Friday, July 10, 2015

Watanzania watakiwa kula korosho kwa wingi.




 
Mkurugenzi wa Bodi ya Korosho Tanzania, Mfaume Nkanachapa Juma, akihutubia katika siku ya maadhimisho ya kuhamasisha ulaji korosho Tanzania yaliyofanyika katika ukumbi wa Mfaume Kawawa ndani ya viwanja vya sabasaba jijini Dar es Salaam.

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo Chakula na Ushirika, Dkt. Yamungu Kayandabila, akigawa korosho kwa watoto na wananchi waliojitokeza katika maadhimisho ya siku ya kuhamasisha kula korosho. Wakwanza kulia ni Kaimu mwenyekiti wa Bodi ya Korosho, Mudhihiri Mudhihiri.


Na Juma Mohamed, Dar es Salaam.

WANANCHI na wakulima wa zao la korosho wametakiwa kula kwa wingi zao hilo ili kuimarisha afya zao na kukuza soko la ndani litakalopelekea kukua kwa uchumi wa taifa.
Hayo yamezungumzwa na Mkurugenzi wa Bodi ya Korosho Tanzania, Mfaume Juma, alipozungumza na NEWS ROOM muda mfupi baada ya kumalizika kwa sherehe ya kuadhimisha siku ya kuhamasisha kula korosho Tanzania, iliyofanyika katika ukumbi wa Mfaume Kawawa katika viwanja vya Mwl. J.K. Nyerere (Sabasaba) jijini Dar es Salaamm.
Alisema zao hilo linafaida nyingi kwa binadamu ambazo sio za kubuni na kwamba hata nchi zilizopiga hatua katika uuzaji wa korosho zilizo banguliwa ambazo ni Vietinam na India, zinatangaza manufaa yake katika soko la kimataifa.
 Alizitaja baadhi ya faida ambazo mtu anaweza kuzipata baada ya kula korosho kuwa ni kuongeza viini lishe mwilini ambavyo ni muhimu zaidi kwa watoto wadogo wanaoanza kula, akina mama wanaonyonyesha na hata kwa wagonjwa, kuwawezesha kupata nguvu na maendeleo ya ukuaji wa mwili.
“Korosho vilevile zina viini vingine vingi tu vya kuongeza madini na joto katika mwili, kwa mfano korosho zina ‘protine’ nyingi sana na ni mara mbili zaidi ya mtu anaekula samaki au nyama wakati zenyewe sio nyama wala sio samaki..ndio maana katika nchi kama India, kwa kufahamu umuhimu huo wengi wao hawali nyama kabisa na badala yake wanakula korosho kwa lengo la kupata kile ambacho kinapatikana katika nyama..” alisema Mfaume.
Akizungumzia kuhusu kufanya maadhimisho hayo katika viwanja vya sabasaba, alisema dhamira yao sio kuiadhimisha tu katika sherehe za sabasaba bali wanafanya hivyo kwasababu ni maonyesho makubwa ya kibiashara, na kwamba wanahamasisha ulaji wa korosho hata katika maonyesho ya wakulima (siku ya nae nane) ambayo yatafanyika mkoani Lindi, lengo likiwa ni kuendana na matukio makubwa ya kitaifa ya kibiashara.
“Mwaka huu tumedhamiria kupeleka ujumbe huu kwenye Nane Nane katika mikoa mingine ambayo hailimi korosho, kwa mfano Mwanza, Arusha au Mbeya..kwahiyo dhamira hii ni endelevu na inaendana na matukio kwasababu lengo sio kufanya katika ngazi ya mkoa, tunaangalia matukio yanayokusanya jamii kubwa zaidi ili ujumbe ufike kwa pamoja..” aliongeza.
Kwa upande wake, katibu mtendaji wa Mfuko wa Kuendeleza Zao la Korosho (WAKFU) Suleiman Lenga, alisema wamejipanga vizuri kuhakikisha wanaboresha ubanguaji wa zao hilo ambapo kwa sasa wameshapata maeneo matatu kwa ajili ya ujenzi wa viwanda vitatu vya ubanguaji.
“Tunao utaratibu wa ujenzi wa viwanda vitatu vya ubanguaji wa korosho, tunavijenga maeneo ya Mangamba Mtwara, ambako tumepata hekari 20 lakini vilevile Mkuranga na hatimae Tunduru, tutajenga viwanda vyenye uwezo wa kubangua tani 30, 000 kwa maana ya tani 10, 000 kwa kila kiwanda.” Alisema.
Naye mjaasiliamali anaejihusisha na uuzaji wa zao hilo kutoka wilayani Masasi mkoani Mtwara, Bernadeta Ndemanga, alisema wananchi wanahamasika kwa kiasi kikubwa kula korosho lakini hakusita kueleza changamoto zinazowakumba kuwa ni malighafi kuwa ghali zaidi na kupelekea wao kuuza ghali zao hilo.
Alisema changamoto nyingine wanayokumbana nayo ni uhaba wa vifungashio, ambapo wanalazimika kutumia vinavyotoka nchini China jambo ambalo linakua kikwazo kwa wajasiliamali wadogo na hata wale waliopo wilayani kufikiwa kwa wakati na kujikuta wanatumia gharama kuvifuatilia jijini Dar es Salaam.

…………………………..mwisho………………………………………………..

No comments: