Sunday, February 8, 2015

NDANDA WAANZA MZUNGUKO WA PILI KWA SARE NYUMBANI



http://shaffihdauda.co.tz/wp-content/uploads/2014/09/IMG-20140913-WA0029.jpg

 http://4.bp.blogspot.com/-tpyjxuXI1mQ/VDApz-MXDcI/AAAAAAAApqQ/DI8GGZAI9go/s1600/HMB_8262.JPG

Na Juma Mohamed, Mtwara.
 
Timu ya soka ya Ndanda Fc ya Mkoani Mtwara imeendelea kupata matokeo yasiyoridhisha katika uwanja wake wa nyumbani wa Nangwanda Sijaona, baada ya hapo jana kujikuta wakibanwa mbavu na Stand United ya Shinyanga na kulazimishwa sare ya kufungana goli 1-1, katika mchezo wao wa mzunguko wa pili wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania bara.
Ndanda waliuanza mchezo huo taratibu kama kawaida yao huku wakiwasoma wapinzani wao ambao walionekana kucheza kwa kasi kutafuta goli la mapema ambalo walifanikiwa kulipata kunako dakika ya tisa mfungaji akiwa ni Chidiebele Abasilim, baada ya uzembe uliofanywa na walinzi wa Ndanda kwa kushindwa kumzuia mfungaji wakijua atakuwa ameotea ndipo alipomlamba chenga golikipa na kuukwamisha mpira kimiani.
Baada ya hapo Ndanda walijaribu kufanya mashambulizi kadhaa langoni mwa Stand wakitaka kusawazisha lakini ilishindikana na kujikuta wanakwenda mapumziko wakiwa nyuma kwa goli hilo moja.
Baada ya mwamuzi Michael Magori aliyekuwa akichezesha mchezo huo akisaidiwa na Omari Kambangwa na Kasimu Mpanga, kupuliza filimbi ya kuanza kipindi cha pili, iliwachukuwa dakika nane tu Ndanda kusawazisha goli lililofungwa na Nassoro Kapama akiwazidi ujanja walinzi wa Stand United.
Ndanda walionekana kucheza kwa kasi na kuutawala mchezo kipindi cha pili ambapo walifika mara kadhaa langoni mwa wapinzani wao lakini mashambulizi yao yaliishia mikononi mwa golikipa Mohamed Makaka wa Stand United na mengine kuokolewa na walinzi huku shuti moja likigonga mwamba na kutoka nje.
Timu zote mbili zilijaribu kufanya mabadiliko, Nanda waliwatoa Masoud Ally, Gideon Benson na Kiggi Makasi na nafasi zao kuchukuliwa na Ibrahim Mwaipopo, Saidi Issa na Rajabu Isihaka, huku Stand United wakiwatoa Mathias Thabit, Hery Mohamed na Hamis Shengo na nafasi zao zikachukuliwa na Abou Ubwa, Danny Manyenye na Shabani Kondo, lakini licha ya mabidiliko hayo y timu zote mbili, mchezo huo mpaka dakika 90 zinamalizika matokeo yalibaki kuwa goli 1-1.
Baada ya mchezo kumalizika, makocha wa timu zote mbili walizungumza, kwa upande wa kocha wa Stand United, Mathias Lole, alisema mchezo ulikuwa mzuri na akisifu pia waamuzi kuchezesha vizuri. “kwa mara yangu ya kwanza, naona waamuzi wakichezesha vizuri sana..kwa upande wa Ndanda walikuwa vizuri, walikuwa na ‘sistimu’ mzuri..tulifunga kwanza wao wakaja wakasawazisha, ila kiujumla mchezo ulikuwa mzuri.” Alisema Lole.
Aliongeza kuwa “kupoteza nafasi ni kawaida na kila mtu anaweza kupoteza nafasi, kwakuwa mchezo wa mpira wa miguu ni mchezo wa makosa.” Alisema.
Akizungumzia mabadiliko yao ya mwisho waliyoyafanya katika dakika nne za nyongeza ambapo mchezaji aliyetakiwa kutoka alikuwa ni Reina Mgungira mwenye jezi nambari 16, lakini akajifanya hajui kama yeye ndio anaetakiwa kutoka licha ya kibao cha mwamuzi wa mezani kuonesha kuwa yeye ndio anaetakiwa kutoka, baadala yake wakalazimisha atoke Hamisi Shengo mwenye jezi nambari 28, na ilichukuwa karibu dakika moja na nusu mpaka Shengo kutoka uwanjani, Lole alisema hiyo ilikuwa ni mbinu tu ya mchezo “yalikuwa ni maandalizi tu yakiufundi ambayo tuliyaandaa..na tulilazimika kufanya vile kwakuwa presha ilikuwa kubwa.” Aliongeza Lole.
Aidha kwa upande wake Kocha wa Ndanda Fc Meja Mstaafu Abdul O. Mingange, alisema mechi ilikuwa ni ngumu sana kwa upande wao na kwamba ni bora hata ucheze na Yanga au Simba. “ni mechi ngumu..lakini na madharau tu ya wachezaji wangu kama ulivyoona, wachezaji wanadharau mechi wanaona kama ni timu ndogo..na hili ni tatizo la wachezaji wa Tanzania, hawaelewi na hawajui umuhimu wa kucheza ligi nyumbani na ugenini.” Alisema Mingange.
Kuhusu mfululizo wa matokeo yasiyoridhisha wanayoyapata katika uwanja wa nyumbani, kocha huyo alisema haoni kama ni matokeo mabaya sana, kwasababu amepata pointi moja katika mchezo huo na walishawahi kushinda huko nyuma katika mechi dhidi ya Azam.
Kwa upande wa mashabiki wa Ndanda Fc wameonesha kutofurahishwa na matokeo ambayo timu yao inayapata katika uwanja huo na kuyaita matokeo ya aibu na hayafai kuyapata katika uwanja wa nyumbani.
“Mimi namuomba kocha wangu ajipange, aiandae vizuri timu ili tufanye vizuri katika mechi zijazo kwasababu hapa ni nyumbani..kwa matokeo tunayoyapata hapa kwakweli ni aibu, tatizo labda ni wachezaji wetu wakiwa hapa ‘hawakazi’ tofauti na ugenini au labda kuna vitu vingine ambavyo havijulikani havijioneshi ndani nyake..mimi nahisi tu labda ni u-siasa siasa tu labda unaingia.” Alisema shabiki mmoja wa Ndanda aliejitambulisha kwa jina moja la Nurudini.
Aliongeza kuwa “labda ushindani tu wa wanasiasa, kwasababu hapa inasemekana kuna ushindani wa wanasiasa wawili maana mara ya kwanza mmoja alikuwa anaimiliki timu ambaye ni mheshimiwa Mbunge (Asnain Murji) na mara ya pili kuna Mbunge mwingine anaisaidia timu (Hawa A. Ghasia), sasa labda ni hao..wote wanaisaidia timu ila naona kama kuna mvutano..sasa kama tatizo ni hao basi tunawaomba wajirekebishe kwakweli, kwasababu kila tukija hapa tunaambulia matokeo ya sare au kufungwa, mashabiki inatuumiza kwakweli.” Alisema Nurudini.
Mtandao huu unafahamu kuwa awali Mbunge wa Mtwara Mjini Asnain Murji alikuwa anaisaidia Ndanda Fc kwa kutoa mabasi yake kuwasafirisha mashabiki kwenda kuishangilia timu pindi inapokwenda kucheza ugenini lakini kwa sasa huduma hiyo ameisitisha japo haijafahamika sababu za msingi za kufanya hivyo. Pia Mtandao huu unafahamu kuwa timu hiyo kwa sasa inasaidiwa na Mbunge wa Mtwara Vijijini na Waziri wa Tamisemi, Mhe. Hawa A. Ghasia ambae anatoa posho kwa wachezaji kila wiki kiasi cha sh. Milioni 1.2. Tunaahidi kulifuatilia kwa kina suala hili la u-siasa unaotajwa kuingia ndani ya timu ya Ndanda na kuwasababishia kupata matokeo yasiyoridhisha katika uwanja wa nyumbani.
Kiuhalisia, timu ya Ndanda haijapata matokeo yakuridhisha katika mechi zake zote ambazo imecheza katika uwanja wa nyumbani wa Nangwanda Sijaona isipokuwa mechi moja pekee waliocheza Novemba 01, mwaka jana dhidi ya Azam na kushinda goli 1-0.
Mechi ya jana dhidi ya Stand United ilikuwa ni mechi yao ya 14 katika mechi zote za Ligi Kuu walizocheza msimu huu, na kati ya hizo mechi sita wamecheza nyumbani na kushinda moja tu dhidi ya Azam, mechi tatu wamefungwa ambazo ni dhidi ya Ruvu Shooting 3-1, JKT Mgambo 1-0 na Simba 2-0. Mechi walizotoa sare ni mbili, ambazo ni dhidi ya Polisi Moro 1-1 na Stand United 1-1.
Katika mchezo wa jana Ndanda waliwakilishwa na Wilbert Mweta, Azizi Sibo, Paul Ngalema, Kasian Ponera, Hemed Khoja, Omega Seme, Jacob Masawe, Masou Ally, Nassoro Kapama, Gideon Benson na Kiggi Makasi.
Stand United walikuwa, Mohamed Makaka, Revocatus Richard, Yasin Mustapha, Iddy Mobby, Peter Mutabuzi, Reina Mgungira, Hanuna Chanongo, Hamisi Thabit, Chidiebele Abasilim, Hery Mohamed na Hamis Shengo.

............................................mwisho...............................................................

No comments: