Monday, November 23, 2015

Wananchi manispaa ya Mtwara walia na Mbunge, ukosefu wa ajira.



Mbunge wa Mtwara mjini kupitia Chama cha Wananchi (CUF), Maftaha Nachuma, akizungumza na waandishi wa habari (Hawapo pichani) juu ya namna atakavyotekeleza ahadi zake



Mbunge wa Mtwara mjini, Maftaha Nachuma (CUF) akipokea zawadi za Kimasai kutoka kwa Elizabeth Mboya.



Na Juma Mohamed.

WANANCHI wa Manispaa ya Mtwara Mikindani mkoani hapa wamelalamikia ukosefu wa ajira licha ya uwepo wa kampuni kadhaa za uwekezaji, na kumtaka mbunge wa jimbo hilo Maftaha Nachuma, kushughulikia kero hiyo kwa kuhakikisha zinapatikana fursa nyingi kwa wazawa kuliko wageni.
Wakizungumza juzi baada ya kumpokea mbunge huyo anayewakilisha Chama cha Wananchi (CUF), akitokea Dodoma katika shughuli ya kuapishwa na uzinduzi wa Bunge la 11, walisema kumekuwa na tabia ya kutoa ajira kwa wageni kuliko wenyeji wa mkoani hapa jambo ambalo ni tofauti na inavyoelezwa na baadhi ya viongozi kuwa ajira zitolewe kwa wazawa zaidi ili wanufaike na uwekezaji.
Muhuzuni Chinjaru, ambaye ni mkazi wa Kilimahewa, alisema kumekuwa na propaganda zinazozungumzwa na baadhi ya watu kuwa ukosefu wa ajira kwa wakazi wa Mtwara ni kutokana na kukosa elimu inayoendana na mahitaji ya sehemu husika, akidai kuwa swala hilo sio la kweli na kwamba wananchi wengi wanaelimu na wamejifunza fani mbalimbali.

Maftaha Nachuma akipokea zawadi

“Kwahiyo tunamuomba Mhe. Mbunge asimamie swala la ajira, hakuna ajira Mtwara, makampuni yanakuja Mtwara mengi sana lakini unaona vijana tunakosa ajira..utaona kampuni inahitaji vijana wa Mtwara wapate ajira pale 100, lakini ukiangalia wanaopata ajira ni vijana 20 na 80 wote ni wakuja, sio upendeleo lakini uzawa upo bwana kila mahali..” alisema.
Aidha, alimtaka Mbunge kutatua kero za migogoro ya ardhi ambayo kwa zaidi ya miaka mitatu imekuwa ni changamoto kubwa kwa wananchi hasa wa maeneo ya Kilimahewa, Matangila na Chame ambayo imeshindwa kutatuliwa na viongozi waliopita.
Alimtaka kuhakikisha anainua kiwango cha elimu ambacho kinaaminika kuwa kimeshuka kutokana na hali ya ufaulu inavyoonekana katika mitihani ya watoto wao na kwamba mwanafunzi anamaliza kidato cha nne akiwa hajui kusoma na kuandika.
“swala la elimu alifanyie kazi kwasababu watoto wafika darasa la tano mpaka la saba mpaka wanamaliza kidato cha nne, hajui kuandika wala kusoma na hata kiingereza hakijui..kwahiyo ni kero kubwa sana, mbunge asimamie vizuri na kama yeye fani yake ya ualimu basi asimamie vizuri..” aliongeza.

Waandishi wa habari pamoja na baadhi ya wananchi wa manispaa ya Mtwara waliojitokeza katika kikao cha Mbunge wa jimbo hilo, Maftaha Nachuma-CUF juu ya kutekeleza ahadi zake pamoja na kuwashukuru wananchi waliomchagua

Naye, Rahma Mtipa, alisema wananchi wanaimani na mbunge huyo kuwa atatekeleza yote aliyoahidi wakati wa kampeni zake za kuomba kura lakini zaidi ni kuwawezesha wanawake kwa kuwapatia fursa mbalimbali zitakazowasadidia kupiga hatua kimaendeleo na kuacha kuwa tegemezi.
“Na kama wanavyosema elimu bure basi tunaomba iwe bure kweli ili watoto wetu wahepuke kuwa wadhurulaji wa mitaani..atuwezeshe kuunda vikundi ili tuseme vikundi hivi vimewezeshwa na mbunge, kwahiyo na sisi tunamuomba atuhamasishe sisi wanawake tuunde vikundi vyetu tuweze kujiajiri wenyewe..” alisema.
Awali akizungumza na waandishi wa habari, Mbunge huyo alisema atahakikisha anatumia fedha za mfuko wa jimbo kutatua kero mbalimbali wanazokumana nazo wananchi katika maeneo tofauti ikiwa ni pamoja na kujenga sehemu ya kupumzikia wauguzi katika Hospitali ya Rufaa ya Ligula, kununua magari ya kubebea wagonjwa (Ambulance) na magari ya kubeba wanafunzi.

Elizabeth Mboya

“Tunalo tatizo la Ambulance kwenye Hospitali zetu, hatuna Ambulance kule Hospitali ya Likombe, hatuna Ambulance Ligula (ipo) wala Mikindani, tutatumia fedha za Jimbo na nimshukuru tu Mhe. Rais kwamba wakati anahutubia Bunge alisema safari hii ataongeza fedha ya Jimbo ili sisi wabunge tuweze kushirikiana naye katika kutatua changamoto zinazowakabili wananchi..” alisema Maftaha.
Kuhusu changamoto ya miundombinu mibovu iliyopo katika Manispaa ya Mtwara inayopelekea wananchi kukumbwa na Mafuriko wakati wa mvua kubwa, alisema atajitahidi kushirikiana na Manispaa kutatua tatizo hilo huku akiahidi kwenda kuhoji kuhusu ujenzi wa mradi wa mfereji mkubwa wa kupeleka maji baharini kujua ujenzi wake umefikia hatua gani.




No comments: