Friday, April 15, 2016

Mbunge aitaka TANESCO kukamilisha miundombinu ya umeme Mtwara mjini.



Mbunge wa Mtwara mjini (CUF), Maftaha Nachuma, akiwahutubia wakazi wa kata ya Naliendele waliojitokeza katika mkutano wa hadhara ulioitishwa na Mbunge huyo kwa ajili ya kuwapongeza wapiga kura wake kwa kumchagua

Wakazi wa kata ya Naliendele waliohudhuria mkutano wa hadhara wa Mbunge wa Mtwara mjini (CUF), Maftaha Nachuma, uliokuwa na lengo la kuwapongeza wapiga kura wake kwa kumchagua kuwa mbunge.


Na Juma Mohamed, Mtwara.

MBUNGE wa Mtwara mjini kupitia Chama cha Wananchi (CUF), Maftaha Nachuma, amesema iwapo Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) litashindwa kufikisha umeme katika maeneo yaliyosalia katika jimbo lake mpaka kufikia mwezi Julai mwaka huu, zitatumika nguvu za umma kwa kufanya maandamano kudai huduma hiyo.
Akizungumza katika mkutano wa hadhara uliofanyika Naliendele wa kuwapongeza wapiga kura wake kwa kumchagua kuwa mbunge, alisema hatua inatokana na ahadi iliyotolewa na serikali kupitia bodi ya TANESCO ambapo iliahidi kumaliza kero ya kukosa miundombinu ya umeme kwa maeneo yaliyobaki katika Manispaa ya Mtwara Mikindani ifikapo mwezi Julai mwaka huu.
“Ni ahadi ya serikali kupitia bodi ya TANESCO Tanzania, bodi ya TANESCO Tanzania imahidi ya kwamba ifikapo mwezi wa saba kila kona ya Mtwara mjini kwakuwa gesi inatokea Mtwara mjini (Mnazibay) umeme utafika ili wananchi washindwe wenyewe kujiunganishia umeme, ahadi ya serikali ni lazima waitekeleze ahadi hiyo..” alisema.

Wakazi wa kata ya Naliendele waliohudhuria mkutano wa hadhara wa Mbunge wa Mtwara mjini (CUF), Maftaha Nachuma, uliokuwa na lengo la kuwapongeza wapiga kura wake kwa kumchagua kuwa mbunge.


Alisema, kupitia kamati ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma ambaye yeye ni mjumbe, ilishawahi kuwaita viongozi wa TANESCO na kuwauliza maswali kadhaa ikiwa ni pamoja na kutaka kujua kwanini maeneo yaliyopo ndani ya manispaa ya Mtwara hayana umeme wakati mitambo ya kuzalisha huduma hiyo ipo ndani ya manispaa hiyo.
Alisema viongozi hao walionekana kukosa majibu kwa baadhi ya maswali walioulizwa, huku akiyataja baadhi ya maeneo hayo kuwa ni Naliendele, Comoro, Mbawala Chini, Miseti na Miembeni.
Aidha, juu ya ofa iliyotolewa na serikali kwa wananchi wa mikoa ya Mtwara na Lindi kuvuta umeme majumbani mwao kwa gharama ya sh. 99,000, alisema wapo baadhi ya watendaji wa TANESCO wanaishawishi serikali kupandisha gharama hiyo na kufikia katika kiwango cha kitaifa cha sh. 177,000.

Mbunge wa Mtwara mjini (CUF), Maftaha Nachuma, akisoma dua bada ya kwenda kudhuru kaburi la  aliyekuwa kaimu mwenyekiti wa CUF kata ya Naliendele, Dismas Mnyale.


“Kuna watendaji wa TANESCO baadhi yao wanakaa na kuiambia serikali iongeze bei na ile ofa iwe mwisho, nilizungumza kwenye kamati ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma tulipowaita bodi ya TANESCO kwamba gesi bado ipo Kusini na popote panapotoka gesi ambayo inalinufaisha Taifa zima, pale panapotoka gesi lazima wanufaike nae kwa kiasi kikubwa..” alisema.
Kwa mujibu wa afisa habari wa shirika hilo, Leila Muhaji, alisema ofa hiyo ambayo awali ilikuwa ifikie mwisho Machi 31 mwaka huu, bado inaendelea na kwamba wananchi wa mikoa hiyo wataendelea kunufaika nayo.



No comments: