Thursday, June 9, 2016

Mkuchika ashinda kesi ya kupinga matokeo ya uchaguzi wa Ubunge Newala.




Mbunge wa Newala mjini (CCM) George Mkuchika akiongea na waandishi wa habari (hawapo pichani) baada ya kumalizika kwa hukumu ya kesi ya kupinga matokeo ya uchaguzi wa Ubunge wa jimbo hilo iliyofunguliwa na aliyekuwa mgombea wa Chama cha Wananchi (CUF) Juma Manguya dhidi yake. Mkuchika alishinda katika kesi hiyo baada ya Jaji wa mahakama kuu ya Tanga, Amour Khamis kutupilia mbali kesi hiyo.


Na Juma Mohamed, Mtwara.
MAHAKAMA kuu kanda ya Mtwara imetupilia mbali kesi ya kupinga matokeo ya ubunge wa jimbo la Newala mjini katika uchaguzi mkuu uliofanyika mwezi Oktoba mwaka jana, iliyofunguliwa na aliyekuwa mgombea ubunge kupitia Chama cha Wananchi (CUF) Juma Manguya dhidi ya mbunge wa jimbo hilo kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Mhe. George Mkuchika.
Akisoma hukumu ya kesi hiyo iliyosikilizwa katika mahakama ya wilaya ya Newala, Jaji wa mahakama kuu ya Tanga, Amour Khamis, alisema maamuzi hayo yametokana na mlalamikaji kushindwa kuthibitisha katika kesi yake kwa kiwango stahiki kwamba uchaguzi huo haukuendeshwa kwamujibu wa sheria, huku walalamikiwa wakitoa ushahidi wa kutosha.
Kesi hiyo namba 1 ya uchaguzi mwaka 2015 ambayo hukumu yake ilianza kwa kusomwa madai yote 13 ambayo yaliwasilishwa na mlalamikaji kabla ya kutolewa maamuzi, ilikuwa katika hali ya ulinzi mkali wa jeshi la polisi huku ikishuhudiwa askari wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) wakizunguka barabarani na gari lao.
Akizungumza baada ya kutolewa hukumu hiyo, Manguya ambaye madai yake yote 13 aliyowasilisha mahakamani hapo yamekataliwa, alisema hakubaliani na maamuzi hayo na kwamba atakaa na jopo lake ili waweze kukata rufaa. 

Mlalamikaji katika kesi ya kupinga matokeo ya uchaguzi wa Ubunge jimbo la Newala mjini, Juma Manguya, ambaye alikuwa mgombea ubunge wa Chama cha Wananchi (CUF) katika uchaguzi mkuu wa mwezi Oktoba mwaka 2015



“Tutakaa na wakili wangu kuangalia zile hoja tatu, ipo hoja ambayo sisi tuna pakupitia ambayo tutakwenda tukae na mawakili tuweze kwenda mbele zaidi..na nachukua nafasi hii kama nilivyotangulia mwanzo kutoka mahakamani kuwataka wale wafuasi wetu wa UKAWA (Umoja wa Katiba ya Wananchi) na Chama cha Wananchi CUF wawe watulivu hapa sio mwisho tutaendelea mbele mpaka pale haki itakapopatikana..” alisema Manguya.
Wakili wa Manguya aliyekuwa akimsimamia katika kesi hiyo, Rainery Songea, ameahidi kwenda kudai nakala ya hukumu ili aipitie vizuri kabla ya taratibu za kukata rufaa.
“Nimemsikiliza Jaji kwa makini na nimeona maamuzi yake yalivyo, kimsingi mimi kama wakili kitu ambacho nataka nikifanye kwanza nataka niombe ‘copy’ (Nakala) ya hiyo hukumu noisome kwa makini lakini pia kwa jinsi nilivyomsikiliza naona kuna kuna vitu Fulani ambavyo vina haja ya kuvikatia rufaa..” alisema.
Kwa upande wake, mshindi katika kesi hiyo, George Mkuchika, aliishukuru mahakama kwa maamuzi hayo na kuahidi kuendelea kuwatumikia wananchi wa jimbo lake bila ubaguzi.

Baadhi ya wananchi wa wilaya ya Newala wakiwa katika viwanja vya mahakama ya wilaya ya Newala wakisikiliza hukumu ya kesi ya kupinga matokeo ya uchaguzi wa Ubunge jimbo la Newala iliyofunguliwa na aliyekuwa mgombea wa Chama cha Wananchi (CUF) Juma Manguya dhidi ya Mbunge wa jimbo hilo kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) George Mkuchika.



“Mimi nataka kusema tu kwamba nashukuru maamuzi ya mahakama nimeyapokea kazi iliyobaki kwangu sasa hivi ni kuwatumikia wananchi wa Newala wote bila kubagua walionipigia kura na ambao hawakunipigia kura..” alisema.
Naye wakili wake Hussein Mtembwa ambaye ni wakili wa kujitegemea aliwataka wafuasi wa Mkuchika kusherehekea ushindi kwa amani na utulivu huku akiwashukuru wadau waliohusika katika kufanikisha ushindi huo pamoja na mahakama kwa kutenda haki.




“Nichukue nafasi hii kuwashukuru wadau wote ambao wamehusika muda wote wa kesi ikiwa ni pamoja na mahakama kwa lile suala moja tu la kutoa haki..sasa kwaniaba ya Mbunge nitoe rai tu kwa wale wafuasi wa Mhe. Mkuchika washerehekee ushindi huu kwa amani na utulivu kabisa..” alisema.
Mahakama hiyo ilimtaka mlalamikaji Juma Manguya, kumlipa mlalamikiwa George Mkuchika gharama zote alizotumia wakati wa uendeshwaji wa kesi hiyo ambapo hata hivyo imempa nafasi ya kuendelea kukata rufaa iwapo hatoridhika na maamuzi.
………………………………………..mwisho……………………………………….

No comments: