Saturday, January 30, 2016

Coastal wasitisha rekodi ya Yanga VPL..Simba mwendo mdundo na Mayanja.




Salum Telela wa Yanga (Kushoto) akimtoka mchezaji wa Coastal katika moja ya michezo ya Ligi kuu ya Tanzania Bara. (PICHA: MTANDAO)


Wachezaji wa Simba wakishangilia moja ya magoli yao yalifungwa kwenye mchezo wa leo dhidi ya African Sports

Wachezaji wa Simba wakishangilia moja ya magoli yao yalifungwa kwenye mchezo wa leo dhidi ya African Sports (PICHA: shaffihdauda.co.tz)


Na Juma Mohamed.

TIMU ya soka ya Coastal Union ya Tanga leo imefanikiwa kusitisha rekodi ya mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, Yanga Sc ambao walikuwa hawajawahi kufungwa tangu kuanza kwa msimu huu, baada ya kuichakaza magoli 2-0 katika mchezo uliopigwa katika uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga.
Mchezo huo ulioamuliwa na Endrew Shamba kutoka mkoani Pwani ulikuwa wakushambuliana kwa pande zote huku wenyeji wakionekana kudhibiti vilivyo sehemu ya kiungo cha Yanga na kufanikiwa kupunguza mashambulizi ya mfululizo langoni mwao.
Wauwaji wa Coastal leo walikuwa ni Miraji Adam aliyeandika goli la kwanza kipindi cha kwanza kwa mpira wa adhabu uliokwenda moja kwa moja na kumshinda mlinda lango wa Yanga Deogratius Munish ‘Dida’ huku Juma Mahadhi akipachika goli la pili kipindi cha mchezo kwa shuti kali lililowababatiza walinzi na kumchanganya Dida.
Kupoteza kwa Yanga katika mchezo huo ikiwa ni siku chache baada ya aliyekuwa katibu mkuu wa klabu hiyo Dkt. Damas Tiboroha kubwaga manyanga, inakuwa ni mara ya kwanza toka kuanza kwa msimu huu kwani kabla ya hapo hawakuwahi kupoteza mchezo wowote zaidi ya sare 3 ambazo walizipata.
Coastal sasa wanafikisha alama 13 baada ya kucheza mara 16 wakisogea mpaka nafasi ya 11 na kuipiku Ndanda ambayo ina alama 12 ikiwa inasubiri kushuka dimbani kesho na Mgambo Shooting ya Tanga, huku Yanga ikiendelea kusalia kileleni mwa ligi kwa alama zao 39 sawa na Azam ambao wanawazidi wastani wa magoli ya kufungwa na kufunga baada ya kushuka dimbani mara 16 huku Wanalambalamba wakiwa wameshuka dimbani mara 15.
Beki wa African Sports (kushoto) akimdhibiti Ibrahim Ajib wakati wa mchezo wa Simba vs African Sports
Beki wa African Sports (kushoto) akimdhibiti Ibrahim Ajib wakati wa mchezo wa Simba vs African Sport (PICHA: shaffihdauda.co.tz)
Katika mchezo mwingine uliopigwa leo uwanja wa Taifa Dar es Salaam, Simba wameendeleza wimbi la ushindi baada ya kuisambaratisha African Sports magoli 4-0 ikiwa ni mwendelezo wa matokeo mazuri anayoyapata kocha mpya Jackson Mayanja aliyeshika nafasi ya Dylan Kerry.
Mabao ya Simba leo yamefungwa na Mganda, Hamis Kiiza aliyefunga mawili katika dakika za 14 na 42, Hassan Kessy dk 31 na Haji Ugando aliyepachika la mwisho katika dk 75 na kuifanya Simba kufikisha alama 36 ikisalia katika nafasi ya Tatu baada ya kucheza mara 16.

No comments: