Waandishi wa habari wa mkoa wa Mtwara wakiwa katika semina ya siku moja ya kujengewa uwezo wa uelewa wa sekta ya Mafuta na Gesi iliyoandaliwa na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania |
Na Juma Mohamed, Mtwara.
SHIRIKA la
Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) limesema lipo kwenye mchakato wa ujenzi wa
mradi wa usambazaji wa gesi asilia kwa ajili ya matumizi ya majumbani,
viwandani na kwenye magari katika mikoa ya Lindi na Mtwara.
Hayo
yamezungumzwa juzi mkoani hapa na meneja wa biashara ya gesi wa shirika hilo,
Emmanuel Gilbert, baada ya kumalizika kwa semina ya siku moja ya kuwajengea
uwezo waandishi wa habari wa Mtwara juu ya uelewa wa sekta ya Mafuta na Gesi
iliyoandaliwa na shirika hilo.
Alisema
tayari upembuzi yakinifu umeshafanyika katika maeneo yatakayopitiwa na mradi
huo na kwamba sasa shirika hilo linasubiri kupatiwa fedha kutoka serikalini kwa
ajili ya kufanya usanifu wa michoro katika maeneo hayo yatakayojengwa
miundombinu hiyo.
Alisema,
licha ya kusubiri pesa hizo jitihada zinazofanywa na shirika kwa sasa ni
kujaribu kuzihusisha sekta binafsi kwa ajili ya kuleta mitaji ambayo itasaidia
kupatikana pesa za kuanza shughuli hiyo.
“Serikali
kama serikali vipaumbele ni vingi, ukisema tu kwamba wanapeleka pesa nyingi
kwenye hii miundombinu kwa ajili ya uwekezaji kwenye hii miundombinu ambayo
inahitaji pesa nyingi kwa ajili ya kuendelezwa..kwahiyo sisi kama TPDC tumekuwa
tukijitahidi sana kuhakikisha kwamba tunawaleta watu wa sekta binafsi ili
waweze kuleta mitaji kwa ajili ya kuendeleza hiyo miundombinu..” alisema.
Alisema,
mradi huo ambao kuanza kwake kunategemea na upatikanaji wa fedha, mtandao wake
wa kutandaza mabomba utakuwa na urefu wa Km 17 kwa mkoa wa Mtwara ambapo
unatarajiwa kuunganisha nyumba 11,000 na magari 4,000 ambayo yatakuwa na
yanauwezo wa kuamua kutumia nishati ya gesi au mafuta, na Km 11 kwa mkoa wa
Lindi.
“Hiyo siyo
‘limit’ kwamba ndiyo mwisho, hiyo project ya kwanza itakapo kamilika na kama
pesa zitaendelea kupatikana mradi utakuwa unapanuka..na niwaambie tu wananchi
wa Mtwara kwamba tunahitaji ‘support’ yao, na yale yaliyotokea nyuma ni kwamba
tu kwasababu ya kukosekana kwa taarifa kwamba upande mmoja ulikuwa na taarifa
na mwingine haukuwa na taarifa na sasa hivi tumejitahidi sana kuhakikisha tuna
‘close’ hiyo ‘gape’..” aliongeza.
Kwa upande
wake, meneja wa utafiti wa shiika hilo, Venosa Ngowi, alisema shirika kwa sasa
lipo katika hatua za kushughulikia ujenzi wa miundombinu katika mtambo wa
kupokea na kuchakata gesi kuibadilisha kutoka kwenye hewa na kuwa katika
kimiminika, ambapo kwa kitaalamu huitwa Liquefied Natural Gas (LNG).
Alisema,
mtambo huo ambao utajengwa katika eneo la Likongo mkoani Lindi na kukamilika
kwake kunatarajiwa kuwa baada ya miaka Minane hadi kumi ambapo utagharimu kiasi
cha dola za kimarekani Billion 30-60.
“Gesi hii
tunaisimika kwenye nyuzi -162 C alafu tunaisafirisha kuipeleka kwenye masoko na
mradi huu ni mkubwa tunafanya pamoja na makampuni ambayo yamegundua gesi
baharini, tunafanya pamoja na Statoil ya Norway, BG pamoja na Ophir Energy.” Alisema.
No comments:
Post a Comment