Thursday, January 14, 2016

Kasi ya wanaojiandikisha darasa la kwanza yawatisha walimu wakuu Mtwara.



Wanafunzi wa shule ya msingi Kambarage, manispaa ya Mtwara Mikindani wakiwa katika harakati za usafi wa mazingira ya shule yao kabla ya kuingia darasani jana baada ya kufungua shule


Na Juma Mohamed, Mtwara.

BAADHI ya shule za msingi katika manispaa ya Mtwara Mikindani zimeonyesha wasiwasi wao juu ya kasi ya wanafunzi wanaojiandikisha na darasa la kwanza kuwa kubwa na kuhofia kuzidi idadi inayokidhi mahitaji yao ya shule, jambo ambalo litapelekea baadhi ya wanafunzi kukosa vyumba vya madarasa na madawati.
Wakizungumza na Nipashe kwa nyakati tofauti, walimu wa kuu wa shule za Kambarage na Ligula mjini hapa walisema kutokana na waraka wa elimu uliowafikia katika shule zao kuwataka wasiwakatae wanafunzi, watalazimika kuwapokea hatakama watafikia idadi inayokidhi mahitaji ya shule.
Hawana Nacha, ambaye ni mwalimu mkuu wa shule ya msingi Kambarage, alisema mpaka kufikia jana asubuhi tayari walikuwa wameshawapokea watoto 120 na bado wanaendelea kuwapokea wengine huku mahitaji ya shule ilikuwa ni watoto 100 kulingana na vyumba vilivyopo.
“Tumepokea kulingana na waraka unavyosema, kwamba motto inabidi apokelewe na apokelewe Yule ambaye yupo maeneo ya jirani na shule husika..wanaozidi tutawachomeka humo humo ikishindikana watakaa nje watasoma huko, sasa hapo husipopokea lazima kuna litalokukuta na hao wote wanatoka jirani na shule..” alisema.
Alisema, licha ya mwaka huu kuwa na fursa ya elimu kutolewa bure, lakini kwa shule hiyo imekuwa ni kawaida kwa wanafunzi kuwa wengi ambapo walikuwa wanalazimika kuwapokea huku wengine wakikaa chini kwa kukosa madawati.
Aliitaka serikali kuboresha miundombinu ya shule hiyo kwa kuongeza madawati, walimu na vyumba vya madarasa ambapo jumla ya walimu waliopo ni 19 huku mahitaji ni walimu 25 na kutokana na wanafunzi wa darasa la awali kukosa chumba, wamelazimika kuchukua ofisi ya walimu kuifanya darasa.
Naye mwalimu mkuu wa shule ya msingi Ligula, Angela Kariko, alisema shule yake ilikuwa ina mahitaji ya wanafunzi 100 lakini kutokana na kasi ya kuwapokea wanafunzi wapya wa darasa la kwanza inavyokwenda kuna uwezekano wa kuzidi idadi hiyo ambapo mpaka kufikia jana asubuhi walikuwa wameshawapokea wanafunzi 95.
Alisema hiyo ni changamoto kubwa kwa shule hiyo ambayo inaweza kusababisha baadhi ya wanafunzi kukosa vyumba vya kusomea na hata madawati huku pia kukiwa na uhaba wa walimu.
“Kwasababu lengo ni watoto wote waingie darasani na wapate masomo tutawaingiza katika vyumba hivi hivi vya madarasa vilivyopo na tutaendelea kuwafundisha huku tukikabiliana na changamoto huku tukieleza ngazi zingine watusaidie..” alisema Sofia Selemani, ambaye ni mratibu wa shule.
Kuhusu fedha za kuteleza mpango wa elimu bure, alisema tayari zimeshaingizwa katika akaunti za shule lakini hawajui ni kiasi gani kutokana na kwamba bado hawajaenda benki kuangalia.
Kwa upande wa shule ya sekondari ya Mtwara Ufundi, walisema tayari wameshapokea fedha kiasi cha sh. Milioni 33 za kutekeleza mpango wa elimu bure zilizotolewa kwa ajili ya matumizi ya mwezi nzima.
Akizungumza ofisini kwake, kaimu mkuu wa shule hiyo, Ahmed Nachundu, alisema mpango huo umesaidia kurahisisha baadhi ya majukumu katika ofisi ya msajili katika kipindi hiki cha kupokea wanafunzi wapya ikiwa ni pamoja na zoezi la ulipaji ada na kufuatilia maagizo mengine yanayohitajika kwa wanafunzi.
“Lakini sasa hivi kutokana na mwongozo uliopo, mwanafunzi anakuja na kila kitu kwasababu ada halipi, anakuja na yunifomu, godoro anakuwa ameshanunua hukohuko, hakuna kuja na jembe, fagio wala kifaa chochote..kwahiyo utofauti ndio huo ukilinganisha na miaka ya nyuma..” alisema.
Baadhi ya wazazi walioambatana na watoto wao kwa ajili ya kwenda kuwaandikisha elimu ya msingi, walielezea furaha yao juu ya mpango huo na kusema umesaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza majukumu ya mzazi kwa mwanafunzi, huku wakikiri kuto takiwa kuchangia kitu chochote zaidi ya kutekeleza wajibu wao wa kuwaandaa watoto kwa yunifomu, daftari na kalamu.
Kuhusu changamoto zilizoelezwa na walimu wa shule za Kambarage na Ligula, kaimu mkurugenzi wa manispaa ya Mtwara Mikindani, Donald Soko, alisema licha ya changamoto hizo, walimu wanatakiwa kuendelea kuwapokea wanafunzi kama maagizo yanavyosema na kwamba kama kuna changamoto zozote wanatakiwa kuwasiliana na uongozi wa manispaa.
Alisema, manispaa itajua cha kufanya maana inawezekana kuna shule nyingine ambazo hazitafikisha idadi ya mahitaji ya shule, hivyo kwa wale watakaozidi itabidi watafutiwe shule nyingine ambazo zitakuwa na nafasi.
“Mimi nadhani wasiwe na wasiwasi sana kwasababu inawezekana labda wazazi wamehamasika na kupeleka watoto shule, kwahiyo wasijenge dhana kwamba ni lazima watoto wazidi, inamaana kama watoto watazidi kwa kiwango hicho cha 100 ambacho wao watakihimili basi wawasiliane na uongozi wa manispaa..” alisema.



No comments: