MIFUKO ya
Hifadhi ya Jamii nchini pamoja na waajiri wametakiwa kutunza vizuri kumbukumbu
za wanachama wao ili kuhepusha usumbufu pindi mwanachama anapohitaji mafao yake
baada ya kustaafu.
Akizungumza
jana mkoani hapa katika ufunguzi wa semina ya siku moja ya kuwajengea uwezo maafisa
kutoka katika kampuni na taasisi mbalimbali mkoani hapa juu ya huduma
zitolewazo na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii wa PPF, mkuu wa wilaya ya Mtwara, Fatma
Ally, alisema katika suala la utunzaji wa kumbukumbu ni muhimu pia
kuwashirikisha wanachama ili wafahamu taarifa za mafao yao.
Mkuu wa wilaya ya Mtwara, Fatma Ally. |
“Na hili
lifanyike kwa kushirikiana kati ya mfuko wa hifadhi pamoja na mwajiri mwenyewe
lakini mwanachama naye ni vyema ikawa sio siri na ajulishwe ni vitu gani
ambavyo tunaviita ni kumbukumbu ili na yeye mwenyewe pia ashiriki kuhakikisha
kumbukumbu zake zimekamilika na muda wa kustaafu ukifika asichelewe kupata
mafao yake..” alisema.
Alisema,
mifuko hiyo inatakiwa kupunguza manung’uniko kutoka kwa wanachama wanapostaafu
anayotokana na ucheleweshwaji wa mafao na kupelekea usumbufu wa kufatilia mara
kwa mara.
Mkuu wa wilaya ya Mtwara, Fatma Ally, akipeana mkono na meneja masoko wa PPF, Abuu Kibiki. |
Aidha, mkuu
wa wilaya aliwataka wananchi na wajasiliamali wadogo kuchangamkia kwa kujiunga
na PPF kupitia mpango wao mpya wa Wote Scheme ambao unazihusisha sekta zisizo
rasmi pamoja na mfumo wa ziada uliopo kwenye sekta rasmi.
Alisema,
mfumo huo unatoa fursa kwa watu au kikundi cha watu chenye mlengo wa kiuchumi
kilichopo kwenye sekta isiyo rasmi kuweza kujiunga ikiwa ni pamoja na mama
lishe, wakulima, wafugaji, wavuvi, waendesha pikipiki, wajasiliamali wadogo,
wasanii na wanamichezo.
“Tukiangalia
pale kiwango cha chini kwa mwezi ni sh. 20,000 ambapo katika wilaya yetu
tukiangalia kuna vijana wengi wanaoshiriki katika biashara ndogondogo unakuta
kuna wajasiliamali wanaongeza thamani ya mazao kama vile korosho, lakini pia
tuna vijana wetu wa bodaboda, bajaji, wavuvi na makundi mengine mengi..”
aliongeza.
Kwa upande
wake, meneja wa mfuko huo kanda ya Kusini, Kwame Temu, alisema lengo kuu la
semina hiyo ni kuwaelimisha wanachama na wadau wa mfuko huo juu ya mafao mapya
ambayo yamezinduliwa likiwamo fao la uzazi na mpango wa Wote Scheme.
Meneja wa PPF kanda ya kusini, Kwame Temu. |
Alisema,
licha ya kuwa kutakuwa na program maalumu ya kukuana na wadau wa sekta zisizo
rasmi hapo baadae lakini wameona ni bora kupitia semina hiyo kutoa elimu juu ya
mafao hayo ambapo aliwataka wanachi wa Mtwara kuchangamkia fursa za kujiunga na
mfuko huo.
Kuhusu suala
la kulipa mafao ya wanachama kwa wakati, alisema mfuko huo umejitahidi
kuboresha huduma zake hasa za Tehama ambapo sasa mwajiri anaweza kutambua
taarifa za mfanyakazi wake akiwa ofisini kwake bila kwenda katika ofisi za PPF
kwa kuingia katika linki atakayo patiwa na mfuko huo.
“Kwahiyo
niseme tu kwamba tumejaribu kupambana na changamoto hiyo ya kumbukumbu na hii
inatuwezesha kulipa mafao yetu kwa wakati kwasababu kama mnavyofahamu siku hizi
ukiweza kuwa katika teknolojia kwa kiwango cha juu na ulipaji unakuwa ni wa
haraka zaidi..” alisema.
No comments:
Post a Comment