Monday, June 6, 2016

Wananchi Mwena kunufaika na kiwanda cha chupa za maji.




Mwenge wa Uhuru ukiwasili katika kiwanda cha kutengeneza chupa za maji ya Ndanda Springs, kilichopo katika kata ya Mwena, wilayani Masasi, kwa ajili ya kuweka jiwe la msingi



Burudani ya asili


Vijana wakiwa nje ya kiwanda cha kutengeneza chupa za maji ya kunywa ya Ndanda Springs, wakisubiri msafara wa mbio za Mwenge wa Uhuru kwa ajili ya kuweka jiwe la msingi kiwanda hicho.




Na Juma Mohamed, Masasi.

WANANCHI wa kata ya Mwena wilayani Masasi wameonesha kuwa na matumaini makubwa ya kujipatia ajira kufuatia ujenzi wa kiwanda cha kutengeneza chupa za maji safi na salama ya Ndanda Springs kinachojengwa katani hapo ambacho kimewekwa jiwe la msingi na mbio za Mwenge wa Uhuru.
Wakizungumza na Nipashe, walisema kwa sasa vijana wengi wanakabiliwa na changamoto za ukosefu wa ajira kiasi cha kupelekea kuona maisha magumu lakini uwapo wa kiwanda hicho utawakomboa kuondokana na hali hiyo .
“Ninafurahi kuanzishwa kwa kiwanda hiki maana kitasaidia kupatikana kwa ajira, vijana wengi tunakaa hatuna kazi, kwahiyo baada ya kufunguliwa hapa nafikiri ajira zitakuwa nyingi baadhi ya ukali wa maisha utapungua..pia tunatarajia maji yatapatikana kwa wingi na hata bei itakuwa nafuu kwakua yatakuwa yanazalishwa kwa wingi na chupa zinapatikana karibu hapahapa..” alisema Marun Majogo.

Moja ya vikundi vya ngoma za asili kinachozunguka na mbio za Mwenge wa Uhuru mkoani Mtwara kikitumbuiza wakati wa uwekaji jiwe la msingi katika kiwanda cha kutengeneza chupa za maji ya Ndanda Springs, Mwena, wilayani Masasi

Naye, Costantino Daudi ambaye ni wakala wa kuuza maji ya Ndanda Springs, alisema kukamilika kwa kiwanda hicho kutawasaidia kuweza kununua maji kwa bei nafuu jambo litakalowafanya na wao waweze kuuza kwa nafuu kwa wateja wao.
Akisoma taarifa ya kiwanda hicho kwa kiongozi wa mbio za mwenge Kitaifa, George Mbijima, mmoja wa wafanyakazi wa kiwanda hicho kutoka kitengo cha uzalishaji, Romanus Mpanda, alisema sambamba na ujenzi huo, kipo kiwanda kingine cha kuzalisha maji safi na salama ya kunywa cha Ndanda Springs.
“Kiwanda hiki cha kuzalisha maji safi ya kunywa kina wafanyakazi 100 wazalendo ambao wengi wao ni vijana wakiume na wakike ambao wametoka katika jamii inayozunguka kiwanda hiki..katika wafanyakazi hao 100, wafanyakazi wakike wapo 61 na wakiume 39..” alisema Mpanda.

Vijana wakiwa nje ya kiwanda cha kutengeneza chupa za maji ya kunywa ya Ndanda Springs, wakisubiri msafara wa mbio za Mwenge wa Uhuru kwa ajili ya kuweka jiwe la msingi kiwanda hicho.

Meneja uzalishaji wa kiwanda cha Ndanda Springs, Benedict Macheso, alikiri kuwapo kwa fursa za ajira katika kiwanda hicho cha chupa ambacho ujenzi wake mpaka ulipofikia umegharimu sh. Bilioi 1.08 na kutarajiwa kumalizika katikati ya mwezi Septemba mwaka huu
Kwa upande wake, kiongozi wa mbio za Mwenge Kitaifa George Mbijima, aliwataka vijana watakaopata nafasi za kuajiriwa kiwandani hapo kufanya kazi kwa juhudi na kuwa waaminifu ili kampuni ipate mafanikio ambayo yatasababisha fursa ya kuongeza viwanda vingine.
“Tufanye kazi kwa bidii ili apate faida, tusipowajibika yeye ana uhuru na wala hafungwi kutafuta wafanyakazi kutoka sehemu nyingine yoyote ya nchi ambao watakuwa tayari kufanya kazi, sasa vijana wenzangu wa hapa tusikubali tukapoteza nafasi hii..tunapopata nafasi tufanye kazi kwa manufaa binafsi lakini tumsaidie ndugu yetu ili aweze kufungua viwabda vingi zaidi..” alisema Mbijima.

No comments: