Thursday, March 26, 2015

DC NEWALA ATOA SOMO KWA VIJANA

Mkuu wa wilaya ya Newala, Christopher Maghalla
Christopher Maghalla na Mweka Hazina wa MRENGO, Mustafa Kwiyunga
Wadau waliohudhuria warsha ya kutathimini fursa na changamoto zinazowakumba vijana katika kujiletea maendeleo ngazi ya jamii, wilayani Newala.
Na Juma Mohamed, Newala.
VIJANA wilayani Newala wametakiwa kujihusisha na shughuli za ujasiliamali ili kuweza kujikwamua kimaisha na kuepukana na hali ya umasikini inayowakabili vijana wengi wasiyojishughulisha hapa nchini.
Wito huo umetolewa na Mkuu wa Wilaya ya Newala, Christopher Maghalla, wakati akifungua warsha ya kutathimini fursa na changamoto zinazowakumba vijana katika kujiletea maendeleo katika ngazi ya jamii, iliyoandaliwa na mtandao wa asasi isiyo ya kiserikali (NGO) ya MRENGO ya mkoani Mtwara, iliyofanyika katika ukumbi wa haspitali ya wilaya ya Newala.
Alisema serikali inahamasisha vijana waungane katika makundi mbalimbali ili iweze kuwasaidia kwa lengo la kutatua changamoto za kiuchumi ambazo zimekuwa zikiwakumba vijana wengi hapa nchini, kiasi cha kupelekea wengine kujihusisha na vitendo visivyokubalika vya uvunjifu wa sheria.
"Serikali kupitia Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto na Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo inatenga bajeti kila mwaka kwa ajili ya kuwasaidia vijana..hii ni kuonesha ni jinsi gani serikali yetu inajali masilahi ya vijana." alisema Magalla.
Aidha, Mkuu huyo wa Wilaya alitoa mfano yeye mwenyewe namna ambavyo alijipatia elimu ya sekondari, kuwa ni kutokana na juhudi zake mwenyewe ambapo aliamua kuungana na kaka yake na kuanza kufanya shughuli ya kusukuma mkokoteni kwa kupeleka nyanya sokoni na baadae ikamsaidia kujipatia kipato ambacho aliamua kuanza shughuli za kilimo cha zao hilo.
Alisema kutokana na kipato alichokuwa akipata kutokana na kuvuna nyanya, kilimuwezesha kufungua saluni, na baadae kujikuta akisoma bila vikwazo vyovyote vya kipato na kutokuwa na utofauti kati yake na watoto waliotoka katika familia za kitajiri.
Katika hatua nyingine, Magalla amewataka wananchi wote wa wilaya ya Newala na maeneo mengine kujitokeza kwa wingi katika zoezi la kujiandikisha katika daftari la wapiga kura, na wale wanaojiona kuwa na vigezo vya kugombea nafasi mbalimbali za uongozi wafanye hivyo, kwani kwa kufanya hivyo itasaidia nchi kuepukana na kuwa na viongozi mafisadi na wasiokuwa na maadili.
Kwa upande wake, mratibu wa warsha hiyo, Shaibu Kasulo, alisema warsha hiyo inafanyika chini ya mradi wa Fahamu, Ongea, Sikilizwa Election (ii) ambao unaangalia masuala mbalimbali ikiwa pamoja na swala la kupiga kura, kujiandikisha katika daftari la wapiga kura pamoja na kufanya tafiti mbalimbali kuhusu wananchi wanavyoshiriki katika upigaji kura.
Alisema mradi umegundua kuwa asilimia kubwa ya wananchi ambao ushiriki wao ni mdogo katika upigaji kura ni vijana na akina mama. Alitoa takwimu za jumla za namna wananchi walivyosiriki katika zoezi la upigaji kura, ambapo alisema katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2000, ushiriki ulikuwa ni kwa asilimia 84.4, mwaka 2005 ulikuwa kwa asilimia 72.4 na mwaka 2010 ni asilimia 42.8 hivyo kuonekana ushiriki wa wananchi unazidi kupungua kadiri miaka inavyozi kwenda.
..............................mwisho.......................................................................

No comments: