa kutumia vema michezo wanayocheza katika uwanja wa nyumbani kwa
kuhakikisha wanapata matokeo ya ushindi, kwasababu viwanja vya ugenini vigumu
kufanya hivyo.
Akizungumza
baada ya kumalizika mchezo huo, kocha wa Ndanda, Hamimu Mawazo, alisema
hakufurahishwa na matokeo waliyopata, lakini bado anaimani na kikosi chake na
kukiri licha ya mapungufu yaliyopo katika baadhi ya maeneo hasa katika
umaliziaji, walicheza vizuri na walionekana kutoa upinzani hasa katika sehemu
ya kiungo.
“Haya ni
moja ya matokeo ya mpira, lakini tuliweza ‘ku dominate’ kwenye uwanja kwa muda
mrefu na tulikuwa na mashambulizi ya kutosha katika goli lao, lakini hatukuweza
kuzitumia vizuri nafasi hizo huku wenzetu waliitumia nafasi moja basi ndio
mpira..sina kwa kulalamikia wala kusikitikia kwasababu ndio mchezo umekwisha na
tumepoteza..” alisema.
Mashabiki waliojitokeza kutazama mechi ya Ndanda na Azam, Nangwanda Sijaona, Mtwara |
Alisema,
kumekuwa na utofauti kati ya kiwango kilichoonyeshwa na wachezaji katika mchezo
uliopita na Toto Africans ambao walilazimishwa sare na mchezo dhidi ya Azam
huku akikiri kuwa na tatizo katika idara ya ushambuliaji ambayo inaongozwa na
Atupele Green.
Aliutaka
uongozi wa timu hiyo kujitahidi katika usajili ujao wa dirisha dogo ili
kuongeza nguvu katika idara hiyo ambayo inaifanya timu kuwa na ukame wa mabo.
Kwa upande
wake, kocha msaidizi wa kikosi cha Azam Fc ambaye aliwahi kukinoa kikosi cha
Ndanda msimu uliopita, Benis Kitambi, alikiri kuwa na changamoto ya ufungaji wa
magoli mengi katika timu yao kiasi cha kuwafanya vinara wa ligi hiyo Yanga Sc
kuwazidi kwa idadi ya magoli na wao kusalia katika nafasi ya pili.
Mshambuliaji wa Ndanda Fc, Atupele Green akikimbilia mpira. |
Alisema,
benchi la ufundi tayari wameshaliona hilo na sasa linafanyiwa kazi ili
kuhakikisha katika michezo inayofuata wanapata magoli mengi hasa wanapokutana
na timu dhaifu, kama ilivyo kwa Yanga ambao waliwafunga magoli 4 Toto Africans.
“Hilo
tumekiri kwamba inabidi tulifanyie kazi, utofauti uliyopo kati yetu na Yanga ni
kwamba wao wanapocheza na timu dhaifu niseme, wanapata magoli mengi kwahiyo na
sisi kama leo tumepata nafasi nyingi lakini hatukuweza kuzitumia..” alisema.
Kuhusu
ushindi wa kwanza katika uwanja wa Nangwanda, alisema ni jambo la kawaida
kwasababu Ndanda sio kwamba wameshinda michezo mingi dhidi yao katika uwanja
huo lakini ni mchezo mmoja pekee katika msimu uliopita ambapo hata na wao
walishinda waliporudiana katika uwanja wa Azam Complex, Chamanzi, Dar es Salaam.
Ndanda
watacheza na Stand United ya Shinyanga katika mchezo unaofuata na wataendelea
kusalia katika uwanja wa Nyumbani huku Azam wakitarajiwa kupambana na JKT Ruvu
huko Chamanzi.
No comments:
Post a Comment