Thursday, December 3, 2015

BG kuchangia vifaa tiba Zahanati ya Shangani, Mtwara.


Mkuu wa wilaya ya Mtwara, Fatma Ally, (Wakwanza kushoto) akiwa na Mkuu wa Ayfa, Usalama, Ulinzi na Mazingira wa BG-Tanzania, Stevenson Murray pamoja na Daktari bingwa wa magonjwa ya kina mama, Dkt. Raphaela Handler, wakati wa kukabidhiana mikataba ya kupatiwa msaada wa fedha za kununulia vifaa tiba kutoka kwa kampuni ya utafutaji na uchimbaji wa mafuta na gesi (BG Tanzania)


Mkuu wa wilaya ya Mtwara, Fatma Ally, (Katikati) akiwa katika picha ya pamoja na viongozi wa kampuni ya BG na wa Zahanati ya Shangani, baada ya kusaini  mikataba ya kupatiwa msaada wa fedha za kununulia vifaa tiba kutoka kwa kampuni hiyo

 Na Juma Mohamed.

UONGOZI wa Zahanati ya kata ya Shangani, manispaa ya Mtwara Mikindani imeingia makubaliano ya kupokea fedha kutoka kampuni ya utafiti na uchimbaji wa gesi na mafuta (BG) kwa ajili ya kununulia vifaa tiba vya magonjwa ya dharula.
Katika mkataba uliosainiwa jana mbele ya mkuu wa wilaya ya Mtwara Fatma Ally na mganga mkuu wa mkoa wa Mtwara, Dkt. Shaibu Maarifa, katika Zahanati hiyo, BG watakabidhi dola za Kimarekani 280,000 ambazo ni zaidi ya sh. Milioni 600.
Akizungumza mara baada ya kusaini mkataba huo, Mkuu wa Ayfa, Usalama, Ulinzi na Mazingira wa BG-Tanzania, Stevenson Murray, alitaja baadhi ya vifaa vitakavyopatikana kutokana na msaada huo kuwa ni pamoja na Gari la wagonjwa (Ambulance) na vifaa vya huduma za afya za dharura zitakazozingatia ajali mbalimbali ikiwemo kung’atwa na nyoka.

Daktari bingwa wa magonjwa ya kina mama katika Zahanati ya Shangani, manispaa ya Mtwara Mikindani, Dkt. Raphaela Handler (Wakwanza kulia) akisaini mkataba kwa ajili ya kupatiwa msaada wa fedha za kununulia vifaa tiba kutoka kwa kampuni ya utafutaji na uchimbaji wa mafuta na gesi (BG Tanzania). kutoka kushoto ni mkuu wa wilaya ya Mtwara, Fatma Ally

Alisema, kampuni hiyo inafanya kazi kwa kushirikiana bega kwa bega na mkoa wa Mtwara na Zahanati hiyo, hivyo ni wajibu kwao kutoa msaada pale panapohitajika kufanya hivyo pamoja na huduma nyingine.
“Kupitia program za uwekezaji kwa jamii, tunapanga mipango ya muda mrefu yenye lengo la kusaidia jamii kukabiliana na changamoto muhimu kwa uendelevu..mipango hii kabambe ya muda mrefu itasaidia kukabiliana na baadhi ya vyanzo vinavyosababisha kutokea kwa hali za dharura.” Alisema.

Kwa upande wake, Mganga mkuu wa kina mama katika Zahanati hiyo, Dkt. Raphaela Handler, alisema msaada huo utasaidia sana kuinua hali ya afya ya jamii kwa kukarabati majengo na kutoa vifaa tiba muhimu, kwani vituo vya huduma za afya ni mahali panaposhughulikia mahitaji ya afya moja kwa moja kwa kuboresha huduma.
“Ninavyoona idadi ya ajali zinazotokana na magari na pikipiki zinazidi kuongezeka kila siku na inafaa sana kuwa na huduma za hali ya juu zaidi ili kwa kuwa na vifaa mbalimbali ili kuweza kuokoa maisha ya wananchi hasa pale wanapopatwa na hali mbaya zaidi..aina ya vifaa ambavyo BG watatupatia havipatikani katika Zahanati au hata hospitali za wilaya, lakini wao watavileta hapa..” alisema.

Mkuu wa wilaya ya Mtwara, Fatma Ally, (Wakwanza kushoto) akiwa na Mkuu wa Ayfa, Usalama, Ulinzi na Mazingira wa BG-Tanzania, Stevenson Murray pamoja na Daktari bingwa wa magonjwa ya kina mama, Dkt. Raphaela Handler, wakati wa kukabidhiana mikataba ya kupatiwa msaada wa fedha za kununulia vifaa tiba kutoka kwa kampuni ya utafutaji na uchimbaji wa mafuta na gesi (BG Tanzania).

Naye, mkuu wa wilaya ya Mtwara, Fatma Ally, akizungumza kwa niaba ya mkuu wa mkoa wa Mtwara, Halima Dengego, aliishukuru BG kwa kutoa msaada huo na kusema kuwa wamekua mstari wa mbele katika kusaidia jamii katika sekta zote muhimu.
“Wamekua wakitoa msaada katika sekta ya afya, elimu, kilimo na hata uvuvi, kwahiyo sisi kama mkoa tunashukuru kwa msaada wao na tunawahamasisha wadau wengine wanapokwenda kufanya kazi na jamii Fulani kuweza kuangalia jamii changamoto zake na kutoa msaada na kuweza kuleta maendeleo zaidi kwenye jamii husika.” Alisema.
BG Tanzania, imedhamiria kujenga uhusiano endelevu na jamii inayowazunguka, na kwamba program za uwekezaji kwa jamii zinatolewa kupitia ushirikiano mkubwa na mashirika yenye utaalamu na kwa kufanya kazi pamoja na serikali na jamii kubainisha maeneo ya kipaumbele na mahitaji ya pamoja.


No comments: