Friday, October 23, 2015

Uchaguzi- Wananchi Mtwara wazidi kukimbia mji, Ujumbe wa vitisho waanza kusambaa.

Baadhi ya wananchi wa manispaa ya Mtwara Mikindani wakiwa kituo kikuu cha mabasi Mtwara kwa ajili ya kusafiri kwenda maeneo mbalimbali ya nje ya mji kwa kuhofia usalama wao katika kipindi cha uchaguzi




Kipeperushi kikionyesha ujumbe wa uchochezi kwa wananchi wa manispaa ya Mtwara Mikindani, kiasi cha kuwafanya baadhi yao kushikwa na hofu wakati wa uchaguzi


Kamanda wa Poli Mkoa wa Mtwara ASP-Henry Mwaibambe, akizungumza na waandishi wa habari na viongozi wa vyama vya siasa wa mkoa wa Mtwara jana, kuhusu hali ya usalama ilivyo na kupokea maoni mbalimbali kutoka kwao.

 Na Juma Mohamed.

IKIWA imebaki siku moja ili ufanyike uchaguzi, hofu ya usalama kwa wananchi wa manispaa ya Mtwara Mikindani imezidi kutanda kiasi cha kusababisha wengi wao kuzidi kuhama mjini na kuelekea maeneo yao ya asili hasa vijijini.
Hali hiyo ilianza kujitokeza siku nne zilizopita kwa baadhi ya wakazi wa manispaa hiyo wengi wao wakiwa kina mama na watoto, huku ikitajwa kuwa ni hofu ya usalama wao kutokana na kuhofia kuzuka kwa vurugu siku ya uchaguzi, Jumapili ya Oktoba 25.
Kwa mujibu wa wananchi hao, hali hiyo imesababishwa na askari polisi na Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) kuzunguka mitaani kwa ajili ya kufanya mazoezi wakiwa na silaha zao.

Baadhi ya wananchi wa manispaa ya Mtwara Mikindani wakiwa kituo kikuu cha mabasi Mtwara kwa ajili ya kusafiri kwenda maeneo mbalimbali ya nje ya mji kwa kuhofia usalama wao katika kipindi cha uchaguzi

Akizungumza katika kikao na waandishi wa habari na viongozi wa vyama vya siasa, Kamanda wa Pilisi Mkoa wa Mtwara ASP-Henry Mwaibambe, aliwataka wananchi hao kutokuwa na wasiwasi wowote juu ya askari kuzunguka mitaani, akisema kuwa suala la kufanya mazoezi ni la kawaida.
Akijibu hoja iliyotolewa na Mgombea Udiwani wa Kata ya Dihimba, Mtwara vijijini, Ismail Liuye, ya kuwataka askari kutoa taarifa kwa wananchi wanapotaka kufanya mazoezi au jambo lolote ambalo litawashtua wananchi ili kuhepusha wasiwasi miongoni mwao, alisema jeshi la polisi wana haki ya kufanya hivyo lakini sio kwa JWTZ ambao wanauwezo wa kufanya mazoezi wakati wowote na mahali popote.
“Vyombo vya ulinzi wanapofanya mazoezi sio lazima mshirikishwe..sisi polisi kwasababu tunamtandao mpana tuna mapolisi kata, tuna mapolisi chungu mzima kwahiyo ni rahisi kuwaambia lakini wanajeshi hawana mamlaka hiyo, na sio lazima wewe wakuambie kwamba leo tutakuwa Chikongola, wao taratibu zao haziwaruhusu na wanaouwezo wa kufanya mazoezi mahali popote pale..” alisema.
Alisema, katika usimamizi wa uchaguzi wanaohusika ni askari polisi, mgambo, askari magereza na uhamiaji na kwamba Jeshi halina mamlaka ya kusimamia uchaguzi kwahiyo hayo wanayoyafanya hayahusiani na uchaguzi.
Akizungumzia suala la kuongezwa kwa magari ya Jeshi la Polisi, alisema ni jambo la kawaida na ndio utaratibu ambao unafanyika hata katika chaguzi zilizopita, kwani ilifanyika hivyo pia katika uchaguzi wa mwaka 2010 ambapo yaliletwa magari 700 huku mwaka huu yakiwa 399.
“Kwahiyo ni utaratibu wa kawaida tu kwasababu tunahitaji kila eneo tuwe na gari..kwahiyo naomba wananchi wetu muwaambie wasiogope kama kuna dalili zozote ambazo sio nzuri basi tujulishane, namba za simu mmnazo na kila sehemu kutakuwa na kiongozi lakini sio kwa ajili ya kufanya fujo.” Alisema.
Kufuatia kusambaa kwa vipeperushi vinavyoashiria hali ya uvunjifu wa amani ambavyo vinawashinikiza wananchi kumchagua mgombea Ubunge wa jimbo la Mtwara mjini kupitia Chama cha Wananchi (CUF), Mftaha Nachuma, alisema tayari jeshi la polisi limepata taarifa na wanavyo hivyo vipeperushi ambapo alisema wanaendelea na uchunguzi ili kumtambua anayesamabaza.
Vipeperushi hivyo ambavyo ambavyo vina ujumbe wa uchochezi ambao unasema “Kama amtamchagua Maftaha Nachuma, Nyumba zenu zitachomwa moto Kazi kwenu” zinaonyesha kuzidi kuwafanya watu waingiwe na hofu iwapo matokeo yatatangazwa tofauti na matarajio yao.
“Alisema sisi polisi tumepata pakuanzia kwa mara ya kwanza hiyo hiyo baada ya kupata taarifa, na tunafahamu aliyetupigia simu kwa mara ya kwanza na tukasema kwanini ametupigia simu yeye kwa mara ya kwanza..na vipeperushi vingi vimesambazwa katika maeneo ya kituo cha polisi lakini tunajiuliza kwanini..” alisema kamanda.
Kwa upande wake, mgombea ubunge wa CUF Maftaha Nachuma, alisema anaamini hivyo vipeperushi wanaosambaza ni wapinzani na sio watu wa Chama hicho, na wanafanya hivyo kwa lengo la kukichafua chama na mgombea ambaye ni yeye kwasababu wanajua ndio chama chenye nguvu katika jimbo hilo kwasasa.
“Kwahiyo mimi naamini hawa ni wapinzani wangu wameamua kunichafua ili lengo lao wanaMtwara ambao wanampenda Maftaha waweze kubadilisha mitazamo.” Alisema.

No comments: