Tuesday, September 11, 2012

TWITE, YONDAN WAIDHINISHWA YANGA




KAMATI ya Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), chini ya Mwenyekiti wake, Alex Mgongolwa, imewaidhinisha Mbuyu Twite na Kevin Yondan kuchezea Yanga katika msimu ujao wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, unaoanza mwishoni mwa wiki.
Habari kutoka ndani ya kikao cha Kamati hiyo, kilichomalizika hivi karibuni, zimesema kwamba pamoja na maamuzi hayo, Yanga imepewa siku 21 kulipa dola 32,000 ambazo Simba SC ilimlipa Twite ili ajiunge nao, lakini baadaye akaghairi na kusaini na kuhamia Yanga.
Uamuzi huu, unafuatia kikao cha pamoja baina ya Simba na Yanga Jumatatu iliyopita kuvunjika bila kufikia makubaliano kuhusu mustakabali wa wachezaji hao.
Katika kikao hicho kilichoanza majira ya saa 7:00 mchana, hoja ya kwanza kuwasilishwa mezani ilikuwa ni suala la beki Twite na upande wa Yanga uliwakilishwa na Sanga na Katibu, Celestine Mwesigwa wakati kwa Simba walikuwepo Makamu Mwenyekiti, Geoffrey Nyange ‘Kaburu’ na Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili, Kapteni wa zamani wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), Zacharia Hans Poppe.
Ikumbukwe, Simba iliwasilisha malalamiko ya kufanyiwa mchezo usio wa kiungwana na Yanga kwa Twite. Ilidai Twite alisaini mkataba na klabu yao Agosti 1, mwaka huu mbele yao, viongozi wa Shirikisho la Soka Rwanda (FERWAFA) na APR na kulipwa dola za Kimarekani 30,000 na nyingine 2,000 za nauli ya kuja Dar es Salaam kujiunga na klabu hiyo. Hata hivyo, mchezaji huyo akahamia Yanga.
Katika mjadala huo, Simba ilikubali kurudishiwa fedha zao, lakini viongozi wa Yanga wakasema hawawezi kutoa hadi waombwe radhi na Mwenyekiti wa Simba, Alhaj Ismail Aden Rage, ambaye alisema viongozi wa klabu hiyo yenye maskani yake makutano ya mitaa ya Twiga na Jangwani wana ‘fedha chafu za EPA’.
Simba wakasema kauli yake ya Rage ilikuwa sehemu ya utani wa jadi, kama ambavyo Yanga walimvalisha jezi Twite yenye jina la Rage.
Kufikia hapo, Simba wakasema hawawezi hata kujadili suala la Kevin Yondan na Kamati ya Mgongolwa ikasema itapitia maelezo ya pande zote, watatoa majibu kwa mujibu wa kanuni na sheria Septemba 10, mwaka huu, yaani leo.
Katika kesi ya Yondan, walalamikaji ni Simba, ambao wanadai beki huyo alisaini Yanga akiwa bado ana mkataba na klabu yao.
Awali, Kamati ya Mgongolwa ilikutana Jumapili iliyopita asubuhi hadi usiku, bila kupata suluhisho la pingamizi hizo na kuamua kutumia busara ya kuzikutanisha pande zinazopingana kujaribu kupata suluhu siku iliyofuata

SOURCE:BIN ZUBEIRY

No comments: