Wednesday, September 24, 2014

MWANZO MBAYA KWA VIGOGO WA SOKA TZ KATIKA VPL



Na Juma Mohamed

MZUNGUKO wa kwanza wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania bara imekamilika Jumapili ambapo jumla ya mabao 18 yamefungwa ikiwa ni michezo ya kwanza kwa timu zote 14 zinazo shiriki Ligi hiyo.
Mechi hizo za kwanza zimeonyesha maajabu makubwa ambayo huenda yakazidi kushangaza wadau wa soka msimu huu kwa timu ngeni katika ligi hiyo Ndanda FC,kutoka Mtwara kuongoza ligi baada ya kuwafunga wageni wenzao Stend United mabao 4-1,huku bingwa Mtetezi Azam ikishinda mabao 3-1
Simba na Yanga zilizokuwa zikipewa nafasi kubwa ya kufanya vizuri kwenye mechi zao za awali mambo yalikuwa magumu kwao baada ya kujikuta zikikabwa koo Yanga iliyokuwa ugenini Jamuhuri Morogoro ilifungwa mabao 2-0 na Mtibwa Sugar na Simba ikatoka sare ya 2-2 na Coastal Union siku iliyofuata Jumapili.
Mbeya City ambayo ilikuwa tishio katika ligi hiyo nayo mambo hayakywa mazuri Jumamosi baada ya kulazimishwa sare ya bila kufungana na Maafande wa JKT Ruvu inayofundishwa na kocha wa zamani wa Yanga Fredy Felix Minziro wakati siku hiyo Mgambo JKT ikatoa kipigo cha bao 1-0 kwa Kagera Sugar kwenye uwanja wa Mkwakwani Jijini Tanga.
Ruvu Shooting, ya Pwani nayo ilianza ligi hiyo vibaya msimu huu baada ya kufungwa nyumbani mabao 2-0 na Tanzania Prisons,matokeo ambayo yamemuumiza mno kocha wake Mkenya Tom Olaba kutokana na maandalizi ambayo wameyafanya kuelekea msimu huu.
Lakini matokeo hayo kwa kifupi yanaonyesha uhalisia wa ligi ya msimu huu wa 2014/2015, itakavyokuwa ngumu na yenye ushindani kutokana na timu nyingi kufanya maandalizi mazuri tofauti na ilivyokuwa misimu iliyopita.
Misimu iliyopita ilikuwa vigumu kuona timu ikipata ushindi ugenini lakini katika mechi za kwanza msimu uliopita katika mechi saba zilizo chezwa siku ya ufunguzi Jumamosi timu mbili za Ndanda Fc na Tanzania Prisons zilipata ushindi ugenini huku JKT Ruvu na Coastal Union iliyocheza na Simba Jumapili kwenye uwanja wa taifa zikipata sare ugenini.
Hii inaonyesha namna ambavyo soka la Tanzania linavyo piga hatua kwa kasi kadiri siku zinavyokwenda lkwa sababu misimu iliyopita ilikuwa siyo rahisi kuona Yanga au Simba zikipoteza mechi za awali kama ilivyotokea msimu huu.
Raundi ya pili itaendelea Jumamosi hii ambapo Simba itaendelea kubaki Dar es Salaam kwenye uwanja wa taifa kuwakabili Polisi Moro, ambayo ilifungwa mabao 3-1 na Azam katika mechi ya ufunguzi,Vinara Ndanda FC,bado watakuwa ugenini Morogoro kucheza na wababe wa Yanga Mtibwa Sugar na Azam siku hiyo itacheza na Ruvu Shooting kwenye uwanja wake wa Azam Complex Chamazi.
Mbeya City nao wataendelea kubaki nyumbani uwanja wa Sokoine Mbeya kuialika Coastal Union na mchezo wa mwisho siku hiyo utapigwa kwenye uwanja wa Mkwakwani Tanga wakati wenyeji Mgambo JKT watakapoikaribisha Stend United kutoka Mkoani Shinyanga.
Jumapili kutakuwa na mechi mbili zote zikifanyika mkoa wa Dar es Salaam Yanga iliyofungwa mabao 2-0 na Mtibwa itakuwa uwanja wa nyumbani wa taifa kuwaalika Tanzania Prisons na JKT Ruvu itakuwa mwenyeji wa Kagera Sugar kwenye uwanja wa Azam Complex.

SOURCE: GOAL.COM

No comments: