Wednesday, January 20, 2016

Ndanda wawachezesha ‘Sindimba’ Mbeya City Nangwanda.



Wachezaji wa Ndanda Fc wakishangilia bao katika mchezo wa ligi kuu ya Vodacom Tanzania Bara dhidi ya Mbeya City jana katika uwanja wa Nangwanda Sijaona Mtwara. Ndanda walishinda kwa goli 4-1


Na Juma Mohamed, Mtwara.

BAADA ya kusota kwa muda mrefu bila kupata matokeo ya ushindi hatimae timu ya soka ya Ndanda Fc ya mkoani hapa hapo jana ilifanikiwa kuondoa ‘gundu’ baada ya kuisambaratisha Mbeya City ya jijini Mbeya kwa jumla ya magoli 4-1 katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara uliofanyika katika uwanja wa Nangwanda Sijaona mkoani hapa.
Katika mchezo huo wa kukamilisha mzunguko wa kwanza wa michuano hiyo wenye michezo 15 ambao ulichezeshwa na mwamuzi Endrew Shamba kutoka Pwani, iliwachukua Dakika 11 tu Ndanda kuweza kuandika bao la kwanza lililokwamishwa na mshambuliaji Atupele Green aliyeitendea haki pasi ya mlinzi wa kulia Hemed Khoja na kasha kuwatoka walinzi wa City na kumchambua mlinda lango Juma Kaseja.
Dakika saba badae, Mshambuliaji pacha wa Atupele, Omar Mponda alitumia vema makosa ya Juma Kaseja aliyeshindwa kuutuliza mpira aliyerudishiwa na mlinzi wa City ambapo Mponda aliyemzidi mbio Kaseja aliukwamisha wavuni na kuandika goli la pili kwa Ndanda dakika ya 18.

Wachezaji wa Ndanda wakipongezana baada ya kufunga goli


Hakika ilikuwa ni siku njema kwa Mponda ambaye alikuwa na ukame wa mabao baada ya kukaa muda mrefu bila kufunga, ambapo katika dakika ya 28 akicheza kwa ushirikiano mkubwa na Atupele, alikwamisha tena wavuni na kuandika bao la Tatu kwa Wanakuchele mara hii akipokea pasi kutoka kwa Atupele kutoka wing ya kulia.
Ndanda walienda mapumzikko huku tayari wana akiba ya magoli 3-0 katika mchezo huo ambao City walionekana kuuanza kwa kasi lakini walinzi na kipa Juma Kaseja wakionekana kufanya makosa binafsi mengi sana kiasi cha kuwarahisishia kazi washambuliaji wa Ndanda ambao leo walionekana kuwa moto wa kuotea mbali.
Kipindi cha pili kilipoanza City walionekana kuja juu kutafuta mabao ya kusawazisha huku Ndanda wakiilinda zaidi na kupanga mashambulizi ya kushtukiza langoni mwa City ambao walifanikiwa kupata kona nyingi katika mchezo huo ambazo hazikuweza kuzaa matunda.
City walifanikiwa kupata goli la kufutia machozi kunako dakika ya 63 kufuatia kazi nzuri iliyofanywa na mlinzi wa kulia John Jerome ambaye alimtengezea krosi nzuri winga Joseph Mahundi ambaye alituliza mpiara na kumuangalia mlinda lango wa Ndanda Jeremia Kisubi, na kasha kuukwamisha mpira wavuni na kuipatia City bao pekee katika mchezo huo.

Mlizi wa kushoto wa Mbeya City, Hassan Mwasapile akiondoa hatari upande wa lango lao.


Alikuwa ni Atupele tena aliyeiandikia bao la Nne Ndanda na kuhitimisha karamu ya mabao hapo jana, mara hii akiunganisha kwa shutu kali mpira uliochongwa kutokea upande wa kushoto na mshambuliaji aliyekuwa ameingia muda mfupi kabla ya kufungwa kwa bao hilo, Buruhani Halfan aliyechukua nafasi ya Omar Mponda.
Mchezo ulikuwa ni wa kuvutia kutokana na viwango vilivyoonyeshwa na timu zote mbili na ufundi kutoka kwa baadhi ya wachezaji, burudani zaidi ikiwa katikati ya uwanja lakini ubabe pia ulichukuwa nafasi na kushuhudiwa kadi kadhaa za njano zikitoka huku kadi nyekundu ikitolewa kwa Mlinzi Harouna Shamte baada ya kuonyeshwa kadi mbili za njano.
Makocha wote walizungumza baada ya mchezo huo ambapo kocha wa Mbeya City, Meja Mstaafu Abdul Mingange, alisema matokeo ameyapokea na Ndanda walistaili kwasababu walicheza vizuri zaidi yao.
“Mchezo ulikuwa nzuri Ndanda walicheza vizuri  nawapongeza wameshinda Ndanda..wachezaji hawakuzidiwa bali ni mchezo tu, huu ndio mpira, anafungwa Barcelona sasa unategemea Mbeya City wasifungwe!.. ‘This is Football’ tumefungwa tunajipanga upya, mimi nasema Ndanda wamecheza vizuri wameshinda, sisemi mabeki wamefanyaje, tuna points 14 sasa usilaumu mabeki ‘forward lines’ hapana huu ndio mpira.” Alisema.
Naye kocha wa Ndanda, Amimu Mawazo ambaye alionekana kuwa mwenye furaha hii leo kwa ushindi huo ambao ni wa pili msimu huu toka pale alipoilaza Coastal union ya Tanga katika mchezo wa pili wa ligi katika uwanja huo kwa goli 1-0, alisema mwanzoni kabla ya kuanza mchezo alikua na wasiwasi kufuatia kikosi chake kuwakosa wachezaji Watano wa kikosi cha kwanza ambao walianza katika mchezo uliopita dhidi ya Yanga ambao walipoteza kwa goli 1-0.
“Yani kwakweli tunajipongeza sana, tulikuwa na uwezo wa kufunga goli zaidi ya Nne, kwahiyo tunajipongeza na haya maeneo mengine ambayo yalikuwa na matatizo tutakwenda kuyafanyia kazi na ‘next time, tutafanya vizuri zaidi.” Alisema.
Kwa upande wa mashabiki wa Ndanda, walionekana kuwa na furaha hii leo huku wengine wakimshangilia na kumpongeza kocha wao Amimu Mawazo ikiwa ni mchezo wa tatu baada ya mashabiki hao kumshinikiza aliyekuwa kocha msaidizi wa timu hiyo Ngawina Ngawina kuweza kuachia ngazi ya kumsaidia Mawazo.
Mwenyekiti wa masahabiki hao, Mohamed Yusufu, aliwataka mashabiki wenzake waendelee kushikamana kwa kuipa hamasa timu ambapo baadhi yao walianza kujiondoa kutokana na mwenendo mbaya wa timu.
Naye, Shani Christopher, alisema katika mchezo huo waamuzi walijitahidi kuchezesha bila upendeleo na ndio sababu ya ushindi huo huku akidai kuwa katika mechi nyingine zinazowakutanisha Ndanda na timu “kubwa” waamuzi watendi haki kwani wanaonyesha upendeleo kwa timu hizo.



No comments: