Thursday, July 5, 2012

NYOSSO APEWA MKATABA MPYA SIMBA SC


Juma Nyosso

BEKI wa Simba SC, Juma Said Nyosso amesaini mkataba wa mwaka mmoja kuendelea kuichezea klabu hiyo, baada ya mkataba wake awali kumalizika, hivyo kumaliza tetesi kwamba anaweza kuhamia kwa watani wa jadi, Yanga SC.
Makamu Mwenyekiti wa Simba SC, Geoffrey Nyange ‘Kaburu’ ameiambia BIN ZUBEIRY mchana wa leo kwamba, Nyosso alisaini mkataba huo Julai 1, mwaka huu.
Kaburu alisema kwamba Simba ina imani na beki huyo wa timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars na ndio maana imemuongezea mkataba.
Aidha, Kaburu aligusia suala la beki wao, Kelvin Yondan aliyehamia kwa watani wa jadi, Yanga akisema kwamba bado ni mchezaji wao halali na wamekwishapeleka malalamiko yao Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), wanasubiri majibu.
Kaburu pia amesema mshambuliaji wa kimataifa wa Zambia, Felix Sunzu tayari amejiunga na wenzake kambini visiwani Zanzibar, ambako timu hiyo inashiriki Kombe la Urafiki.
Kaburu amesema Simba itaendelea kuwa Zanzibar hata baada ya michuano hiyo, wakijiandaa na Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame, ambalo linatarajiwa kuanza kutimua vumbi Julai 14, Simba wakifungua dimba na URA ya Ugandea Julai 16.

MAREFA WA KOMBE LA YANGA WATAJWA


Marefa wa Kagame mwaka jana, wakisindikizwa na
Polisi kwa usalama wao, baada ya maamuzi yao kutowafurahisha mashabiki
 
BARAZA la Vyama vya Mpira wa Miguu Afrika Mashariki na Kati (CECAFA) limeteua waamuzi 15 kuchezesha michuano ya Kombe la Kagame itakayofanyika jijini Dar es Salaam kuanzia Julai 14-28 mwaka huu.
Waamuzi hao wanatakiwa kuwasili Dar es Salaam, Julai 11 mwaka huu kwa ajili ya vipimo vya afya na mtihani wa utimamu wa viungo utakaofanyika Julai 12 na 13 mwaka huu Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam chini ya wakufunzi wa CECAFA.
Kwa upande wa waamuzi wa kati (centre referees) walioteuliwa ni Anthony Ogwayo (Kenya), Dennis Batte (Uganda), Israel Mujuni (Tanzania Bara), Issa Kagabo (Rwanda), Thierry Nkurunziza (Burundi), Farah Aden Ali (Djibouti) na Waziri Sheha (Zanzibar).
Waamuzi wasaidizi (assistant referees) ni Elias Kuloba (Kenya), Peter Sabatia (Kenya), Musa Balikoowa (Uganda), Hamis Changwalu (Tanzania Bara), Jesse Erasmo (Tanzania Bara), Simba Honore (Rwanda), Abdulahi Mahamoud (Djibouti) na Josephat Bulali (Zanzibar).
Yanga ndio bingwa wa michuano hiyo, baada ya kuifunga Simba katika fainali 1-0, mwaka jana,

COPA COCA COLA YAFIKIA PATAMU


WAKATI hatua ya 16 bora ya michuano ya Copa Coca-Cola 2012 inaanza Jumamosi (Julai 7 mwaka huu), timu 14 zitakazocheza hatua hiyo zimeshajulikana baada ya mechi zilizochezwa leo (Julai 5 mwaka huu) katika viwanja vinne tofauti.
Tanga iliyoigaragaza Kaskazini Pemba mabao 4-0 katika mechi iliyochezwa Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume, Dar es Salaam imechukua moja kati ya nafasi nne kutoka kundi B. Mabao ya Tanga yalifungwa na Mbwana Musa dakika ya 30, 55 (penalti) na 58 wakati lingine lilifungwa dakika ya 53 na Issa Mwanga.
Kwa ushindi huo, Tanga iliyofikisha pointi tisa inaungana na Mjini Magharibi yenye pointi 13, Morogoro pointi 12 na Mwanza pointi 11 kutoka kundi hilo kucheza hatua ya 16 bora.
Mara iliyoichapa Mtwara mabao 4-1 kwenye Uwanja wa Tanganyika Packers ulioko Kawe, Dar es Salaam na kufikisha pointi tisa nayo imepata tiketi ya 16 bora kutoka kundi C ikiungana na Dodoma yenye pointi 12, Kinondoni pointi 11 na Temeke pointi tisa.
Mabao ya Mara ambayo hadi kipindi cha kwanza kinamalizika ilikuwa mbele kwa 3-0 yalifungwa na George William dakika ya pili, Edson Mwara dakika ya 17 na 45, na Hassan Ally dakika ya 88. Mtwara walipangusa machozi dakika ya 36 kwa bao la Ramadhan Njunja.
Ndoto za Ilala kucheza 16 bora zimeyeyuka baada ya kulala mabao 2-1 mbele ya vinara wa kundi A Ruvuma kwenye Uwanja wa Tamco mkoani Pwani. Mbali ya Ruvuma iliyofikisha pointi 16, timu nyingine zilizopata tiketi ya 16 bora kutoka kundi hilo ni mabingwa watetezi Kigoma wenye pointi 12, Rukwa pointi kumi na Arusha pointi nane.
Mchuano wa kupata timu mbili za mwisho kucheza 16 bora uko katika kundi D ambalo linasubiri matokeo ya mechi ya leo jioni kati ya Kusini Unguja na Tabora itakayochezwa Uwanja wa Nyumbu mkoani Pwani.
Kagera ambayo leo imeifunga Shinyanga mabao 2-0 kwenye Uwanja wa Nyumbu ni moja kati ya mbili ambazo zimeingia 16 bora kutoka kundi hilo. Nyingine ni Kilimanjaro iliyoongoza kwa kufikisha pointi 18 ikifuatiwa na Kagera yenye pointi tisa.
Nafasi mbili zilizobaki zinawaniwa na Pwani yenye pointi saba, Singida (7), Tabora (6) na Kusini Unguja yenye pointi nne.

No comments: