Wednesday, September 9, 2015

Matapeli wa ajira waingia Mtwara..

Kaimu Mkurugenzi wa halmashauri ya Manispaa ya Mtwara Mikindani, Donald Nssoko, akizungumza na waandishi wa habari kuhusu kuwepo kwa vitendo vya utapeli vinavyofanywa na watu wasiojulikana dhidi ya Manispaa hiyo




Na Juma Mohamed.

HALMASHAURI ya Manispaa ya Mtwara Mikindani imewataka wananchi wanaotafuta ajira kuwa makini na vitendo vya kitapeli vinavyofanywa na baadhi ya watu wanaojifanya maafisa utumishi wa halmashauri, wakiwa na lengo la kujipatia fedha kwa njia ya rushwa.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, Donald Nssoko, alisema kumekuwa na utapeli unaofanywa na watu wasiojulikana ambao wanawapigia simu watu ambao waliwahi kufanyiwa usaili katika halmashauri hiyo kwa kuwaambia wanahitajika ofisini kwa ajili ya kupatiwa ajira.
Alisema, jumla ya watu watatu kutoka maeneo tofauti hapa nchini wametapeliwa kiasi tofauti cha fedha, baada ya kupigiwa simu na watu wanaojitambulisha kuwa wao ni maafisa utumishi wa halmashauri hiyo, na kwamba wanahitaji fedha ili waweze kuwapatia ajira walizoomba, kwani hakuna kitu kinachopatikana bure.
“Ni vizuri kuweka taadhari kwa umma ili wananchi wetu wasiweze kupata hasara, na ndio maana leo nimewaita ili tuwa taarifu wananchi kwamba wajihepushe wanapopigiwa simu na watu wasiowafahamu ambao ni matapeli wakiwaeleza kwamba kuna nafasi ambazo ziko wazi hapa manispaa ya Mtwara Mikindani..na sio watu wa mkoa wa Mtwara iwe ni kwa nchi nzima, kwasababu kuna dada mmoja alipigiwa simu akiwa yuko Kigoma..” alisema.
Alisema waliotapeliwa ni Christina Rutayega mkazi wa Kigoma ambaye alitapeliwa kiasi cha sh. 120,000, Glory Valentine mkazi wa Tanga sh. 200,000 na Maimuna Mohamed sh. 250,000.
Aidha, alisema halmashauri hiyo ilipata kibali cha kuajiri watumishi wanane wa vitengo viwili tofauti February 18 mwaka huu chenye kumbukumbu namba CB 170/362/01/C/63, ambapo waliohitajika kuajiriwa ni watunzaji wa kumbukumbu wasaidizi wa daraja la pili (4) na madereva wa daraja la pili (4).
Alisema halmashauri ilifuata taratibu zote za kuendesha usaili na kwamba usaili wa mchujo ulifanyika Mei 19 mwaka huu kwa nafasi zote, baada ya kupitia maombi ya 36 ya waombaji.
“Kwa mantiki hiyo, nafasi zote za waajiriwa kwa maana ya watunza kumbukumbu wasaidizi daraja la pili nafasi nne na madereva wasaidizi daraja la pili nafasi nne..nafasi zote hizo baada ya kukamilisha mchakato wa usaili, watahiniwa wote hao waliajiriwa..” aliongeza.
Kwa upande wake, Glory Valentine, ambaye alitapeliwa kiasi cha sh. 200,000 alisema, alipigiwa simu na mtu ambaye alijitambulisha kama aifisa utumishi na kumuambia kuwa kutokana na kwamba aliomba nafasi ya kuajiriwa katika manispaa ya Mtwara Mikindani, anatakiwa amtumie kiasi hicho cha fedha ili aweze kupata ajira.
Alisema, baada ya kuambiwa atume fedha hiyo, alifanya jitihada za kuipata na kisha kumtumia ambapo aliambiwa atapigiwa simu na watu wa manispaa hiyo siku moja baadae, lakini haikuwa hivyo na kwamba siku iliyofuata alipompigia simu kutaka kumuuliza kwanini hajapigiwa, simu yake haikupokelewa.
“Siku ya nne akanipigia simu na kuniuliza kama nilipigiwa, nikamjibu hapana..akanitafuta tena siku iliyofuata akataka nimuongeze ten ash. 500,00, nikamuambua baba yangu ameniambia mpaka atakapoiona hiyo barua ya kazi atakuongeza hata zaidi ya hiyo..akataka nimpe namba ya baba, nikampa na akawasiliana naye..” alisema.
Na kuongeza “alivyowasiliana naye akamwambia yeye aje tu kesho Mtwara, na barua yake nimemwambia mkurugenzi asiende sehemu yeyote aje kuchukua kwangu alafu aje na hiyo hela..” aliongeza.
Alisema, kabla ya kufunga safari ya Mtwara aliamua kuwasiliana na mtu aliyekuwa mkoani hapa na kumuulizia kuhusu suala la ajira akamjibu kuwa swala hilo halipo, ambapo hakuweza tena kusafiri na kuacha kuwasiliana naye tena kwa kujua tayari ni tapeli.
Naye, Christina Rutayega mkazi wa Kigoma, alisema alipigiwa simu na baba yake akimweleza kuwa amepata kazi mkoani Mtwara na anatakiwa kuripoti kazini ndani ya siku tatu, huku akisema amepewa taarifa hizo kwa njia ya simu na mtu aliejitambulisha kwa jina la Mrisho.
Alisema baada ya kuambiwa hivyo, alilazimika kusafiri siku ya pili yake mpaka Dar es Salaam ambako alilala kabla ya kufika Mtwara siku iliyofuata na kupokelewa na rafiki yake ambaye anafahamiana na afisa utumishi wa Manispaa hiyo.
“Nilivyomwambia akasema ngoja kwanza niwasiliane na afisa utumishi wa pale, baada ya kuwasiliana naye akaambiwa kwamba hakuna kitu kama hicho..tukampigia simu tena yule mtu tukamwambia, na ilikuwa Jumapili, akasema wewe njoo kesho saa nne maana asubuhi nitakuwa kwenye kikao..mimi nikaenda ile Jumatatu saa nne nikampigia simu baada ya kufika, akaniambia ni subiri yupo sokoni.” Alisema
Na kuongeza “nikamwambia sasa mboni unanisumbua hivi kaka, akasema wewe subiri, nikasubiri mpaka saa sita ikabidi niondoke nikarudi nyumbani..” aliongeza.
Alisema, ilikuwa rahisi kumuamini mtu huyo kwasababu aliyepigiwa simu ni mzazi wake na kwamba namba ya simu aliyoitumia ilikuwa katika wasifu wake (CV) kwahiyo sio kitu rahisi kwa mtu kuweza kuipata.
Wakati huo huo kamanda wa Polisi mkoani hapa, Henry Mwaibambe, alisema matukio ya utapeli ya aina hiyo yamekuwa mengi na kuwataka wananchi kutokubali wanapopigiwa simu wakitakiwa kutoa pesa kwa ajili ya kutafutiwa kazi viandani au mahali sehemu zingine.
Alisema, alipgiwa simu na mtu kutoka wilayani Mkuranga akimweleza kuwa alipigiwa simu na mtu ambaye yuko mkoani hapa na kumwambia kuwa amtumie fedha sh. 500,000 ili apate kazi katika kiwanda cha Saruji cha Dangote, na kwamba tayari ameshamtumia sh. 200,000.



No comments: