Sunday, February 7, 2016

MAWAZO: Viongozi wa Ndanda walinikosea sana.

Aliyekuwa kocha wa Ndanda Fc, Amimu Mawazo.



Na Juma Mohamed, Mtwara.

BAADA ya wiki mbili za kuwa nje ya majukumu ya kukinoa kikosi cha Ndanda Fc ya mkoni hapa inayoshiriki ligi kuu ya Vodacom Tanzania Bara, aliyekuwa kocha wa timu hiyo Amimu Mawazo, ameibuka na kudai kuwa viongozi wa Ndanda walimkosea kwa kufanya maamuzi ya kumuweka pembeni bila kumshirikisha.
Amimu ambaye alipewa majukumu ya kukinoa kikosi hicho kuanzia mwanzoni mwa msimu kwa makubaliano ya kushikilia nafasi hiyo ambaye iliachwa wazi na Jumanne Charles ambaye alikuwa na leseni C  huku waraka wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kwa wakati huo kuwataka makocha wa vilabu vya ligi kuu kuwa na Leseni B za ukocha, alisema viongozi hao hawakupaswa kumficha jambo lolote katika maamuzi yao.
Alisema walipaswa kukaa naye na kumweleza sababu za kuachana naye lakini haikufanyika hivyo na baadala yake alisoma taarifa kupitia vyombo vya habari ikiwa ni pamoja na magazeti yakidai kuwa moja ya sababu ni kuto kubali ushauri kutoka kwa wasaidizi wake katika benchi la ufundi, jambo ambalo alilipinga.
“Mara mwandishi wa Ndanda anaandika vyake kuhusiana na mimi mara gazeti lingine linaandika vitu tofauti kuhusu mimi..sasa mimi nashangaa kwasaabu niliona vitu vingine vinaandikwa mimi sivijui, kwasababu kuna gazeti nimeshawahi kuona limeandika kwamba kwasababu ya kutokubali kushuriwa..lakini mimi ni ‘Technician’ ananishauri nani tena..” alisema.
Alisema kushauriwa katika mpira kupo lakini sio lazima kila ushauri unaopewa ukubaliane nao, unaweza kupokea ushauri lakini unaangalia kama utaona hauna tija basi unaachana nao, na kueleza kuwa unapofanya kazi ya uwalimu wa mpira wa miguu hupaswi kuwa mwoga katika kufanya maamuzi.
Alisema hata kama sababu ilikuwa ni matokeo mabaya ambayo timu ilikuwa ikiyapata katika michezo yake 15 ya mzunguko wa kwanza wa ligi ambapo alishinda mchezo mmoja pekee dhidi ya Coastal Union kwa goli 1-0 na kupata alama 9 katika michezo hiyo 15 ambayo walikwenda sare mara 6 na kupoteza mara 8, alitakiwa kuambiwa kwasababu kazi ya uwalimu suala la kuachishwa kazi sio kitu cha ajabu.
“Mimi nilikuta timu wakati imesajiliwa, labda niwapeni ‘background, sasa timu ikishasajiliwa ule uwezo wa wachezaji unaufahamu vipi, kwahiyo unaanza kufanya kazi kwanza kwa kuwajua majina alafu sasa ndio uanze kazi ya kuufahamu uwezo wa kila mchezaji, baada ya hapo sasa unze kuangalia kila mchezaji anamanufaa katika nafasi gani..kwahiyo matokeo yale mabaya mimi siyakatai kwasababu watu si ndio wanaona..” alisema.
Aidha, aliweka wazi kwamba hana chuki kabisa na timu hiyo ambayo amekuwa nayo kwa kipindi kirefu kuanzia inacheza katika ligi daraja la kwanza ambapo suala la kuingia na kutoka akiwa kama mwalimu ni kawaida kwake kwani ilishawahi kutokea hata wakati timu hiyo ilipoamua kuachana na kocha ambaye aliipandisha daraja na kuifikisha ligi kuu, Denis Kitambi na kuamua kumkabidhi yeye wakati ikitafuta mwalimu mwingine.
Kwahiyo nasema mimi bado ni mpenzi wa timu ya Ndanda, na ni mtu ambaye bado timu ya Ndanda naithamini na sina chuki naye kwasababu timu ya Ndanda haijanikosea hata hili lililofanyika sio timu inawezekana ni mambo tu ya ngazi mbalimbali..” aliongeza.
Amimu ambaye ni mkufunzi wa TFF mwenye Lesi A ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) na Leseni B ya Chama cha Mpira wa Miguu cha Ujerumani (DFB), kabla ya kupewa jukumu la kukinoa kikosi hicho alikuwa mkurugenzi wa ufundi wa timu.
Kwa upande wake, msemaji wa timu hiyo Idrisa Bandari, alisema maamuzi ya kumuondoa Mawazo kwenye nafasi hiyo yalitokana na kikao cha kamati ya utendaji ambacho kilikaa kabla ya mchezo wa Ndanda na JKT Ruvu uliochezwa kwenye uwanja wa Nangwanda Sijaona, na Ndanda kupoteza kwa kufungwa magoli 3-1.
Alisema kamati iliamua kuvunjwa kwa benchi lote la ufundi ambapo maamuzi hayo yalipelekwa kwenye bodi ya wakurugenzi ambao hata hivyo waliamua wavute subira lakini wakati timu ikiwa katika mapumziko mafupi wakati ule michuano ya kombe la mapinduzi ikiendelea visiwani Zanzibar, aliyekuwa msaidizi wa Mawazo, Ngawina Ngawina aliamua kuachia ngazi kwa madai kushinikizwa na mashabiki wa timu hiyo ambao walimshutumu kuwa anaigawa timu na hana maelewano mazuri na mkuu wake.
“Suala la mzee Amimu kama mtakumbuka sisi tuliingia mkataba na mwalimu Jumanne Charles ambaye alikuwa na Leseni C ambayo hata hivyo Shirikisho la Mpira (TFF) walipoleta waraka walitaka mwalimu ambaye anafundisha timu za ligi kuu awe na Leseni B kwahiyo moja kwa moja waraka ule ukamwondoa Jumanne Charles..” alisema na kuongeza:
“Tulichokifanya tukamwomba mzee Amimu aje afanye kazi ile ya kocha mkuu mpaka pale tutakapopata mwalimu..kwahiyo tangu kipindi kile viongozi walikuwa wanahangaika kutafuta mwalimu ambaye atakuja kutusaidia kwenye timu..” aliongeza.
Alisema baada ya mchakato huo wa muda mrefu wa kutafuta mwalimu, timu hiyo ilifanikiwa kuingia makubaliano na mwalimu wa JKU ya Zanzibar, Malale Hamsini ambaye alijiunga na timu ikielekea katika mchezo wake na Mgambo Shooting ya Tanga kabla ya kurejea JKU kuiongoza katika michezo yake ya Kimataifa.

Bandali alibainisha kwamba kamati ya utendaji ilikubaliana kuwa Mawazo arejeshwe katika nafasi yake ya ukurugenzi wa ufundi na alishapelekewa barua ya kuitwa katika majukumu hayo.

No comments: