Thursday, April 2, 2015

Mnyika kuongoza uzinduzi wa kanda mpya ya Chadema kusini.



John Mnyika

Na Juma Mohamed, Mtwara.

Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), John Mnyika, anatarajiwa kuzinduwa kanda ya kusini ya chama hicho mkoani hapa Aprili 12 mwaka huu.
Akizungumza na NEWS ROOM jana, Afisa wa chama hicho kanda ya kusini, Filbert Ngatunga, alisema katika uzinduzi huo, Mnyika ataambatana na baadhi ya viongozi wengine wa Kitaifa na kuungana na viongozi wa kimkoa na kanda, na wataanza na vikao vya ndani Aprili 11 kabla ya kufanya mkutano wa hadhara utakaoanza saa nane mchana katika viwanja vya mashujaa.
Mwanzo kanda ya kusini ilikuwa inaundwa na mikoa mitatu ambayo ni Lindi, Mtwara na Ruvuma ambapo makao makuu yalikua mjini Songea, mkoani Ruvuma.
Alisema, kutokana na maboresho yaliyofanywa na chama, waliamua mkoa wa Ruvuma kuuhamishia katika nyanda za juu kusini ambapo umeungana na mikoa ya Njombe, Mbeya, Iringa na Rukwa na kufanya kanda hiyo kuundwa na mikoa mitano.
“Kanda ya kusini sasa itakuwa imebaki na mikoa ya Lindi na Mtwara, ambapo sasa viongozi wengi wa hiyo kanda ya kusini walikuwa wanatoka mkoa wa Ruvuma..kwahiyo baada ya kuuhamishia nyanda za juu kusini, tunatakiwa sasa tuunde uongzi mpya wa kanda ambao utaweza kutuvusha kuanzia sasa mpaka kipindi cha uchaguzi utakapoisha.” Alisema Ngatunga.
Akifafanua zaidi alisema, kutokana na mfumo wa kanda kuwa haujakamilika katika katiba ya chama, kamati kuu iliazimia na kuunda timu maalum zitakazoshughulikia masuala ya chama kwa kipindi maalum, kwahiyo kanda hizo zimeundwa ikiwa bado hazijawekwa katika mfumo wa kikatiba wa Chadema.
Aidha, alisema kuanzia Ijumaa ya April 3 mwaka huu wataanza kufanya mikutano ya hadhara katika kata mbali mbali za mtwara manispaa na mtwara vijijini na wataanzia katika kata ya Railway, na ajenda zitakuwa ni kuwaelimisha wananchi kuhusu katiba inayopendekezwa, kutoa elimu kuhusu daftari la mpiga kura na changamoto zilizojitokeza katika zoezi la kujiandikisha katika daftari hilo mkoani Njombe.

……………………………………mwisho………………………………………………………………

No comments: