Wednesday, January 20, 2016

TPA yatakiwa kukusanya Trilioni 1 kwa mwaka.


Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhe. Makame Mbarawa (wapili kushoto) akiongea na watendaji wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari tanzania (TPA) mkoa wa Mtwara, baada ya kufanya ziara ya kikazi Bandarini hapo


Na Juma Mohamed, Mtwara.

SERIKALI imeitaka Mamlaka ya Usimiamizi wa Bandari Tanzania (TPA) kuongeza makusanyo yake kwa mwaka kutoka sh. Bilioni 600 ambazo walijipangia mpaka kufikia Trilioni 1 ili fedha zisaidie kutatua matatizo ya wananchi, kuliko kuacha zikipotea kwa uzembe wa watendaji.
Akizungumza mkoani hapa baada ya kufanya ziara katika Bandari ya Mtwara, Waziri wa Uchukuzi, Ujenzi na Mawasiliano, Mhe. Makame Mbarawa, alisema serikali ya awamu ya Tano imejikita katika kuhimiza uwajibikaji kwa watendaji, na haitokuwa na huruma kwa mtu yeyote atakayefanya kinyume na hayo.
Alisema, serikali haitowaagiza wakusanye mapato ambayo hayapo isipokuwa ni yale yaliyopangwa kukusanywa kwa mujibu wa sheria na ambaye hakubaliani na maagizo hayo anapaswa kuondoka mwenyewe bila kungoja kufukuzwa.
“Sasa hivi sitokufukuza kama nakuhamisha, nakufukuza moja kwa moja..utakwenda huko kwenye chama cha wafanyakazi lakini naamini na chama hicho hakitomsaidia mtu ambaye hakusanyi kodi, kitakua ni chama cha ajabu kinampigania mtu ambaye hataki kufanya kazi yake ipasavyo, chama cha wafanyakazi najua kinatetea wananchi ambao wanastaili.” Alisema.

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhe. Makame Mbarawa, akiongea na wafanyakazi wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) mkoani Mtwara wakiongozwa na meneja wa Bandari hiyo Prosper Kimaro (hawapo pichani), baada ya kufanya ziara ya kikazi


Alisema, bandarini kuna udhaifu mkubwa sana ambao serikali haiwezi kuuvumilia na kwamba itaendelea kuchukua hatua mpaka pale itakapojiridhisha kuwa pamekaa vizuri hata ikibidi kubakiza wafanyakazi wachache kuliko kuwanao wengi ambao hawaleti tija inayohitajika.
Alisema, maamuzi hayo hayatofanywa kwa kumuonea mtu bali kwa wale ambao hataweza kutimiza wajibu wao kwani bandari inauwezo wa kukusanya mapato mengi zaidi na kuahidi kwa bandari ya Mtwara kuwapa malengo yao ya makusanyo kwa mwaka.
“Leo mnasema tunatumbua majipu, majipu hapa ni mapato tunataka..kama tukipata mapato yanayotokana na sheria sisi wala hatuna shida na bandari, lakini hivi inavyokwenda lazima tujipange, Bandari ya Mtwara nyie lazima tutawapa ‘Target’ mpya kwasababu tumemwambia mkurugenzi mkuu tunataka ‘Target’ ya Trillion 1 atutafutie ‘This yer’..” alisema Waziri na kuongeza:
“Sio yeye mwenyewe ajipangie Bilioni 600, kwanza haiwezekani mwenyewe unajipangia inatakiwa bosi wako ajue alafu akuambie  kwamba mimi nataka ukusanye hiki, wewe unahangaika na ile ‘Target’ lakini ilikuwa haifanyiki hivyo..serikali imeshamwambia, mwaka unaokuja wa fedha atupatie Trilioni 1 sasa kama hakupata atatueleza kwamba nimeshindwa kukusanya kwasababu hizi..” aliongeza.

Meneja wa Bandari ya Mtwara, Prosper Kimaro, akiwasilisha taarifa ya Bandari hiyo kwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhe. Makame Mbarawa (Hayupo pichani) ambaye alifanya ziara katika Bandari hiyo


Kwa upande wake, meneja wa Bandari ya Mtwara, Prosper Kimaro, alisema miongoni mwa mipango waliojiwekea ni kuongeza Gati 4 katika Bandari hiyo ambapo kwa kuanzia wataanza kwa ujenzi wa Gati moja ambayo tayari mamlaka imeshaamua na ujenzi wake utatumia fedha za ndani.
Alisema tayari tebda kwa ajili ya ujenzi wa Gati hilo ilishatangazwa na ilishafunguliwa ambapo baada ya kukamilika ujenzi huo ndipo mchakato kwa ajili ya Gati nyingine Tatu utaanza.





No comments: