Saturday, December 19, 2015

CWT Mtwara yawajengea uwezo Walimu.


Na Juma Mohamed, Mtwara.

CHAMA cha Walimu Tanzania (CWT) mkoani hapa kimeendesha mafunzo ya siku tatu kwa viongozi wa chama hicho kutoka katika ngazi ya mkoa, wilaya na vitengo vya wanawake, kwa lengo la kuwajengea uwezo juu ya masuala mbalimbali yakiuongozi.
Mafunzo hayo yaliyoratibiwa na baraza kuu la CWT Taifa na kuhusisha viongozi kutoka katika wilaya zote za mkoa wa Mtwara, ndio yakwanza tangu kufanyika kwa uchaguzi mkuu wa chama hicho mwezi Mei mwaka huu.
Wakizungumza baada ya kufungwa kwa mafunzo hayo, baadhi ya walimu wamesema awali walikuwa wakikabiliwa na changamoto nyingi za kiuongozi zaidi ikiwa ni juu ya matumizi ya fedha za chama ambazo walishindwa kupanga mlolongo mzuri.
Mariam Makubomula, kutoka halmashauri ya Mtwara vijijini, alisema alikuwa katika wakati mgumu kuweza kujibu maswali ya wanachama ambao wengi wao walikuwa wakihoji kuhusu asilimia zinazokatwa kutoka katika fedha za wanachama, ambapo baada ya kupata mafunzo hayo atakua na majibu.
Mwenyekiti wa Kitengo cha Walimu Wanawake (KE) Manispaa ya Mtwara Mikindani, Graceana Nyoni, alisema miongoni mwa changamoto zinazowakabili walimu wanawake ni kipato duni ambacho hakikidhi mahitaji yao kwa kila mwezi jambo linalopelekea kuwa na maendeleo hafifu.
“Walimu mishahara yao ni midogo, ukilingalisha na maisha ya hapa Mtwara mjini haviendani kabisa..maisha hapa yapo juu sana, sasa mwalimu akisema aangaike na mshahara tu ule hauwezi kutosha, anakuwa na majukumu mengi mwalimu utakuta anakuwa na mikopo na mambo mengine mengi, lakini kwa msaada wa mafunzo haya hapa tukienda kuwaelimisha wanachama wetu au walimu wanawake, tunaweza tukatengeneza miradi mingi..” alisema.
Naye, Mgreth Kalage, mwakilishi kutoka kitengo KE Manispaa ya Mtwara, alisema walimu wanawake wengi wanapata changamoto ya walezi wa watoto wao inapotokea wamejifungua, na kutakiwa kurudi kazini baada ya miezi mitatu kiasi cha kulazimika kuwaacha watoto wao ambao ni wachanga wakilelewa na wasaidizi wa kazi.
Alisema, itakuwa ni fursa kwa walimu hao iwapo wataamua kuanzisha kituo cha kulelea watoto ambacho waaajiri wasichana maalum kwa ajili ya kazi hiyo ambao watakuwa wapatiwa mafunzo ya shughuli hiyo.
Katibu wa chama hicho, Fratten Kwahison, alisema kupitia mafunzo haoyo, walimu wameweza kupata ufumbuzi wa mambo mbalimbali ambayo yalikuwa ni kikwazo kwao katika utendaji wa kazi zao pamoja na mifumo dume ambayo ilikuwa ni changamoto kwa walimu wakike.
“Sisi kina baba siku zote hatuwapi nafasi kina mama, utakuta anakua kiongozi lakini inapofikia katika masuala ya maamuzi hatuwashirikishi vyakutosha..sasa kwenye semina hii wameelimishwa na wamejua ni namna gani na wao wanaweza wakafanya yale majukumu ambayo wanaume wanafanya..” alisema.




No comments: