Friday, November 20, 2015

DC Mtwara ataka wahalifu wa uvuvi haramu kuongezewa adhabu.

Mkuu wa wilaya ya Mtwara, Fatma Ally.


Na Juma Mohamed.

MKUU wa wilaya ya Mtwara, Fatuma Ally, ameshauri serikali kufanya marekebisho ya adhabu zilizoainishwa katika vifungu vya sheria za makosa ya uvuvi haramu ili kuweza kudhibiti tatizo hilo ambalo linaonekana kuwa sugu katika baadhi ya maeneo yanayojihusisha na shughuli hiyo.
Akizungumza juzi mkoani hapa katika semina ya kujenga uelewa juu ya athari za uvuvi unaotumia milipuko kwa Maofisa wanaoshiriki katika uchunguzi, mashitaka na hukumu za kesi zinazohusu uvuvi huo iliyoandaliwa na Baraza la Mazingira la Taifa (NEMC), alisema hiyo imekua ni moja ya changamoto inayoikabili sekta hiyo kutokana na sheria zilizopo kutotoa adhabu kali kwa waalifu.
“Adhabu zilizoanishwa kwenye sheria ya makosa ya uvuvi haramu ni ndogo, yani hazina uzito sana kwahiyo zinamfanya muhalifu kutoogopa kwasababu anajua ataadhibiwa kwa adhabu ndogo na kuendelea na shughuli yake..kwahiyo labda tushauri tu kwamba zitolewe adhabu kali kwa makosa ya uvuvi haramu..” alisema.
Alisema, changamoto nyingine katika kukabiliana na uvuvi haramu ni ushiriki mdogo kwa jamii katika utoaji wa taarifa kwa serikali kwa kuhofia usalama wao kutoka kwa baadhi ya wahalifu, ambapo hiyo inatokana na kuishi pamoja na wahalifu ambao wengine ni ndugu.
Alisema, wapo wanaotoa taarifa kwa simu kwenda kwa vyombo vya usalama juu ya kinachoendelea katika maeneo yao lakini wakifika kwa lengo la kutaka kupata undani wa kilichotokea inakua ngumu kupata ushirikiano.
“Ukiwa mbali watakutumia massage (ujumbe) Mhe. Huku kuna hiki na hiki lakini ukifika pale kwenye eneo ushirikiano hupati tena, watakudanganya tu lakini ukweli ni wenzao na wako nao kwasababu tunavyokaa huko vijijini tunaowana basi utakuta ni shemeji yake..lakini tuna changamoto nyingine ya umasikini sasa unakuta hii hali ya kipato kuwa duni unakuta viongozi nao muda wao wa ziada wanashiriki katika uvuvi haramu..” alisema.
Aidha, alivitaka vyombo husika kujitahidi kwenda vijijini kuwaelimisha wananchi waweze kuachana na dhana potofu kwamba mapambano dhidi ya uvuvi haramu ni jukumu la serikali na vyombo vyake, na baadala yake waamini kwamba mtu wakwanza anayeweza kufahamu wahalifu ni mwananchi wa eneo husika.

Semina hiyo imekuja ikiwa ni wiki moja baada jeshi la polisi mkoani hapa kuwakamata watu watatu kutokana na kukutwa na vifaa mbalimbali vya milipuko vinavyotumika katika uvuvi haramu wa kutumia baruti katika bahari ya Hindi, katika oparesheni maalumu ya kuwakamata wanaojihusisha na mtandao huo.

No comments: