Thursday, October 29, 2015

MTWAREFA walia na mapato kiduchu Nangwanda-Mtwara, ligi kuu.

Waamuzi wakiwaongoza wachezaji wa timu za Ndanda na Stand Utd kuelekea uwanjani tayari kwa kuanza mchezo wa ligi kuu katika uwanja wa Nangwanda Sijaona juzi mkoani Mtwara.


Kiungo wa Stand Utd, Jackob Masawe, akimtoka mshambuliaji wa Ndanda Fc, Thomas Morris wakati wa mchezo wa ligi kuu juzi katika uwanja wa Nangwanda, Mtwara. Timu hizo zilitoka suluhu ya 0-0




Mshambuliaji wa Ndanda Fc, Atupele Green, akijaribu kumtoka mlinzi wa Stand Utd, katika mchezo wa ligi kuu ya Tanzania bara juzi katika uwanja wa Nangwanda Sijaona, Mtwara.


Baadhi ya watazamaji waliojitokeza katika uwanja wa Nangwanda Sijaona, Mtwara juzi kushuhudia mchezo wa ligi kuu ya Tanzania Bara, kati ya Ndanda na Stand Utd.


Baadhi ya watazamaji waliojitokeza katika uwanja wa Nangwanda Sijaona, Mtwara juzi kushuhudia mchezo wa ligi kuu ya Tanzania Bara, kati ya Ndanda na Stand Utd.



Na Juma Mohamed.

CHAMA cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Mtwara (MTWAREFA), kimelalamikia mapato finyu yanayopatikana katika uwanja wa Nangwanda Sijaona mkoani hapa, yanayotokana na michezo mbalimbali ya ligi kuu ya Tanzania Bara inayoihusisha timu ya soka ya Ndanda Fc.
Akizungumza leo ofisini kwake, katibu wa chama hicho, Charles George, alisema uchache huo wa mapato unatokana na idadi ndogo ya watazamaji wanaoingia uwanjani wakati timu ya Ndanda inacheza hasa na timu ambazo hazina majina makubwa kama ilivyo kwa Simba, Yanga na Azam.
Alisema, MTWAREFA inajikuta ikiingia katika madeni na baadhi ya wadau na taasisi kadhaa kutokana na ukosefu wa mapato, ambapo hadi sasa ni zaidi ya sh. 500,000 wanadaiwa kwa kukosa fedha katika mechi za Ndanda dhidi ya Toto Africans, Azam na Stand Utd.
“Sisi kama Mtwarefa kwakweli tunapata wakati mgumu sana kuweza kukamilisha taratibu zote za maandalizi ya mchezo, tunafanya kazi kwa kusuasua kwakweli, hata hizi asilimia 8 za mchezo ambazo tunapata ni hela ndogo sana kiasi kwamba tunashindwa kulipa..kwasababu katika gharama za mchezo, inatakiwa ulipe polisi, huduma ya kwanza, gari la wagonjwa, waokota mipira, wauzaji na wakaguzi wa tiketi na vituo vya kuuzia tiketi..” alisema.
Alisema, katika madeni wanayodaiwa hadi sasa kutokana na gharama za michezo kuanzia mchezo wa Ndanda na Toto Agricans na Azam na Stand Utd ni zaidi ya sh. 500,000 ambapo katika mchezo dhidi ya Toto deni lilikuwa ni sh. 282,000 huku mchezo wa juzi dhidi ya Stand wanadaiwa sh. 242,000.
“Tutapata wapi hatujui, lakini hawa watu walifanya kazi walionekana na sisi tunakubali kama tuliwaandaa kwa ajili ya kufanya shughuli ya maandalizi ya mchezo, kwahiyo lazima tutafute fedha za kuwalipa, lakini tutawalipa lini hiyo tutaangalia kadri ya uwezekano utakavyokuwa..” alisema.
Aidha, katibu huyo amekiri kuwa na changamoto ya kukosa vyanzo mbadala vya mapato tofauti na kutegemea mapato ya mlangoni, na kwamba chama kinajitahidi kupitia vikao vyao kuandaa vyanzo vingine vitakavyosaidia kupata fedha nje ya viingilio.
Aidha, akizungumzia mapato yaliyopatikana katika michezo miwili iliyopita kati ya Ndanda na Azam, na ule wa Ndanda na Stand, alisema michezo hiyo jumla iliingiza kiasi cha sh. Milioni 6.9.
Ndanda na Azam uliingiza sh. 5,041,000 ambapo klabu mwenyeji ambayo ni Ndanda ilipata sh. 1,192,000  huku Azam wakiambulia kiasi cha sh. 851,000, na kwamba katika mchezo wa juzi dhidi ya Stand timu hizo ziliingiza kiasi cha sh. Milioni 1.9 huku klabu mwenyeji ikipata sh. 359,000 na wageni walipata sh. 256,000.
Wakati huo huo, Mtwarefa iliwataka makatibu wa vyama vya soka vya wilaya zote kuwasilisha taarifa zao za ligi za wilaya ikiwa ni pamoja na idadi ya timu shiriki, msimamo na mabingwa mapema ambapo mpaka kufikia Novemba 5 mwaka huu wawe wameshawasilisha.
“Taarifa za simu sio sahihi, walete kwa maandishi, mwisho tarehe 5 saa 10 jioni, wilaya yeyote ambayo haitoleta ‘ripoti’ ya ligi ya wilaya ifikapo saa 10:01 siku hiyo hatuwezi kuipanga kwenye ratiba ya ligi ya mkoa.
Alisema, kwamujibu wa kalnda, ligi ya mkoa ilitakiwa iwe tayari imeshaanza kama ilivyo katika mikoa mingine, lakini imechelewa kutokana na wilaya zote kuwa bado hazijawasilisha taarifa zake za ligi zao.
“Wanitumie haraka iwezekanavyo ili kamati ya utendaji ikianzia katika kamati ya ligi ya mkoa iweze kukaa hara na kupitia hizo taarifa kwa ajili ya kuanza kuchezesha hiyo ligi ya mkoa..” aliongeza.





No comments: