Wednesday, November 11, 2015

Polisi Mtwara wakamata Milipuko ya Mabomu.


Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mtwara ACP-Henry Mwaibambe, akiongea na waandishi wa habari baada ya kukamatwa kwa Milipuko ya kutengeneza Mabomu pamoja na watu wanaotuhumiwa kuhusika uuzaji wa vifaa hivyo.

 Na Juma Mohamed

WATU watatu wanashikiliwa na jeshi la polisi mkoani hapa kutokana na kukutwa na vifaa mbalimbali vya milipuko vinavyotumika katika uvuvi haramu wa kutumia baruti katika bahari ya Hindi, katika oparesheni maalumu ya kuwakamata wanaojihusisha na mtandao huo.
Wanaoshikiliwa kutokana na oparesheni hiyo iliyofanywa na jeshi hilo kwa kushirikiana na Marine Park pamoja na kikosi maalum cha Taifa kinachoshughulikia uhifadhi wa mazingira pamoja na Bahari, ni Mussa Kais (30), Dadi Selemani (31) na Hose Chikota (24) ambao ni wakazi wa Mtwara vijijini.
Akizungumza mapema leo na waandishi wa habari, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mtwara ACP-Henry Mwaibambe, alisema katika upekuzi walioufanya juzi usiku nyumbani kwa Musa Kais, walifanikiwa kukamata Viwashio (Fuse) 44, Detonator 39, Explogel-Nusu kipande, Daftari moja la mauzo ya vifaa, fedha kiasi cha sh. 353,000 pamoja na simu moja aina ya Tecno.

Vifaa mbalimbali vya kutengeneza milipuko ya Mabomu pamoja na Milipuko yenyewe, vilivyokamatwa na jeshi la Polisi mkoa wa Mtwara, kutokana na opareshini waliyoifanya kwa kushirikiana na Marine Park pamoja na Kikosi Maalum cha Taifa cha Kushughulikia Uhifadhi wa Mazingira na Bahari.

Aidha, alisema watuhumiwa wengine katika nyakati tofauti, walikamatwa na malighafi za kutengenezea milipuko hiyo ambayo ni, Mbolea Kg 6, Kg tatu zikiwa zimechanganywa na Explogel, Chupa sita za milipuko ambazo zilikuwa tayari zimechanganywa kwa ajili ya kulipuliwa, waya wa vilipuzi wenye urefu wa mita tano na nusu na vipande vingine, pamoja na Majongoo ya Bahari 55.
“Wito kwa wananchi wa Mtwara, watu hawa ni maadui wa maendeleo ya Mkoa wa Mtwara, watu hawa ni hatari sana..ninaimani ndani ya miezi mitatu au mine ijayo kutakuwa hakuna samaki Mtwara, hivi vitu ni hatari sana na vinaharibu mazalia ya samaki na samaki wenyewe..Mtwara ni mkoa wa uwekezaji tunafahamu hayo nadhani watu ni wengi wako hapa, watu hawa ni maadui zetu wote na tusiwaone mafahari, tuwaone kuwa ni maadui..” alisema.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mtwara, ACP-Henry Mwaibambe, akionyesha baadhi ya vifaa vya kutengeneza Mabomu vilivyokamatwa na jeshi la polisi kutokana na opareshini waliyoifanya kwa kushirikiana na Marine Park pamoja na Kikosi Maalum cha Taifa cha Kushughulikia Uhifadhi wa Mazingira na Bahari.

Alisema, ni wajibu kwa wananchi wa Mtwara kushirikiana na jeshi la polisi kuweza kuutambua mtandao huo na kuwakamata, na kwamba watuhumiwa hao wanahojiwa na baada ya muda mfupi watafikishwa mahakamani.
“Naomba tuendelee kuwahamasisha wananchi, hawa watu hawafai kabisa, kuna maali nimewahi kukaa katika maisha yangu, maeneo ambayo wanatumia uvuvi wa namna hii hamna samaki kabisa..kwahiyo tushirikiane, hii vita sio ya polisi pekee ni vya jamii nzima..” aliongeza.



No comments: