Sunday, February 8, 2015

PPF WAKABIDHI MSAADA WENYE THAMANI YA SH. MILIONI 5 KWA WAHANGA WA MAFURIKO.

http://www.tic.co.tz/media/PPF.png

 
Na Juma Mohamed, Mtwara.
 
Shirika la Hifadhi ya Jamii (PPF) limekabidhi msaada wa vyakula vyenye thamani ya shilingi milioni 5, kwa ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Mtwara kwa lengo la kuwasaidia waathirika wa mafuriko.
Ofisa Huduma kwa Wateja Kanda ya Kusini, Liliani John Mhina amesema vyakula walivyokabidhi ni Unga, Maharage na Mchele ambavyo vyote kwa ujumla vina thamani ya shilingi milioni 5.
“Jumla ya msaada wote tuliokabidhi ni tani tatu na nusu ambapo Unga ni mifuko 90, mchele ni gunia 10 ambazo kila gunia moja lina kg 100 na maharage ni gunia nne ambazo kila gunia moja lina kg 100.” Alisema Liliani.
Aidha kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Mtwara bwana Wilmani Ndile, baada ya kupokea msaada huo alitoa shukrani zake kwa PPF na kusema kuwa waliamua kupeleka maombi kutokana na kaya nyingi kuathirika na mafuriko na kuwasababishia kukosa chakula.
“Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ilipeleka taarifa ya kuomba msaada kutokana na mafuriko. PPF walipokea na kulifanyia kazi, na ilichukuwa siku nne tu toka tupeleke maombi na wao kuanza kuyafanyia kazi, kwahiyo Jumatatu tutapeleka barua rasmi ya kukiri kupokea msaada. Na tulifanya hivyo baada ya kubaini kuwa waathirika wa chakula ni wengi.” Alisema Ndile.
Ndile aliongeza kuwa kaya zilizoathirika ni 900 na kwa mtu mmoja mmoja ni zaidi ya wananchi elfu tatu (3,000) ambapo ameahidi kuwafikishia msaada huo walengwa.
“Tumepata ‘sapoti’ ya chakula kiasi cha tani 73.5 ambazo ni kama gunia 730 za mahindi mpaka sasa ikiwa ni pamoja na kusafirishiwa, tumepewa fedha kiasi cha shilingi milioni 36 za kununulia maharage kwa ajili ya chakula. Na wananchi wajue kwamba kwanzia kesho (jana) tunaanza kugawa chakula” Aliongeza Ndile.
Akizungumzia miundombinu ya Manispaa ya Mtwara, Ndile alisema bado wanasubiri msaada mwingine kwa ajili ya kuboresha miundombinu kutoka kwa wahisani wengine ikiwa ni pamoja na Ofisi ya Waziri Mkuu. Alisema kuhusu ujenzi wa mfereji mkubwa wa maji uliopo kata ya Kiyanga, Manispaa ya Mtwara, ni kwamba wiki ijayo utakuwa unakamilika na kwamba ni mradi mkubwa ambao una thamani ya shilingi 1 bilioni.
Manispaa ya Mtwara ilikumbwa na mafuriko mwezi uliopita na kuathiri miundombinu ya mji, pamoja na kaya zipatazo 900 ambapo ilipelekea wananchi kukosa baadhi ya mahitaji muhimu ikiwa ni pamoja na chakula na malazi.
 
…………………………………….mwisho……………………………………………………

No comments: