Tuesday, February 2, 2016

Zaidi ya kaya 500 manispaa ya Mtwara mikindani zakumbwa na mafuriko.


Mkazi wa mtaa wa Kiyangu kata ya Shangani manispaa ya Mtwara Mikindani akivuka maji ambayo yamejaa katika nyumba mbalimbali kufuatia mvua kubwa iliyoambatana na upepo mkali iliyonyesha kuanzia usiku wa juzi kuamkia jana na kusababisha mafuriko


Baadhi ya wakazi wa mtaa wa Kiyangu, kata ya Shangani manispaa ya Mtwara Mikindani wakihamisha vyombo na mali zao kufuatia nyumba zao kujaa maji kutokana na mvua kubwa iliyoambatana na upepo mkali iliyonyesha kuanzia usiku wa juzi kuamkia jana na kusababisha mafuriko






Na Juma Mohamed, Mtwara.

ZAIDI ya kaya 500 katika manispaa ya Mtwara Mikindani zimeathirikia na mafuriko yaliyotokana na mvua kubwa iliyonyesha kuanzia usiku wa juzi kuamkia jana, na kupelekea wananchi wengi wa kaya hizo kupoteza mali zao na vyakula kutokana na kuingiliwa na maji katika nyumba zao.
Akitoa tathmini ya mafuriko hayo, mkuu wa wilaya ya Mtwara, Fatma Ally, alisema amejitahidi kuzungikia maeneo mbalimbali katika kata zote 18 za manispaa hiyo akiambatana na kamati ya maafa na kubaini kuwa hakuna maafa yeyote kwa binadamu wala nyumba ambayo imebomolewa na mvua hiyo zaidi ya upotevu wa mali na vyakula.
“Hali tuliyoikuta ni kwamba kaya zilizoathirika ni nyingi ingawa bado tunataka tupate taarifa kamili kutoka kwa watendaji wa kata na wanaendelea kutuletea taarifa zao za mukhtasar wa vikao vya kamati za maafa ambazo wameshakaa huko kwenye kata na tumeshaanza kuzipokea..lakini mpaka sasa hivi inaonyesha ni zaidi ya nyumba 500 zimeweza kuingiliwa na maji ndani.” Alisema.

Baadhi ya wakazi wa mtaa wa Kiyangu, kata ya Shangani manispaa ya Mtwara Mikindani wakihamisha vyombo na mali zao kufuatia nyumba zao kujaa maji kutokana na mvua kubwa iliyoambatana na upepo mkali iliyonyesha kuanzia usiku wa juzi kuamkia jana na kusababisha mafuriko


Alisema, pamoja na kuziagiza kamati za maafa za kata kuwasilisha taarifa zao, kupitia kamati yake ya maafa ya wilaya wameziagiza kamati hizo kuandaa makazi ambayo yatasaidia kwa wale ambao kaya zao zimeathirika zaidi ili waweze kwenda kujihifadhi huko.
Alisema bado wilaya inafanya jitihada za kuandaa makazi kwa ajili ya wananchi watakaokosa hifadhi katika kata zao ambapo wametenga eneo katika Chuo cha Walimu Mtwara (TTC) ambalo linauwezo wa kuhifadhi zaidi ya kaya 30 huku jitihada za kupata maeneo mengine zikiendelea kufanyika.
“Kwahiyo tumeagiza kwenye kata zote kama wananchi watakosa kabisa sehemu za kusitiriwa basi wawalete kwetu tutawasitiri lakini bado tunaendelea kutafuta sehemu nyingine kama pale pataja basi tuwapeleke sehemu nyingine na tutaweza kuwagharamia chakula kwa hizi siku chache zitakazokuwa kama changamoto kwao.” Alisema.

Alisema, kamati ya maafa imetoa agizo kwa mkurugenzi wa halmashauri kwa kushirikiana na mstahiki Meya na kamati ya fedha kuhakikisha fedha zinapatikana kwa ajili ya kukarabati miundombinu ambayo imeathiriwa na mvua.
Aidha, alisema licha ya mfereji mkubwa uliochimbwa kuanzia Kiyangu kwa lengo la kupeleka maji baharini kuonekana kuzidiwa na maji kiasi cha kuonekana bado yanafurika katika nyumba zilizopo maeneo hayo, bado umejitahidi kusaidia kupeleka maji baharini ukilinganisha na ilivyokuwa siku za nyuma.

Hata hivyo, baadhi ya wakazi wanaoishi maeneo yaliyo karibu na mfereji huo walionekana kutoridhishwa na ubora wake na kudai kuwa umezidiwa na maji kiasi cha kuonekana kama bado hauna msaada kwasababu maji bado yamefurika kwenye nyumba za watu.

No comments: