Wednesday, January 6, 2016

Waliovamia maeneo manispaa ya Mtwara watakiwa kuanza kubomoa.

Kaimu mkurugenzi wa Manispaa ya Mtwara Mikindani, Donald Sokko.


Na Juma Mohamed, Mtwara.

WANANCHI waliovamia na kujenga katika maeneo ya wazi katika manispaa ya Mtwara Mikindani wametakiwa kubomoa majengo yao wenyewe ili waweze kuokoa sehemu ya vifaa ambavyo vitawasaidia katika matumizi mengine kuliko kusubiri manispaa ianze kutekeleza zoezi hilo.
Akizungumza na waandishi wa habari juzi ofisini kwake, kaimu mkurugenzi wa manispaa hiyo, Donald Sokko, alisema iwapo wanachi watakaidi kutekeleza agizo hilo na kungoja lifanywe na manispaa, watalazimika kulipia gharama za ubomoaji na kukosa hata baadhi ya vifaa kama mabati na matofali.
“Naomba tu nitoe rai kwa wananchi wote ambao wamevamia maeneo ya wazi, kwamba ni vizuri wakabomoa wenyewe ili waweze kuokoa sehemu ya vifaa ambavyo walivitumia katika ujenzi, kwasababu wakibomoa wenyewe itakuwa ni rahisi kuweza kupata matofali, mabati kuliko manispaa itakapoingia gharama ya kubomoa, na zile gharama kila mwananchi atazigharamia kwa fedha yake mwenyewe..” alisema.
Alisema, tayari manispaa imeshawatambua wananchi ambao wamevamia maeneo hayo kutokana na tathmini ambayo ilishafanyika na kuweza kuyabaini maeneo yote yaliyojengwa kwa makosa, ambapo wahusika tayari wameshaandikiwa barua za ilani za kuwataka kubomoa majengo yao.
Alisema, ilani ambazo zimesambazwa kwa wavamizi hao ni zaidi ya 100 huku zikiwataka wale ambao wana vielelezo vyovyote ambavyo viliwapa nguvu ya kujenga waviwasilishe manispaa kwa ajili ya kuhakiki na kuweza kuwatambua watu ambao walitoa ruhusa ya wao kujenga.
“Na kama kutakuwa na mtumishi yoyote atakuwa amehusika katika kusababisha kwamba wananchi wanajenga katika maeneo yanayomilikiwa na serikali, basi manispaa itachukua hatua kali za kinidhamu katika kuhakikisha kwamba watumishi wa aina hiyo hawafanyi kazi katika manispaa yetu..na ilani tuliowaandikiwa tuliwapa siku 14, na siku hizo bado hazijaisha kwahiyo baada ya kukamilika ndipo hatua zitaanza kuchukuliwa.” Alisema na kuongeza:
“Baadhi ya maeneo ambayo wananchi wamevamia ni Shangani, maeneo ya Chuno na kiujumla maeneo ni mengi na tayari tumeshasambaza ilani ili wananchi waweze kubomoa wenyewe kwa hiyari yao..” aliongeza.
Baadhi ya wananchi wanaoishi katika maeneo hayo walisema wanasubiri tu utekelezaji wa zoezi hilo kwani hawana la kufanya kutokana na kukiri kuwa walijenga kimakosa.
“Kibali mwanzoni tulipata tu kwa ajili ya bustani baadae tukaona kwasababu maji yamepungua mzee akaona bora ajenge banda la kuku, kuhusu mabati tutaangalia kwa mchana wa leo (juzi) pengine tunaweza kutoa..” alisema, Akwinata Haule, mkazi wa mtaa wa Majengo kata ya Chuno.



No comments: